KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 21, 2010

Jokha Kassim aipua albamu yake binafsi


MWIMBAJI nyota wa muziki wa taarab nchini, Jokha Kassim amekamilisha kazi ya kurekodi albamu yake binafsi, inayokwenda kwa jina la ‘Acha nijishebedue’.
Akizungumza mjini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita, Jokha alisema albamu hiyo itakuwa na vibao vinne, ambavyo alijigamba kuwa ni moto wa kuotea mbali.
Alivitaja vibao hivyo kuwa ni ‘SMS za nini’, ‘Kinyang’anyiro’, ‘Kelele za mlango’ na ‘Acha nijishebedue mke mwenzangu anijue’.
Uamuzi wa Jokha, mwimbaji wa kundi la Five Stars Modern Taraab kurekodi albamu hiyo, umekuja wakati mwimbaji mwenzake, Isha Ramadhani ‘Mashauzi’ akiendelea kutesa na albamu yake ya ‘Mama nipe radhi’.
Isha alirekodi albamu hiyo mapema mwaka huu na hadi sasa vibao vyake kama vile ‘Mama nipe radhi’, ‘Tugawane ustaatabu’ na ‘Kila mtu na mtuwe’ vikishika chati kwenye vituo mbalimbali vya radio na televisheni nchini.
"Nimeamua kutoka na albamu yangu ili kuonyesha kipaji na uwezo wangu katika fani hii ya uimbaji wa taarab. Naamini albamu hii itashika vilivyo,"alijigamba Jokha.
Mwimbaji huyo mwenye sauti yenye mvuto na sura jamali alisema, albamu hiyo inatarajiwa kuingia sokoni hivi karibuni na kuwataka mashabiki wake wajiandae kupata uhondo babu kubwa.
Jokha alisema uzinduzi wa albamu hiyo utafanyika katika jiji la Dar es Salaam na utasindikizwa na baadhi ya waimbaji nyota wa muziki huo nchini, wakiwemo Khadija Omar Kopa na Isha Mashauzi.
Kabla ya kujiunga na Five Stars Modern Taarab, Jokha aliwahi kutamba katika vikundi vya Zanzibar Stars, East African Melody na Jahazi.
Baadhi ya vibao vilivyomweka kwenye chati ya juu katika muziki wa taarab ni pamoja na 'Utakufa nacho’, ‘Alonacho kajaaliwa’, ‘Mtenda akitendewa’ na ‘Aso mtu ana Mungu’.
Katika hatua nyingine, kundi la muziki wa taarab la Five Stars linatarajiwa kufyatua albamu mbili kwa mpigo mwishoni mwa mwezi huu.
Rais wa kundi hilo, Ally Jay alisema wiki hii kuwa, maandalizi yote muhimu kwa ajili ya uzinduzi wa albamu hiyo, utakaofanyika kwenye ukumbi wa klabu ya Msasani, Dar es Salaam, yamekamilika.
Alizitaja albamu hizo kuwa ni ‘Shukrani kwa mpenzi’ na ‘Ndio basi tena’, ambazo alitamba kuwa, zitakuwa moto wa kuotea mbali kutokana na mpangilio wa ala na mashairi.
Jay alisema uzinduzi wa albamu hizo utasindikizwa na waimbaji mahiri wa muziki huo nchini, akiwemo Fatuma Binti Baraka (Bi Kidude), Hashimu Saidi na kundi la Offside Trick 'Wazee wa Bata' kutoka Zanzibar.
Kiongozi huyo wa Five Stars alisema, mashabiki watakaohudhuria uzinduzi huo, watazawadiwa zawadi mbalimbali, zikiwemo kanda za kaseti zenye nyimbo zilizomo kwenye albamu hiyo. Kundi la Five Stars lilizinduliwa Juni mwaka jana na hivi sasa linatamba kwa albamu yao ya kwanza, inayojulikana kwa jina la 'Riziki mwanzo wa chuki'.

No comments:

Post a Comment