KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, June 30, 2014

MBRAZIL WA YANGA WE ACHA TU


Andrey Coutinho akisaini mkataba wa kuitumikia Yanga kwa kipindi cha miaka miwili mbele ya Katibu Mkuu Beno Njovu leo makao makuu ya klabu


Kiungo mshamabuliaji Andrey Marcel Ferreira Coutinho raia wa Brazil leo amesaini mkataba wa miwili kuitumikia timu ya Young Africans kwa ajili ya michuano mbalimbali ikiwemo ya Ligi Kuu ya Vodacom pamoja na mashindano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika.

Katibu mkuu wa Young Africans Bw Beno Njovu amesema usajliwa mchezaji Coutinho ni sehem ya muendelezo wa maandalizi ya msimu mpya wa Ligi Kuu na kama ilivyokawaida wao mambo yao ni kimyakimya.

Coutinho ambaye alizaliwa tarehe 12 Januari 1990 amekulia kwenye mji wa Berem ambapo alianza kucheza soka la kulipwa katika klabu ya Paysandu Sports Club kabla ya kwenda nchini Asia katika nchi ya Myanmar katika klabu ya Rukhapura United.

Mpaka anajiunga na klabu ya Young Africans Andrey Coutinho alikuwa akichezea timu ya Castanhal EC iliyopo kwenye Ligi Daraja la pili ambao aliweza kuichezea kwa michezo yote ya mzunguko wa pili mwaka 2014.

Katika hatua nyingine kikosi cha Young Africans kinatarajia kuendelea na mazoezi kesho chini ya kocha Marcio Maximo katika ufuke wa Coco Beach ikiwa ni siku yake ya kwanza na jioni katika Uwanja wa Bandari Tandika kuanza kazi baada ya leo kuwa na mkutano wa ndani na wachezaji wake pamoja na benchi la ufundi.

MAXIMO AAHIDI MAKUBWA YANGA



Kocha Mkuu mpya wa Yanga SC Marcio Maximo (kushoto) akiongea na waandishi wa habari makao makuu ya klabu ya Yanga, kulia ni msaidizi wake Leonado Neiva


Kocha mbrazil Marcio Maximo leo amesaini mkataba wa miaka miwili kwa ajili ya kuwatumikia Mabingwa mara 24 wa Ligi Kuu ya Vodacom timu ya Young Africans pamoja na msaidizi wake Leonadro Neiva ambao wamesema wamekuja kuisaidia Yanga iweze kufanya vizuri kwenye michuano mbalimbali.

Akiongea na waandishi wa habari makao makuu ya klabu ya Yanga, Maximo amesema anajiskia furaha sana kurudi kufanya kazi Tanzania, kwani watu wake ni wakarimu, wapenda mpira hivyo anaona kama yupo nyumbani japo awamu hii ni kwa majukumu ya ngazi ya klabu tofauti na awali alipokua ngazi ya Taifa.

Nimekuja kufanya kazi na Yanga, nawashukuru viongozi wake kwa kuamua kuniamini na kunipa nafasi hii, wamenifuatilia kwa awamu tatu mfululizo na hatimaye safari hii wamefanikiwa kunipata kwa kushirikiana na wakala wangu Ally Mlei sasa kazi ni moja tu kuijenga Yanga.

"Jumatatu naanza kazi moja kwa moja pamoja na msaidizi wangu Neiva kwa kushirikiana na kocha wa kikosi cha U-20, wachezaji waliopo na wachezaji wa kikosi cha U20 watakua wakifanya mazoezi pamoja alisema" Maximo".

Natambua tuna wachezaji wengi katika timu za Taifa mbalimbali ikiwemo ya Tanzania (Taifa Stars), Uganda (The Cranes) na Rwanda (Amavubi) ambao wapo wanayatumikia mataifa yao, na punde watakapomaliza majukumu hayo wataungana nasi kwa maandalizi.

Kuhusu Kaseja yale yalishapita, najua ni kipa mzuri mwenye uwezo na uzoefu wa kutosha na kipindi hiki najivunia kuwa na makipa watatu wenye uwezo mzuri, Yaliyopita Yameshapita yalikuwa ni timu ya Taifa na sasa tumekutana Yanga kazi yetu ni moja tu kuifanya klabu iwe kwenye hadhi ya Kimataifa zaidi.

Naye kocha msaidizi Leonado Neiva amesema tumekuja kufanya kazi, kwa kushirikiana na wachezaji waliopo kutoka sehem mbambali barani Afrika na Amerika tutapata mchanganyiko mzuri wa uchezaji.

Wakala wa Maximo Barani Afrika Bw Ally Mlehi kwa upande wake amewaomba wapenzi, wanachama na washabiki wa Yanga kuwa wavumilivu kwani soka ni tofauti ni chai ambayo ukikoroga sukari tu unasikia utamu, badala yake wanapaswa kuwapa muda makocha na baadae wataaona matunda yake

AVEVA MWENYEKITI MPYA SIMBA, KABURU MAKAMU MWENYEKITI




Na Samira Said, DAR E SALAAM

RAIS mpya wa Klabu ya Simba ya jijini Dar es Salaam, Evans Aveva, amesema kwamba anawaahidi wanachama wa klabu hiyo waliomchagua hatawaangusha baada ya kumpa ridhaa ya kuwaongoza katika kipindi kingine cha miaka minne atakayokaa madarakani kwa mujibu wa katiba.

Aveva alifanikiwa kuibuka mshindi katika uchaguzi huo ambao awali ulizingirwa na 'mizengwe' mbalimbali hadi kufikia kusimamishwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) wakati wa mchakato wake kwa kupata kura 1,455 dhidi ya mpinzani wake aliyekuwa anaungwa 'mkono' na wafuasi wa Michael Wambura, aliyeenguliwa, Andrew Tupa, aliyepata kura 388

Akizungumza muda mfupi baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa nafasi hiyo katika uchaguzi uliofanyika jana Jumapili kwenye Ukumbi wa Bwalo la Maafisa wa Polisi Oysterbay jijini, Aveva, alisema kuwa anafahamu kazi yake anayotakiwa kuifanya akiwa madarakani ambayo wanachama wa Simba imewaumiza kwa kipindi cha miaka minne iliyomalizika.

Aveva alisema kwamba atahakikisha anavunja makundi yaliyopo katika klabu hiyo ili kuleta umoja, ushirikiano na mshikamano ndani ya klabu hiyo na anafahamu wazi makundi hayo yalikuwepo kama sehemu ya kutekeleza demokrasia ya kila mwanachama.

