KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, October 27, 2010

Mwasiti kufyatua albamu mpya


BAADA ya ukimya wa muda mrefu, msanii Mwasiti Almasi ameibuka na kusema anatarajia kudondosha albamu yake mpya mara baada ya kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Mwasiti alisema albamu yake hiyo itakuwa na vibao vinane, kikiwemo ‘Si kisa pombe’ alichokiimba kwa kumshirikisha rapa Quick Racka.
Albamu hiyo itakuwa ya pili kwa Mwasiti tangu alipoanza kung’ara katika muziki wa kizazi kipya, kutokana na tungo zake zenye mvuto na pia sauti maridhawa. Albamu yake ya kwanza inajulikana kwa jina la ‘Niambie’.
"Kwa sasa najiandaa kufyatua albamu yangu mpya ya pili, ambayo itakuwa na nyimbo nane na nimezirekodi kwenye studio tatu tofauti,” alisema mwanadada huyo.
Alizitaja studio alizorekodi vibao hivyo kuwa ni Ngoma Records, Fishcrab ya Lamar na Sound Crafters ya Enrico.
Licha ya maandalizi kuachia albamu hiyo kuendelea vyema, Mwasiti alisema hadi sasa bado hajaamua aiite jina gani kwa vile lengo lake ni kutafuta jina litakalowavuta mashabiki baada ya kuingia sokoni.
"Jina ndo bado naendelea kulitafuta, isipokuwa kila kitu kinaendelea vyema. Natumaini kila kitu kitakamilika mwezi ujao," alisema.
Mwanadada kutoka kundi la THT, alianza kutamba mara baada ya kuachia wimbo uliotamba wa 'Haooo' kabla ya kufyatua vibao vingine kama vile 'Niambie,' 'Huruma' na 'Nalivua pendo'.

No comments:

Post a Comment