KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 21, 2010

SIMBA YAIPUMULIA YANGA

Na Mwandishi Wetu, Mwanza
SIMBA jana ilizunduka katika michuano ya soka ya ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kuicharaza AFC mabao 3-1 katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.
Kwa matokeo hayo, Simba bado inashika nafasi ya pili katika msimamo wa ligi hiyo, ikiwa na pointi 18 baada ya kucheza mechi nane, nyuma ya vinara Yanga wanaoongoza kwa kuwa na pointi 19.
Yanga inaweza kuongeza tofauti ya pointi kati yake na Simba iwapo itaishinda JKT Ruvu leo katika mechi nyingine ya ligi hiyo, itakayochezwa kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.
Simba ingeweza kuifunga AFC mabao mengi zaidi, hasa kipindi cha pili, lakini papara za washambuliaji wake, Emmanuel Okwi, Mussa Hassan ‘Mgosi’ na Patrick Ochan zilikuwa kikwazo.
Pambano hilo halikuwa na mvuto katika kipindi cha kwanza kutokana na timu zote kucheza soka ya kiwango cha chini na kushindwa kugongeana pasi za uhakika.
Iliwachukua Simba dakika tatu kuhesabu bao la kwanza lililofungwa na Hillary Echesa kwa mpira wa adhabu baada ya Emmanuel Okwi kuangushwa na beki mmoja wa AFC nje kidogo ya eneo la hatari.
Dakika tano baadaye, Jerry Santo aliiongezea Simba bao la pili baada ya kumalizia pasi maridhawa aliyotanguliziwa na Amri Kiemba.
AFC ilipata nafasi nzuri ya kufunga bao dakika ya 25 wakati Abdalla Juma alipofumua shuti kali la umbali wa mita 20, lakini kipa Juma Kaseja alilipangua na kuwa kona isiyokuwa na matunda.
Dakika ya 28, Ochan alitengenezewa pasi safi na Haruna Shamte na kubaki ana kwa ana na kipa Azizi Simon, lakini shuti lake lilitoka pembeni ya lango.
Okwi aliipotezea Simba nafasi nyingine nzuri ya kufunga bao dakika ya 33 baada ya kuwatoka mabeki wawili wa AFC, lakini shuti lake lilitoka nje.
AFC ilijibu mapigo dakika ya 45 baada ya Bakari Kigodeko kupewa pasi na kubaki uso kwa uso na kipa Kaseja wa Simba, lakini shuti lake lilitoka nje. Timu hizo zilikwenda mapumziko Simba ikiwa mbele kwa mabao 2-0.
Mchezo ulichangamka katika kipindi cha pili baada ya AFC kupata bao la kujifariji dakika ya 54. Bao hilo lilifungwa na mshambuliaji Jimmy Shoji baada ya kuunganisha wavuni kona iliyochongwa na Kigodeko.
Dakika 10 baadaye, Mgosi aliiongezea Simba bao la tatu, kufuatia kazi nzuri iliyofanywa na Okwi na Azizi Gilla waliogongeana pasi nzuri pembeni ya uwanja kabla ya kutoa pasi kwa mfungaji.
AFC ilipata pigo dakika ya 71 baada ya beki wake, Amri Msumi kutolewa nje kwa kadi nyekundu kwa kosa la kumchezea rafu mbaya Okwi. Awali, Msumi alikuwa ameonyeshwa kadi ya njano.
Pamoja na kucheza ikiwa pungufu, AFC ilipata nafasi mbili nzuri za kufunga mabao dakika ya 83 na 86, lakini zilipotezwa na Abdallah Juma na Shoji baada ya mashuti yao kuokolewa na kipa Kaseja.
Papara za Mgosi na Okwi ziliikosesha tena Simba bao dakika ya 90 baada ya kutokea piga nikupige kwenye lango la AFC. Shuti la kwanza la Mgosi lilimbabatiza kipa Azizi Simon wa AFC na lile la pili la Okwi lilitoka nje.
Simba: Juma Kaseja, Haruna Shamte, Juma Jabu, Kevin Yondani, Juma Nyoso, Hillary Echesa/ Mussa Mgosi, Jerry Santo, Amri Kiemba/Azizi Gilla, Rashid Gumbo, Patrick Ochani, Emmanuel Okwi.
AFC: Azizi Simon, Simon Mganga/Zahor Jairani, Andrew Carlos, Amri Msumi, Mohamed Upatu, Razaki Muhidin, Abdalla Juma, Kiworu Francis/Simon Nsajigwa, Juma Shoji, Bakari Kigodeko, Hilali Bigwa.

No comments:

Post a Comment