KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 14, 2010

SIMBA: Tupo Gado!


KLABU ya Simba imetamba kuwa, haina wasiwasi na pambano lao la ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Yanga, litakalochezwa keshokutwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.
Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, kikosi chao kimekamilika katika kila idara na kimejiandaa vyema kwa pambano hilo.
Kaburu alisema mchezaji mwingine aliyekuwa majeruhi, kipa Ali Mustafa ‘Barthez’, amesharipoti kambini mjini Mwanza baada ya kupona maumivu yaliyokuwa yakimsumbua.
Makamu Mwenyekiti huyo alisema, nahodha Nico Nyagawa alitarajiwa kujiunga na kambi ya timu hiyo jana, ambayo imekuwa ikifanya mazoezi asubuhi na jioni kwenye Uwanja wa CCM Kirumba.
Alisema wachezaji pekee, ambao hawapo kambini ni beki Salum Kanoni na mshambuliaji, Uhuru Selemani wanaoendelea kupatiwa matibabu mjini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Kaburu, baadhi ya viongozi wa klabu hiyo pamoja na wanachama wa kundi la Friends of Simba wanatarajiwa kuwasili Mwanza kesho kwa ndege kwa ajili ya kuongeza nguvu kwenye timu hiyo.
Kaburu alisema, mara baada ya kutua Mwanza, kundi hilo la viongozi na wanachama hao watakutana na wachezaji kwa ajili ya kupanga mikakati ya ushindi katika mechi hiyo.
Naye Ofisa Habari wa Simba, Clifford Ndimbo alitamba kuwa, maandalizi yote muhimu kwa ajili ya mechi hiyo yamekamilika na kinachosubiriwa na kuwashikisha adabu wapinzani wao.
Wakati huo huo, habari zilizopatikana jana jioni zilieleza kuwa, mchezaji Mussa Hassan ‘Mgosi’ ameumia mazoezini na anapatiwa matibabu kwenye hospitali ya Sekou Toure ya mjini Mwanza.

No comments:

Post a Comment