Alisema kuwa makundi hayo yatakapomalizika ndipo mafanikio na maendeleo ya pamoja yatatimia na hilo ndiyo jambo ambao Wana-Simba wanatakiwa kulitekeleza kwa pamoja ili kufikia malengo waliyojiwekea.

"Nina kazi kubwa mbele yenu, naamini sitowaangusha, nitafanya kazi kwa umakini mkubwa ili kufikia malengo tuliyojiwekea, nawashukuru wote walioniunga mkono na hata wale ambao hawakunipigia kura kwa sababu kila mmoja ametumia haki yake ya kidemokrasia, nawapongeza pia wagombea wengine walioshinda na wale waliokosa kura zao hazikupotea ila ni maamuzi ya wanachama yanatakiwa kuheshimiwa," alisema Aveva.

Aliongeza kuwa uchaguzi umemalizika na kinachotakiwa kufuata ni wanachama kujipanga kwa ajili ya kuimarisha umoja na utulivu ili mpira uchezwe ndani ya timu yao

AHADI ALIZOTOA
Wakati aliposimama kuomba kura kwenye ukumbi huo wa uchaguzi, Aveva, alisema kuwa mara atakapofanikiwa kuingia madarakani atahakikisha anaongeza idadi ya wanachama wa klabu hiyo kutoka 7,000 na kufikia 50,000.

Aveva alisema kuwa anaamini kwa kuongeza wanachama, klabu yao itaweza kupata rasilimali watu na kujiweka katika nafasi nzuri ya kujiongezea mapato na kuwataka wanachama wawe wanalipa ada zao kila mwaka na si kusubiri wakati wa uchaguzi.

Alisema anauzoefu ndani ya Simba na akiwa mwenyekiti wa kamati mbalimbali alizoziongoza aliipatia klabu mafanikio hivyo watarajie mazuri zaidi baada ya yeye kupata ridhaa ya wanachama ya kuwa rais mpya na wa kwanza wa Wekundu wa Msimbazi.

WENGINE WALIOSHINDA
Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo saa 9:58 usiku wa kuamkia leo Jumatatu, Mjumbe wa Kamati ya Uchaguzi na aliyesimamia zoezi hilo, Amin Bakhresa, alisema kuwa mshindi wa nafasi ya Makamu wa Rais ni Geofrey Nyange 'Kaburu' ndiye aliibuka kidedea kwa kupata kura 1,046 na kuwashinda Jamhuri Kihwelu 'Julio' (412), Swedy Mkwabi (373) na Bundala Kabula aliyeambulia kura 25.

Bakhersa pia aliwatangaza wagombea watano waliochaguliwa kuunda Kamati ya Utendaji kuwa ni pamoja na zilichukuliwa na Iddi Kajuna aliyepata kura 893, Said Tully (788), Collins Frisch (758), Ally Suru ( 627) na kwa upande wa mwanamke aliyeibuka kinara ni Jasmine Badour.

Mjumbe huyo wa kwanza mwanamke kuingia katika uongozi alipata kura 933 na kuwagalagaza wapinzani wake Asha Muhaji aliyepata kura 623 na Amina Poyo (330).

Saturday, June 28, 2014

MAHAKAMA KUU YATUPILIA MBALI OMBI LA KUZUIA UCHAGUZI MKUU SIMBA, UNAFANYIKA KESHO

KLABU ya Simba itafanya uchaguzi wake mkuu kesho baada ya Mahakama Kuu kutupilia mbali maombi ya wanachama watatu wa klabu hiyo kutaka uchaguzi huo usimamishwe.

Wanachama hao wa Simba, Josephat Waryoba, Saidi Ally Monero na Hassan Hassan kwa niaba ya wenzao 60, waliwasilisha maombi hayo Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, wakiomba amri ya zuio la muda la uchaguzi huo.

Walikuwa wakiiomba mahakama hiyo iwape kibali cha kufungua kesi ya uwakilishi na pia itoe amri ya zuio la uchaguzi huo.

Hata hivyo, Mahakama Kuu katika uamuzi wake uliotolewa jana na Jaji Agustine Mwarija baada ya kusikiliza hoja za pande zote, yaani watoa maombi na wajibu maombi, ilikubaliana kufungua kesi ya uwakilishi, lakini ikatupilia mbali maombi ya zuio la uchaguzi.

Jaji Mwarija alifikia uamuzi wa kutupilia mbali maombi ya wanachama hao baada ya kubaini kuwa yamewasilishwa mahakamani isivyo sahihi kisheria, kutokana na kutokuwepo kesi ya msingi mahakamani.

Alisema kwa mujibu wa kanuni ya 1 (8) ya mahakama hiyo ya uendeshaji wa mashauri ya jinai, kesi inayowahusisha watu wengi wenye masilahi yanayofanana, inaweza kufunguliwa na mmoja wao au baadhi yao kwa niaba ya wengine baada ya kupata kibaku cha mahakama.

Kuhusu maombi ya zuio la muda, Jaji Mwarija alisiea mahakama inaweza kutoa zuio pale tu panapokuwepo na kesi ya msingi iliyofunguliwa mahakamani, lakini kesi hiyo haipo.

SMALL BOYS, MSHIKAMANO, PACHOTO ZAPIGWA FAINI





Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) zimezipiga faini ya kati ya sh. 300,000 na sh. 500,000 klabu za Mshikamano FC, Pachoto Shooting Stars, Town Small Boys na Kiluvya United kutokana na makosa mbalimbali ikiwemo viongozi, wachezaji na washabiki kufanya vurugu kwenye mechi za Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) iliyomalizika hivi karibuni.

Uamuzi huo umefanywa na Kamati ya Mashindano ya TFF iliyokutana juzi (Juni 23 mwaka huu) jijini Dar es Salaam kupitia masuala mbalimbali ikiwemo taarifa za mechi, na malalamiko kutoka kwa baadhi ya timu zilizoshiriki RCL iliyochezwa katika vituo vya Mbeya, Morogoro na Shinyanga.

Town Small Boys ya Ruvuma imepigwa faini ya sh. 500,000 kwa mujibu wa kanuni ya 37(13) ya Kanuni ya RCL kutokana na udanganyifu kwa kumtumia mchezaji Agaton Mapunda ambaye hakustahili ingawa usajili wake ulithibitishwa na TFF, kwa kutokuwepo pingamizi kutoka klabu yoyote katika kipindi cha pingamizi.

Licha ya usajili wake kuthibitishwa na TFF, Kamati ilibaini mchezaji huyo hakutoka ndani ya Mkoa wa Ruvuma kama kanuni za RCL zinavyoelekeza. Hata hivyo, matokeo ya mechi hiyo dhidi ya Njombe Mji iliyomalizika kwa bao 1-1 yanabaki kama yalivyo kwa mujibu wa kanuni ya Kanuni ya 52 (3 na 4) na 31(11) ya RCL kwa kuwa mchezaji Mapunda alithibitishwa na TFF (qualified player).

