KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, October 17, 2010

PAPIC: Safari bado ndefu


KOCHA Mkuu wa Yanga, Kostadin Papic amesema licha ya timu yake kuibwaga Simba, bado safari ya kutwaa ubingwa wa ligi kuu ya Tanzania Bara ni ndefu.
Papic alisema hayo juzi, muda mfupi baada ya Yanga kuichapa Simba bao 1-0 katika mechi ya ligi hiyo, iliyochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini hapa.
Kocha huyo kutoka Serbia alisema, licha ya timu yake kuibuka na ushindi, haikucheza vizuri na atalazimika kuzifanyiakazi dosari kadhaa zilizojitokeza katika mchezo huo.
Alisema kilichoiwezesha timu yake kuibuka na ushindi ni bahati aliyonayo kwa Yanga, lakini alikiri kuwa, wapinzani wao walicheza vizuri zaidi na kupata nafasi nyingi za kufunga mabao.
“Tumeshinda, lakini timu yangu haikucheza vizuri ikilinganishwa na Simba. Kilichotuwezesha kushinda ni bahati na kuitumia vyema nafasi tuliyopata kufunga bao,”alisema.
Naye mshambuliaji Jerry Tegete, aliyeifungia Yanga bao hilo la pekee alisema, kumtungua kipa Juma Kaseja ni kitu cha kawaida katika maisha yake ya soka.
Akizungumza baada ya mchezo huo, Tegete alisema Kaseja ni kipa wa kawaida na hana jipya ama uwezo wa kuiokoa timu yake isifungwe kama anavyofikiriwa na mashabiki wengi.
"Mimi naona kawaida na wala sina dawa yoyote bali ni soka tu," alisema mchezaji huyo anayeongoza kwa kufunga mabao matano katika ligi kuu ya msimu huu baada ya Yanga kucheza mechi saba.
Tegete pia alitangaza hali ya hatari kwa wapinzani wao wote wa ligi hiyo, ambapo alisema kila timu watakayocheza nayo, watailamba mabao na salamu hizo zimeanzia kwa Simba.
Wakati huo huo, baba mzazi wa mchezaji huyo, John Tegete amesema amekoshwa na mtoto wake kwa kufunga bao katika mechi ya watani wa jadi, lakini alimtaka asibweteke na mafanikio hayo.
"Hakuna siku, ambayo nimefurahi kama leo, mwanangu kufunga goli ni mafanikio kwake, zawadi ninayompa ni kumuongezea upendo kwa sababu ndio kitu cha msingi katika maisha ya mtoto," alisema.
John Tegete ndiye meneja wa uwanja wa CCM Kirumba wa Mwanza na inaaminika ni mnazi wa kutupwa wa Yanga. Pia aliwahi kuchezea timu ya Pamba kabla ya kustaafu soka.

No comments:

Post a Comment