KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 21, 2010

BITEBO: Simba, Yanga zinashusha kiwango cha Stars

Na Mwandishi Wetu, Mwanza
MWANASOKA wa zamani wa timu ya Pamba ya Mwanza, Khalid Bitebo, amesema klabu za Simba na Yanga zimekuwa zikichangia kushuka kwa kiwango cha timu ya taifa, Taifa Stars.
Akizungumza mjini hapa mwishoni mwa wiki iliyopita, Bitebo alisema uamuzi wa klabu hizo kongwe nchini kusajili wachezaji wengi wa kigeni, ndio unaosababisha kiwango cha Taifa Stars kushuka.
Bitebo, ambaye enzi zake alikuwa maarufu kwa jina la Zembwela alisema, kuwepo kwa wachezaji wengi wageni katika klabu hizo kunawanyima nafasi wanasoka wazalendo kuonyesha vipaji vyao.
“Mimi siku zote huwa nasema, Simba na Yanga ndio mhimili wa soka ya Tanzania. Klabu hizi mbili ndizo zinazotoa wachezaji wengi wa Taifa Stars, hivyo zinaposajili wachezaji wengi wa kigeni, zinawanyima nafasi wanasoka wazalendo kuonyesha vipaji vyao,”alisema.
Aliongeza kuwa, japokuwa wanasoka wa kigeni wanasaidia kuleta ushindani katika ligi, lakini wingi wao ndani ya Simba na Yanga unashusha ari ya wanasoka wazalendo.
Mkongwe huyo wa soka alisema ni vyema viongozi wa Simba na Yanga wabadili mwelekeo kwa kutoa kipaumbele zaidi katika kusajili wachezaji wazalendo badala ya wageni.
Bitebo pia alieleza kushangazwa kwake na kiwango duni cha soka kilichoonyeshwa na timu za Simba na Yanga zilipomenyana katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara iliyochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita.
Alisema kutokana na ukongwe wa timu hizo, uwezo zilionao kifedha na pia kuundwa na wanasoka wengi wageni, Simba na Yanga hazikupaswa kuonyesha kiwango duni.
Katika mechi hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Yanga iliichapa Simba bao 1-0 na kuendeleza rekodi ya ushindi kwa watani wao hao.

No comments:

Post a Comment