Vilevile mchezaji huyo amepigwa faini ya sh. 200,000 kwa mujibu wa kanuni za 48(4) na 31(11) za RCL. Nayo malalamiko ya Njombe Mji dhidi ya mchezaji David Noel Makakala kuwa ndiye aliyecheza mechi hiyo badala ya Carlos Mapunda yametupwa kwa kukosa vielelezo na ushahidi wa kuthibitisha hilo.

Kiluvya United FC ya Pwani imepigwa faini ya sh. 300,000 kwa mujibu wa kanuni ya 37(1) kutokana na vurugu za washabiki wake kwenye mechi namba 46 dhidi ya Abajalo iliyochezwa mjini Morogoro.

Pachoto Shooting Stars ya Mtwara na Mshikamano FC ya Dar es Salaam zimepigwa faini ya sh. 500,000 kila moja kwa kufanya vurugu kubwa kwenye mechi yao namba 100 iliyovunjika mjini Morogoro. Pia Mshikamano FC wamepewa pointi tatu na mabao matatu kwa mujibu wa kanuni ya 23(1na5) na 22(d).

Wachezaji na viongozi wa Pachoto Shooting na wachezaji wa Mshikamano FC waliofanya vurugu na kupigana, suala lao linapelekwa kwenye Kamati ya Nidhamu ya TFF kwa uamuzi na hatua za kinidhamu.

Nayo Tanzanite ya Manyara imefungiwa kucheza mashindano yote rasmi kwa msimu mmoja, na kuteremishwa daraja hadi ligi ya wilaya mara itakapomaliza kifungo chake kwa mujibu wa kanuni ya 21(3)(a), 37(14) na 22(a). Tanzanite iliadhibiwa kwa mujibu wa kanuni ya 23(1,5 na 6) baada ya kumpiga mwamuzi kwenye mechi dhidi ya AFC na baadaye kugomea mchezo. Ilishindwa kulipa faini na kujitoa mashindanoni kwa kuondoka kituoni.

Wachezaji wanaotuhumiwa kumpiga mwamuzi mpaka kumjeruhi suala lao litapelekwa kwenye Kamati ya Nidhamu ya TFF.

Kamati imetupa malalamiko ya African Sports ya Tanga dhidi ya Abajalo ya Dar es Salaam, Ujenzi FC ya Rukwa dhidi ya AFC, Panone FC ya Kilimanjaro dhidi ya Volcano FC ya Morogoro, na Mvuvumwa FC ya Kigoma dhidi ya Mbao FC ya Mwanza kwa kukosa vielelezo na ushahidi.

Pia malalamiko ya Mvuvumwa FC dhidi ya Geita Veterans ya Geita juu ya kuwachezesha Ibrahim Alphonce, Zamoyoni Magoma na John Mtobesya kwa kuwa hawakusajiliwa yametupwa kwa vile wachezaji hao ni halali, isipokuwa orodha ya wachezaji wa Geita Veterans FC iliyotolewa kwa ajili ya pingamizi ilikuwa na upungufu kiuchapaji ambapo wachezaji sita hawakuorodheshwa.

Nao makamishna Edward Hiza na Jimmy Lengwe waliokuwa kituo cha Morogoro wamepewa onyo kutokana na ripoti zao kuwa na upungufu.

Vilevile Kamati ya Mashindano imezitangaza rasmi timu za African Sports, Geita Veterans na Panone FC kupanda kucheza Ligi Daraja la Kwanza (FDL) msimu wa 2014/2015.

RAY C ASIMULIA KILICHOMSIBU, AWATOA CHOZI WANANCHI




NA SOLOMON MWANSELE.

REHEMA Chalamila maarufu zaidi kama Ray C, siyo jina geni kwa wapenzi wa muziki wa Kizazi kipya nchini, maarufu zaidi Bongo fleva.Ni mmoja wa wasanii walioufikisha muziki huu hapa ulipo leo.

Ray C ni alianza kupata umaarufu, na mafanikio lukuki akiwa na umri mdogo wa miaka 17, na kuweza kutingisha vilivyo, akianzia kazi ya utangazaji katika kituo cha radio ya East Afrika, mnamo mwaka 1999, na mwaka mmoja baadaye alijiunga na radio Clouds.

Mwaka huo huo wa 2000, alianza kujihusisha na muziki wa kizazi kipya na kuweza kuliteka vilivyo soko huku mashabiki wake wakimuongezea jina lingine la kwa kuanza kumuita ‘Kiuno bila mfupa’ kutokana na unenguaji wake mahiri jukwaani.

Ray C aliweza kuutangaza vyema muziki wa Bongo Fleva, katika nchi za Marekani, Dubai ,Sweden, China, Uganda, Kenya, Afrika ya Kusini, Uingereza, Oman, Australia, Norway, Msumbiji, India na Nigeria.

Kutokana na mafanikio yake hayo katika fani hizo, za utangazaji na muziki wa Bongo Fleva, Ray C aliweza aliweza kujenga nyumba nzuri na kubwa, akiwa na umri huo mdogo na baadaye kununua magari, na vile vile kufanikiwa kufungua maduka makubwa jijini Dar es Salaam.

Lakini ghafla ujana uliompaisha na kumpeleka juu, ukamgeuza kichwa chini miguu juu, hali iliyopelekea nuru na nyota yake iliyokuwa inawaka kufifia, ambapo Ray C akawa haonekani tena, kiasi cha kufikia hatua baadhi ya watu kumzushia kuwa amefariki dunia.

Hivi karibuni Ray C alitoa ushuhuda mzito, na uliovuta hisia za mamia ya watu waliohudhuria maadhimisho ya Siku ya Kupiga vita matumizi ya dawa za kulevya Duniani, ambayo kitaifa yalifanyika katika viwanja vya Ruanda Nzovwe jijini Mbeya.

Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo alikuwa ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Mohammed Gharib Bilal.Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uratibu, Sera na Bunge), William Lukuvi, pia alihudhuria.

Ray C anasema mara baada ya kujiingiza, katika matumizi ya dawa za kulevya uwezo wake wa kufanya muziki ulitoweka, na akajikuta anaanza taratibu katabia ka kuuza vitu vyake kimoja baada ya kingine.

“Nilianza kwa kuuza vitu vidogo vidogo, baadaye nikauza gari zangu, nyumba na maduka yote nikayafilisi.Nikaanza kuwa mtu wa kujificha, huku nikiendelea kudhoofika, ilifika wakati nililazimika kutembea nikiwa nimevaa ‘kininja’.

