KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 21, 2010

Niliandika usia nikiwa kitandani-Cherly Cole



LONDON, England
MWANAMUZIKI nyota wa Uingereza, Cherly Cole amefichua kuwa, aliandika usia juu ya kifo chake akiwa kitandani baada ya madaktari kumweleza kwamba, alikuwa hatarini kupoteza maisha kutokana na kuugua ugonjwa wa malaria.
Cherly (27), mke wa zamani wa beki Ashley Cole wa klabu ya Chelsea ya England amesema, alipewa saa 24 za kuendelea kuishi wakati alipokuwa akipambana na ugonjwa huo miezi minne iliyopita.
Mwanamuziki huyo wa kundi la zamani la muziki la Girls Aloud, amefichua hayo alipokuwa akihojiwa na kituo kimoja cha televisheni cha Uingereza kuhusu maisha yake.
“Niliandika usia juu ya kifo changu nikiwa kitandani,”alisema Cherly wakati wa mahojiano hayo.
Katika mahojiano hayo yaliyodumu kwa saa mbili, mwimbaji huyo pia alizungumzia kwa uwazi kuhusu kuvunjika kwa ndoa yake na Ashley Cole na kusisitiza kuwa, siku zote bado ataendelea kumpenda.
Alisema kuvunjika kwa ndoa yao kuliufanya moyo wake usononeke, lakini bado anamuheshimu na kumpenda mwanasoka huyo, ambaye pia anachezea timu ya taifa ya England.
Cherly alidokeza kuwa, bado amekuwa akiwasiliana mara kwa mara na Cole, licha ya kumsaliti katika kipindi cha miaka mitatu na nusu ya ndoa yao. Wanandoa hao walitengana rasmi Septemba mwaka huu.
Mwanadada huyo alidondokwa na machozi aliposema kuwa, bado anaamini Cole alikuwa mwanaume mwaminifu na kuongeza: “Kwa vile tumeshalimaliza tatizo hili, natumaini tunaweza kuwa tena marafiki. Siku zote nitaendelea kumpenda Ashley.”
“Nikitazama nyuma tulikotoka, najihisi kama niliyeganda. Tulikuwa na ndoa nzuri na yenye furaha na siku ya harusi yetu, ilikuwa ya aina yake, lakini sielewi nini kilichotokea. Hadi sasa, bado najiuliza swali hilo,”alisema mwanamuziki huyo.
Cherly, mzaliwa wa mji wa Newcastle wa Uingereza, alishindwa kushiriki katika maandalizi ya kipindi cha X Factor, kufuatia kuugua malaria Julai mwaka huu. Alijiunga na kipindi hicho mwishoni mwa wiki iliyopita kilipoanza kuonyeshwa laivu baada ya kuonekana yupo fiti.
Wakati wote wa mahojiano hayo, Cherly alikuwa karibu na mama yake mzazi, Joan pamoja na wanamuziki wenzake wa kundi la Girls Aloud, Kimberley Walsh na Nicola Roberts, ambao walitokwa machozi alipokuwa akizungumzia ugonjwa wa malaria.
Kwa mujibu wa Cherly, madaktari walimweleza kwamba alikuwa hatarini kufa baada ya kupatwa na ugonjwa huo alipokuwa ziarani nchini Tanzania.
Alikiri kwamba, alikunywa chupa tatu za vodka usiku, siku moja kabla ya kupiga picha za ziara yao nchini Tanzania na kujihisi kama aliyelewa kupita kiasi. Alisema huo ulikuwa ndio mwanzo wa kuugua kwake malaria.
Cherly alikiri kuwa, ni wakati alipokuwa akiugua ugonjwa huo, ndipo alipoamua kuandika wosia na kufikiria jinsi ya kugawanya mali zake kwa rafiki na familia yake.
“Nilifikiri ningekufa. Ukweli ni kwamba, nilifikiri nilikuwa nikikaribia kufa. Nilifikiri kama nilikaribia kufa, nataka nife haraka kwa sababu nilikuwa kwenye maumivu makali,”alisema.
Cherly, ambaye aliingiza pauni milioni 1.2 za Uingereza kutokana na vipindi vilivyopita vya X Factor, pia alizungumzia uhusiano wake na Simon Cowell.
“Ni mmoja wa watu muhimu katika maisha yangu,”alisema Cherly.
Hata hivyo, Cherly alikiri kuwa, kwa sasa, hapati nafasi ya kujihisi mwanamke wa kawaida kama ilivyokuwa zamani. “Baadhi ya wakati najihisi kama niliye mtegoni,”alisema Cherly. “Siwezi kurudi Newcastle na kuvaa suti za michezo na raba.
Katika hatua nyingine, Cherly ametunga wimbo unaoelezea maisha ya ndoa kati yake na Ashley Cole na yaliyojitokeza baada ya ndoa hiyo kuvunjika. “Niliuza almasi zote na kuchoma moto nguo zako zote,” ameimba Cherly katika moja ya beti za wimbo huo, alioupa jina la ‘Happy Tears’.
Maneno mengine yaliyomo kwenye wimbo huo ni kama ifuatavyo:
‘Nililia wakati niliposikia umetembea nje ya ndoa Nililia wakati niliposema naondokaNilikata nywele zangu na kuchora vidole gumba vyanguNililia wakati suti yako iliposhika motoNililia wakati moyo wangu uliposhindwa kuaminiLakini sasa sitokwi tena na machozi’
Wimbo huo ni miongoni mwa vibao vipya vya mwanamuziki huyo vilivyomo kwenye albamu yake ya ‘Messy Little Raindrops’, inayotarajiwa kuingia sokoni Novemba Mosi mwaka huu.
Katika albamu hiyo, Cherly ameonyesha uwezo mkubwa wa kuimba kwa hisia kali na imeelezwa kuwa, mahojiano yake na televisheni moja ya Uingereza huenda yakamsaidia kuongeza mauzo.
Cherly alisema, anataka albamu yake hiyo iwe na mvuto wa aina yake kwa mashabiki na ndio sababu kava yake imetengenezwa kwa utaalamu wa hali ya juu.
“Naifurahia albamu hii, lakini siwezi kuweka wazi kila kitu hadi wakati utakapowadia,”alisema mwanamuziki huyo mwenye mvuto na kuongeza kuwa, japokuwa hakuandika mashairi ya nyimbo zake yeye mwenyewe, lakini aliyapitia na kuridhika nayo.
Kibao kingine kilichomo kwenye albamu hiyo ni pamoja na ‘Promise This’, ambacho kimeshaanza kushika chati kwenye vituo mbalimbali vya radio na televisheni nchini Uingereza. Cherly anaamini ataongeza umaarufu wa kibao hicho wakati atakapofanya onyesho kwenye kipindi cha X Factor kitakachorushwa hewani Oktoba 24 mwaka huu.
000000

No comments:

Post a Comment