Mungu wangu!Nilikuwa nimenasa kwenye mdomo wa Mamba, dawa za kulevya zilikuwa zinanimaliza, na nilipokuja kushtuka nilikuwa nimenasa.Maisha yangu yakawa si starehe tena bali ni mateso na aibu” anasema Ray C.

Anaongeza, alipokuwa katika uteja alikwenda mbali zaidi ya kuuza vitu vyake vya thamani, na roho inamuuma sana anapokumbuka siku, alipomshikia kisu mama yake mzazi ili kumlazimisha ampe fedha ili akanunue dawa za kulevya.

Akiongea huku akishikwa na uchungu mkubwa, na machozi kumtoka akiwa jukwaani akionekana kujutia matendo yake, Ray C anasema roho inamuuma sana anapokumbuka siku alimnyonga mkono mama yake na kumpokonya simu.

“Ninapokumbuka haya roho huwa inaniuma, kuliko hata kupoteza vitu vyangu vya thamani.Namshukuru mama alitambua kuwa sikuwa mimi, hivyo hakunikatia tamaa aliendelea kunihangaikia na kufanya maombi sana” anasema Ray C huku akijifuta machozi.

Anaongeza kwa kumuomba msamaha mama yake mzazi, kwa mateso aliyompa na kumshukuru mama yake huku akimuombea kwa Mungu, azidi kumbariki na kuwaomba wazazi wote nchini kuiga mfano huo kwa kuwasaidia vijana wao.

Ray C anasema anakumbuka alivyofukuzwa kama mbwa, kwa muuza dawa za kulevya kwa sababu alikuwa hana fedha, na anaumia sana anapokumbuka siku alizokuwa analala kwenye boksi, kwani hakuweza kurudi nyumbani akiwa ana ‘arosto’, yaani bila kuvuta unga.

Anasema kwa sababu ya kukosa dawa za kulevya, kutokana na kutokuwa na fedha alilazimika kulala kwenye boksi, akisubiria labda itatokea ‘kampani’yaani rafiki, ili imnunulie dawa apone anasema yalikuwa ni mateso ya ajabu, ambayo hayana mfano.

Msanii huyu wa muziki wa Bongo Fleva, anaongeza kuwa mateso na dharau alizozipata hazikuwa za peke yake, kwani familia yake pia ilikuwa katika dimbwi la mateso, familia yote iliumwa ambapo mama yake alilia sana na kuhangaika.

Anamnukuu mama yake mzazi:”Mwanangu nini hiki…umerogwa na nani mwanangu?Eeeh Mungu nisaidie”.Kilikuwa ndio kilio cha mama kila wakati.

Anaongeza mtu aliyekuwa anategemewa na familia, alikuwa anatoweka taratibu na sasa akawa mzigo mkubwa kwa familia.Alikuwa anaumia sana na kutaka kuacha matumizi ya dawa za kulevya, lakini alikuwa amenasa kwenye meno makali ya Mamba, na hakuwa na ujanja.

“Mama alihangaika sana na ndugu zangu pia walikosa raha.Mama alikuwa ni mtu wa kwenda kwenye maombi kila wakati.Alikuwa na fedha lakini naye uchumi wake uliporomoka, na kutoweka kwa sababu yangu” anasema Ray C huku akijifuta machozi.

Anasema hatimaye Mungu, alimuinua Rais Jakaya Kikwete, ambaye alijitolea kumsaidia kwa kumpa matibabu, na kwa sababu hata yeye mwenyewe, alikuwa na dhamira ya dhati ya kuacha dawa za kulevya, kwake ilikuwa ni jambo rahisi kuachana na dawa hizo.

Anaongeza kuwa anatumia fursa hiyo, kwa mara nyingine kumshukuru mwenyezi Mungu kwa kumpa fursa nyingine ya kuwa Ray C, lakini siyo yule wa zamani bali kuwa mwenye akili na mitazamo mipya kabisa ya maisha, na ambaye watanzania na Taifa litanufaika naye.

Anasema kwa namna ya kipekee, na kwa mara nyingine anamshukuru Rais Kikwete, kwa kumsaidia na kumuomba Mungu azidi kumbariki.Anamuahidi kwa kumsaidia yeye wengi watapona, na anajua hiyo ndio ilikuwa dhamira yake (Rais Kikwete), ili awe mfano ili wengi waokoke na janga hilo la matumizi ya dawa za kulevya.
“Naamini Mungu alikuwa na mpango na mimi, hivyo ni lazima nimtumikie kwa njia hii” anasema Ray C.

Anabainisha kilichomuingiza kwenye matumizi ya dawa za kulevya, ilikuwa ni marafiki wabaya na mahusiano mabaya ya kimapenzi, ambapo kupitia mtu aliyempenda na kumuamini sana, katika mazingira ambayo hayakuwa wazi, alijikuta amenasa kwenye matumizi ya dawa hizo.

Anaongeza, alipokuwa katika tatizo hilo alijifunza mambo matatu, ambayo anayataja kuwa ni sio watu wote wanaotumia dawa za kulevya, wameingia huko wakijielewa.

Pili, kuna unyanyapaa mkubwa wanaofanyiwa waathirika wa dawa za kulevya, kutoka kwa jamii na vyombo vya dola, na kwa asilimia kubwa unyanyapaa huo unatokana na uelewa mdogo, juu ya hali halisi ya tatizo.

Tatu, alijifunza kuwa watu kuendelea kutumia dawa hizo, na nyingi hatarishi wanazokuwa nazo hakutokani na wao kupenda, bali mateso makali ambayo mtu anayapata anapokosa dawa hizo, na kuwa anayajua mateso mazito waliyonayo, tofauti na jamii inavyofikiri.

Ray C anasema kutokana na Mungu kumsaidia, kwa kumtumia Rais Kikwete, na jinsi yeye mwenyewe anavyoguswa na tatizo hilo, shukrani yake ni kwa Rais kufanya juhudi za kuielimisha jamii juu ya athari za dawa za kulevya, na pia kuwasaidia waliokwisha kuingia watoke huko na ambao hawajaingia wasithubutu.

“Kwa kufanikisha hilo, nimeamua kuanzisha asasi inayoitwa Ray C Foundation, asasi hii ina lengo la kufanya uelimishaji mkubwa kwa jamii, kupitia makundi yake mbalimbali pamoja na kusaidia walioathirika, warudi kuwa watu wa kawaida” anasema Ray C.

Kupitia asasi yake hiyo, tayari wameanza kampeni ya shule kwa shule wakitembelea baadhi ya shule za sekondari jijini Dar es Salaam, ambapo wana lengo la kuzitembelea shule zote za sekondari katika mikoa yote ya Tanzania, hasa ile iliyoathirika zaidi na dawa za kulevya.

Anasema, vile vile wameanza kutembelea vijana watumiaji wa dawa za kulevya kwenye maskini zao, na kuwaelimisha waache na katika kipindi cha miezi miwili tu ya kampeni hiyo, vijana 25 wameamua kuacha na wanapata matibabu ya Methadone.

Ray C anaongeza kwa miezi kumi sasa, amekuwa akizungumza kupitia vyombo mbalimbali vya habari, juu ya uwezekano wa kuacha dawa za kulevya kwa watumiaji, na wasio watumiaji kujiweka mbali na dawa hizo.

Anabainisha hilo limechangia ongezeko la watu, wanaotaka kuacha na kupata matibabu na kuwa utekelezaji wa malengo hayo kupitia Ray C Foundation, umepokelewa kwa shauku kubwa na watanzania, lakini anakumbana na changamoto ya uwezeshaji.

Anamuomba Makamu wa Rais Dk.Bilal, serikali, watu binafsi, na taasisi mbalimbali kuiunga mkono Ray C Foundation, ili iweze kutekeleza mikakati na malengo iliyonayo, kwani Taifa linaangamia na hali ni mbaya sana.

“Kwa namna ya pekee, pia natumia nafasi hii kuiomba serikali, kufanya uwekezaji mkubwa katika huduma ya matibabu kwa waathirika wa dawa za kulevya, kwa kufungua huduma hiyo katika hospitali za wilaya na za Rufani nchini” anasema Ray C.

Anaongeza hilo ni kutokana na idadi kubwa ya watu wanaopata ufahamu, na kuamua kuacha matumizi ya dawa za kulevya, inakuwa kwa kasi kubwa kutokana na kampeni wanazoendelea kuzifanya

Sunday, June 22, 2014

UCHAGUZI MKUU SIMBA RUKSA, TFF YAKUTANA NA KAMATI YA BUNGE




Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) baada ya kupokea na kuzingatia maombi ya Simba (barua imeambatanishwa), na kwa kuzingatia Ibara ya 26 ya Kanuni za Uchaguzi za TFF toleo la 2013 limeiruhusu klabu hiyo kuendelea na mchakato wa uchaguzi wao uliopangwa kufanyika Juni 29 mwaka huu.

TFF inawahimiza wanachama wa klabu ya Simba kuwa watulivu na wafanye uchaguzi wao kwa amani.

TFF YAELEZEA MIKAKATI YAKE BUNGENI
Uongozi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ukiongozwa na Jamal Malinzi jana (Juni 21 mwaka huu) mjini Dodoma umekutana na Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Maendeleo ya Jamii chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Said Mtanda (Mbunge wa Mchunga).

Katika kikao hicho TFF ilielezea mikakati yake ya maendeleo ya mpira wa miguu pamoja na maandalizi ya timu ya Taifa kwa ajili ya mchezo wake dhidi ya Msumbiji.

TFF iliiahidi Kamati ya Bunge kuwa itaendelea kuwa inafanya shughuli zake kwa karibu na Serikali na kamati hiyo ya Bunge.

Katika kikao hicho, ujumbe wa benki ya CRDB ukiongozwa na Meneja wa Electronic Banking, Bw. Mangire Kibanda ulihudhuria ili kutoa ufafanuzi juu ya mradi wa kuuza tiketi za elektroniki, mradi ambao maandalizi yanaendelea vizuri.

Friday, June 20, 2014

TFF, PLAN INTERNATIONAL KUHAMASISHA HAKI ZA WATOTO



Wakati mamilioni ya Watanzania wakifuatilia Fainali za Kombe la Dunia nchini Brazil, Shirika la kutetea haki za watoto la Plan International limeingia ubia na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kwa ajili ya kutetea na kuhamasisha juu ya ulinzi wa haki za mtoto hapa nchini.

Kwa lengo hilo, mkataba wa ushirikiano umesainiwa leo katika ofisi za makao makuu ya TFF jijini Dar es Salaam baina ya Mkurugenzi wa Plan International Tanzania, Jorgen Haldorsen na Rais wa TFF, Jamal Malinzi. Ushirikiano huo unalenga kufanya kazi pamoja katika kushughulikia masuala ya ukatili wa kijinsia, ndoa na mimba za utotoni.

Kwa mujibu wa Haldorsen, mchezo wa mpira ndio unaoongoza nchini na kote duniani kwa kuwa na ushabiki mkubwa na kwamba joto kali juu ya Fainali za Kombe la Dunia linaloendelea Brazil ni ushahidi tosha.

“Tunatambua uwezo wa mchezo huu wa kuwajumuisha watu. Sasa tunataka tuwajumuishe watu sio tu kwa ajili ya furaha lakini pia kama njia ya kuleta mabadiliko juu ya usawa wa kijinsia kwa kutetea na kuhamasisha juu ya haki za mtoto wa kike,” aliongeza.

Mkurugenzi huyo alidokeza kuwa ushirikiano na TFF ni sehemu ya kampeni ya kimataifa inayoendeshwa na shirika hilo kote ulimwenguni inayoitwa ‘Because I Am A Girl’-BIAAG au kwa Kiswahili- KWA SABABU MIMI NI MSICHANA ambayo inalenga kuwatoa mamilioni ya wasichana kutoka katika umaskini kupitia uhamasishaji juu ya haki zao, elimu na stadi za maisha.

“Kwa kupitia ubia huu tutakuwa na uwezo wa kuwafikia mamilioni ya Watanzania na tutawapa wasichana ujumbe kuwa KWA SABABU MIMI NI MSICHANA, lazima nipate fursa sawa na wavulana. KWA SABABU MIMI NI MSICHANA, lazima niwe na uwezo wa kufunga magoli ya kufikia ndoto zangu katika maisha,” Haldorsen alieleza.

Kwa upande wake, Rais wa TFF, ambaye ni mjumbe katika Kamati ya Huduma kwa Jamii ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Ulimwenguni- FIFA, alisema kuwa ubia huo ni sehemu ya utekelezaji wa sera za huduma kwa jamii ya TFF na kwamba wana furaha kushirikiana na Plan International kwa lengo hili muhimu.

“Ushirikiano huu ni muhimu sana kwetu kwani unakileta chombo kikubwa kabisa cha michezo hapa nchini pamoja na shirika la Plan International hususan kwa ajili ya haki za mtoto wa kike. Tunategemea kutumia mtandao wetu nchi nzima kuelimisha juu ya usawa wa kijinsia na uhamasishaji wa haki za mtoto wa kike,” alisema Rais Malinzi.

Kwa pamoja tutashughulikia masuala ya usawa wa kijinsia, hususan kupambana na ndoa za utotoni ambazo zinawazuia mamilioni ya watoto wa kike nchini wasiweze kumaliza shule, kufikia ndoto zao katika maisha, na vile vile kuwaacha waendelee kuteseka katika umaskini,” Rais Malinzi aliongeza.

KUHUSU PLAN INTERNATIONAL: Plan International ni shirika la kimaendeleo la misaada ya kibinadamu, linalomlenga mtoto lisilofungamana na mrengo wowote wa kidini, kisiasa au kiserikali.

Plan International ilianzishwa zaidi ya miaka 70 iliyopita na inaendesha shughuli zake katika nchi 70 duniani. Plan International imekuwa inafanyakazi hapa Tanzania tangu mwaka 1991 ikiwasaidia watoto na jamii kupata huduma za afya, elimu, maji, usafi na mazingira, kujikimu na ulinzi. Inaendesha miradi Dar es Salaam, Morogoro, Dodoma, Geita, Pwani, Mwanza na Rukwa.

KAMPENI YA KWA SABABU MIMI NI MSICHANA –BIAAG: Kampeni ya Kwa Sababu Mimi ni Msichana-BIAAG (2012-2016) ni kampeni ya Plan ulimwenguni kote inayolenga kuelimisha na kutetea haki za mtoto wa kike na kuwatoa mamilioni ya wasichana kutoka kwenye lindi la umaskini kupitia elimu na utoaji wa stadi za maisha na kazi.

Kampeni hii inalenga kupambana na ubaguzi wa kijinsia na kuboresha maisha ya wasichana milioni 4 duniani na zaidi ya laki 3 hapa Tanzania kwa kuwawezesha kujiunga shuleni, kupata stadi za kiufundi na maisha, kujikimu, na kushiriki katika shughuli mbalimbali katika jamii na kulindwa, kwa kukabiliana na vikwazo dhidi ya maendeleo ya mtoto wa kike.

26 WAITWA STARS SAFARI YA GABORONE





Wachezaji 26 wa Taifa Stars wanaingia kambini Jumatatu (Juni 23 mwaka huu) kwa ajili ya safari ya Gaborone, Botswana.

Kwa mujibu wa Kocha Msaidizi wa timu hiyo Salum Mayanga, wachezaji hao wanatakiwa kuripoti katika hoteli ya Accomondia jijini Dar es Salaam kujiandaa kwa safari hiyo inayotarajiwa kuwa Juni 24 mwaka huu.

Wachezaji hao ni wanaotakiwa kuripoti kambini ni Deogratias Munishi, Aishi Manula, Benedictor Tinoko, Kelvin Yondani, Said Moradi, Nadir Haroub, Joram Nason, Shomari Kapombe, Oscar Joshua, Edward Charles, Aggrey Morris na Pato Ngonyani.

Wengine ni Frank Domayo, Amri Kiemba, Erasto Nyoni, Jonas Mkude, Said Juma, Haruna Chanongo, Himid Mao, John Bocco, Simon Msuva, Kelvin Friday, Ramadhan Singano, Khamis Mcha, Mrisho Ngasa na Mwegane Yeya.

KOZI YA UKOCHA LESENI B YAFIKIA TAMATI


Kozi ya makocha wa mpira wa miguu ya Leseni B inayotambuliwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) iliyodumu kwa wiki mbili inafungwa kesho (Juni 20 mwaka huu) jijini Dar es Salaam.

Makocha 26 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar wameshiriki katika kozi hiyo chini ya wakufunzi wa CAF, Sunday Kayuni, Salum Madadi wa Tanzania na Honory Janza kutoka Zambia. Ufungaji wa kozi hiyo unatarajiwa kufanywa saa 5 asubuhi kwenye hosteli za TFF zilizopo Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume.

Walioshiriki kozi hiyo ni Abdalla Mohammed Juma (Zanzibar), Abdul Banyai (Temeke), Abdul Nyumba (Temeke), Abdulmutik Haji (Zanzibar), Aley Mohammed (Zanzibar), Ali Vuai Shein (Zanzibar), Dennis Kitambi (Morogoro), Dismas Haonga (Ilala), Emmanuel Massawe (Shinyanga), Fikiri Elias (Arusha), Fulgence Novatus (Mwanza), Hababuu Ali Omar (Zanzibar), Juma Mgunda (Tanga) na Kidao Wilfred (Ilala).

Wengine ni Maka Mwalwisi (Mbeya), Malale Hamsini Keya (Zanzibar), Mecky Maxime (Morogoro), Mohammed Tajdin (Temeke), Mussa Furutuni (Dodoma), Nassor Salum Mohamed (Zanzibar), Peter Mhina (Ruvuma), Said Mohamed Abdulla (Zanzibar), Salim Makame (Zanzibar), Salum Ali Haji (Zanzibar), Sebastian Nkoma (Ilala), Wane Mkisi (Dar es Salaam).

WAMBURA APIGWA CHINI SIMBA, UCHAGUZI UPO PALEPALE



Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imeikataa rufani ya Michael Wambura kupinga kuenguliwa kugombea urais katika uchaguzi wa klabu ya Simba unaotarajiwa kufanyika baadaye mwezi huu.

Wambura aliwasilisha rufani yake mbele ya Kamati hiyo iliyokutana leo (Juni 19 mwaka huu) jijini Dar es Salaam chini ya Kaimu Mwenyekiti Wakili Mwita Waissaka kupinga uamuzi wa kumwengua katika kinyang’anyiro hicho uliofanywa na Kamati ya Uchaguzi ya Simba kwa kufanya kampeni kabla ya muda uliopangwa.

Baada ya kupitia vielelezo, kanuni na sheria, Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF imeridhika kuwa mrufani (Michael Wambura) alifanya kampeni kabla ya muda kinyume na Ibara ya 6(1)(a) na (g), Ibara ya 6(1)(l) pamoja na Ibara ya 14(3) ya Kanuni za Uchaguzi za TFF toleo la 2013.

Kwa mujibu wa ibara hizo, Kamati ya Uchaguzi ya Simba inayo mamlaka ya kumwengua (disqualify) mgombea anayefanya kampeni ama kukiuka maagizo halali ya Kamati ya Uchaguzi.

Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF imeziagiza kamati zote za uchaguzi za wanachama wa TFF kufuata kanuni za uchaguzi kama zilivyoainishwa katika Katiba zao ili kuepusha rufani za mara kwa mara.

Uamuzi wa Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF umezingatia Katiba ya TFF pamoja na kanuni zake, na pia Katiba ya Simba.

Thursday, June 12, 2014

WAMBURA KIDUME, AIBWAGA KAMATI YA UCHAGUZI SIMBA


MGOMBEA wa nafasi ya rais katika uchaguzi mkuu wa klabu ya Simba, Michael Wambura amepitishwa kuwania nafasi hiyo katika uchaguzi mkuu ujao.

Wambura aliondolewa katika mbio hizo na Kamati ya Uchaguzi ya Simba chini ya Mwenyekiti, Damas Ndumbaro kwa madai ya kukosa sifa.

Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), jana ilimtangaza Wambura kuwa mgombea halali wa nafasi hiyo katika uchaguzi mkuu wa Simba, uliopangwa kufanyika Juni 29 mwaka huu.

Kufuatia kupitishwa kuwania nafasi hiyo, Wambura sasa atachuana vikali na mpinzani wake wa karibu, Evans Aveva.

Wambura alifutiwa uanachama wa Simba katika kikao cha Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo, kilichofanyika Mei 5, 2010 kwa madai ya kuipeleka klabu hiyo mahakamani katika kesi namba 100/2010.

Inadaiwa Wambura alikiuka katiba ya Simba Ibara za 11 (1), (e), (2) 12 (3) na 55 kwa kosa la kupeleka masuala ya michezo mahakamani.

Mwenyekiti wa Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF, Julius Lugaziya, alisema Wambura amerejeshwa kwa kuwa Kamati ya Utendaji ya Simba ilishindwa kulinda katiba ya klabu hiyo.

Alisema tangu asimamishwe, amekuwa akifanya shughuli za Simba bila kuzuiwa na kulipa ada ya uanachama, kushiriki mikutano ya wanachama na ya dharula kwa kipindi chote.

"Sharti la msingi la katiba kuwa ni mwanachama halali tu ndiye anaruhusiwa kushiriki kwenye mikutano,"alisema.

"Uongozi au mwanachama wa Simba kwa mujibu wa katiba ana uwezo wa kuhoji mahudhurio ya mwanachama asiye na haki ya kushiriki, lakini kwa Wambura haikuwa hivyo,"alisema.

Alisema endapo chombo au kikao chochote kinafanya uamuzi na baadhi ya wajumbe wasiopaswa kushiriki na kutoa uamuzi, uamuzi uliopitishwa unakosa nguvu za kisheria.

"Kama hivyo ndivyo, je vikao vilivyoandaa katiba ya Simba na kuipitisha, ambavyo Wambura alishiriki, vina athari gani kuhusu uhalali wa katiba ya Simba?" Alihoji

Alisema hata vikao vilivyoteua kamati ya uchaguzi, ambavyo Wambura alishiriki, nayo itakuwa batili.

WABRAZIL KUTUMIA KAA KUTABIRI MATOKEO


Salvador, Brazili

KAMA ilivyokuwa katika fainali za Kombe la Dunia mwaka 2010 zilizofanyika Afrika Kusini, utabiri wa kutumia wanyama katika kinyang’anyiro kinachoanza leo Brazili umeibuka tena, huku mwenyeji Brazil akiwa na matumaini na mtabiri wake-kaa.

Akitumia kubashiei kwa kuchagua chakula, kaa huyo aliyepachikwa jina la Kichwa Kikubwa, juzi alitabiri kwamba mwenyeji huyo ataibuka na ushindi dhidi ya Croatia katika mechi ya ufunguzi.

Kichwa Kikubwa ndilo jibu kwa Pweza Paulo wa Ujerumani, ambaye alianza kutumika katika michuano ya mwaka 2010 na kusababisha msisimko mkubwa duniani.

Katika zizi la kaa lililoko Praia do Forte Kaskazini mwaka Salvador, kaa huyo wa kiume mwenye umri wa miaka 25 juzi alipewa kuchagua kati ya kula samaki aliyening’inizwa kwenye bendera ya Brazil na mwingine kwenye bendera ya Croatia.

Baada ya kujaribu kula samaki aliyekuwa amening’inizwa kwenye mpira ikimaanisha matokeo ya sare, Kichwa Kikubwa aliamua kuchagua anayewakilisha Brazili.

Kundi dogo la watu waliokuwa wakishuhudia hali hiyo lilishangilia kutokana na uchaguzi huo wa Kichwa Kikubwa.

Wachina wameamua kumtumia kundi la ndama wa dubu aina ya panda kutabiria timu yao katika michuano hiyo.

Hata hivyo mwaka 2010 utabiri wa Paul ulikwama baada ya Ujerumani kupoteza mechi kwa Hispania katika nusu fainali ya mashindano hayo.

Wednesday, June 11, 2014

NYOTA WA ZAMANI KMKM, TAIFA STARS, ALI ISSA KEPTENI AFARIKI DUNIA


Na Salum Vuai, Zanzibar


MCHEZAJI mstaafu wa timu ya soka ya KMKM Ali Issa Simai, amefariki dunia jana wakati wa magharibi baada ya kuugua kwa muda mfupi, na kuzikwa leo huko Chukwani Wilaya ya Magharibi Unguja.

Marehemu, ambaye alijulikana zaidi kwa jina la ‘Kepteni’ kutokana na kuwa nahodha wa KMKM kwa muda mrefu, alikutwa na mauti nyumbani kwake Fuoni baada ya kurudi kutoka katika shughuli zake za kawaida.

Mwaka 1974, kiungo huyo mshambuliaji alijiunga na timu ya kikosi cha wanamaji wakati huo ikiitwa Navy na kudumu nayo hata ilipobadilishwa jina na kuitwa KMKM (Kikosi Maalumu cha Kuzuia Magendo), akitokea klabu ya Ujamaa yenye maskani yake mtaa wa Rahaleo.

Mmoja wa wanasoka waliocheza pamoja naye Abdalla Maulid, ameliambia gazeti hili kuwa, marehemu alikuwemo kwenye kikosi cha washika magendo hao kilichoshiriki michuano ya klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati mwaka 1974 yaliyofanyika mjini Dar es Salaam, yakiwa katika mwaka wake wa kwanza.

Maulid alifahamisha kuwa, mwaka 1975, kepteni huyo aliitwa katika timu ya taifa ya Zanzibar iliyoshiriki mashindano ya Chalenji kwa vijana, yaliyofanyika uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam, na ubingwa kuchukuliwa na Kenya.

Aidha mwaka huo wa 1975, marehemu aliyesifika kwa umahiri wake wa kumiliki mpira na mbinu za kufumania nyavu, aliteuliwa katika timu kubwa ya taifa iliyokuwa chini ya kocha Muingereza George Dunga.

Pamoja na kuibeba vyema klabu yake katika ligi kuu ya muungano kuanzia mwaka 1976 na kufanikiwa kutwaa ubingwa mwaka 1984, marehemu Ali Issa pia aliisaidia Navy (sasa KMKM) kucheza klabu bingwa Afrika mwaka 1978, ambapo walifika hatua ya nne bora.

Nahodha huyo alidumu na KMKM hadi mwaka 1990 alipoamua kutundika madaluga, na kuendelea kuchezea timu ya maveterani, Wazee Sports.

Mazishi ya marehemu huyo aliyeacha watoto kumi, yalihudhuriwa na mamia ya wananchi na wanamichezo mbalimbali, ambapo mwili wake ulisaliwa katika msikiti uliopo karibu na uwanja wa Amani, na baadae kupelekwa malazoni Chukwani.

Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu pahala pema Peponi. Amin.

Tuesday, June 10, 2014

KIKWETE ASHIRIKI MAZISHI YA MZEE SMALL

 Rais Kikwete akisaini Kitabu cha Maombolezo
 Rais Dkt Jakaya Mrisho Kikwete akiwa amejumuika na waombolezaji mbali mbali kwenye Msiba wa msanii maarufu wa filamu za vichekesho nyumbani kwa marehemu Tabata Kimanga jijini Dar es salaam leo Juni 9, 2014.Kusoto ni Rais wa Chama cha Filamu nchini,Simon Mwakifwamba na kulia ni Mtoto wa Small Ngamba
 
Mama Salma Kikwete akimpa pole mjane wa Marehemu Saidi Ngamba “Mzee Smal” wakati alipokwenda kuhani msiba wa msanii huyo maarufu wa filamu za vichekesho nyumbani kwa marehemu Tabata Kimanga jijini Dar es salaam leo Juni 9, 2014.
 


Rais Dkt Jakaya Mrisho Kikwete akishiriki katika dua wakati alipokwenda kuhani msiba wa msanii maarufu wa filamu vichekesho Marehemu Saidi Ngamba “Mzee Small” nyumbani kwa marehemu Tabata Kimanga jijini Dar es salaam leo Juni 9, 2014.  
Rais Dkt Jakaya Mrisho Kikwete na Mama Salma Kikwete wakiwafariji wafiwa wakati walipokwenda kuhani msiba wa msanii maarufu wa filamu vichekesho Marehemu Saidi Ngamba “Mzee Small” nyumbani kwa marehemu Tabata Kimanga jijini Dar es salaam leo Juni 9, 2014

KARIA KUFUNGUA KOZI YA MAKOCHA LEO, MWANAKATWE KUZIKWA BABATI

Makamu wa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia atakuwa mgeni rasmi kwenye uzinduzi wa kocha ya makocha wa mpira wa miguu ya Leseni B inayotambuliwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF).

Uzinduzi wa kozi hiyo ya wiki mbili utafanywa leo (Juni 10 mwaka huu) saa 6 mchana kwenye hosteli za TFF zilizopo Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume jijini Dar es Salaam.

Makocha zaidi ya 20 wenye Leseni C kutoka Tanzania Bara na Zanzibar wanashiriki katika kozi hiyo inayoendeshwa na Mkufunzi wa CAF, Sunday Kayuni. Mkufunzi mwingine wa kozi hiyo anayetambuliwa na CAF ni Mkurugenzi wa Ufundi wa TFF, Salum Madadi.

KANALI MWANAKATWE KUZIKWA LEO BABATI
Maziko ya aliyekuwa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wakati huo likiitwa FAT, Kanali mstaafu Ali Hassan Mwanakatwe yanafanyika leo (Juni 10 mwaka huu) Magugu, Babati mkoani Manyara.

Kanali Mwanakatwe alifariki dunia Juni 7 mwaka huu katika Hospitali Kuu ya Jeshi (GMH) Lugalo jijini Dar es Salaam wakati akipatiwa matibabu baada ya kuanguka bafuni nyumbani kwake Mbezi Beach.

TFF imetoa ubani wa sh. laki tano kwa familia ya marehemu Kanali Mwanakatwe, na katika maziko hayo inawakilishwa na mjumbe wa Kamati ya Utendaji wa Kanda ya Arusha na Manyara, Omari Walii.

AMBUNDO, SHIZA WATESA UHOLANZI

Wachezaji wa Tanzania walioko Uholanzi, Dickson Ambundo na Shiza Yahya wameanza kuonekana muda na waandaaji ya mashindano ya AEGON Copa Amsterdam.

Kwa mujibu wa wakala wa wachezaji wa Uholanzi, Denis Kadito, AEGON Copa Amsterdam ni mashindano ya kimataifa yanayoshirikisha timu kubwa kutoka nchi mbalimbali ulimwenguni kwa wachezaji wa miaka chini ya 19.

Kwa Uholanzi, Ajax Amsterdam huwa lazima washiriki, na pia huwa kuna timu ya ridhaa inayotengenezwa kwa kuchagua “best talent” kutoka Uholanzi. Mchujo wa wachezaji hao kutengeneza timu ya kombaini, ulianza na wachezaji wasiopungua 1,000.Kombaini hiyo inaitwa Men United na inafundishwa na mchezaji wa zamani wa kimataifa wa Uholanzi, Ronald de Boer. Ronald e Boer ni pacha wa kocha wa Ajax (First team).

Ronald de Boer pia ni kocha wa wachezaji washambuliaji wa Ajax. Shiza na Ambundo waliingizwa kwenye mchujo na wakafanya vizuri, mwishoni wakaitwa kwenye timu ya wachezaji 18 waliotengeneza timu ya Men United. Hii ni mara ya kwanza wachezaji wasio Waholanzi kuingizwa katika timu hiyo.

Mashindano ya Copa Amsterdam yameanza juzi (Juni 8 mwaka huu) na yanaisha kesho (Juni 11 mwaka huu. Katika mashindano hayo kuna makundi mawili. Kundi A ni AFC Ajax (Amsterdam), Ajax Cape Town ( Afrika Kusini), Fluminense (Brazil), Hamburg SV (Ujerumani) wakati B ni Men United, Panathinaikos (Ugiriki), FC Aerbin (China) na Cruizero (Brazil).

Shiza na Ambundo wamecheza mechi zote tatu. Shiza amekuwa akicheza namba tatu wakati Ambundo anapiga namba tisa, saba na kumi na moja.

Sunday, June 8, 2014

BREAKING NEEEWS. MZEE SMALL AFARIKI DUNIA



HABARI ZILIZOTUFIKIA HIVI PUNDE ZIMEELEZA KUWA, MSANII MKONGWE WA SANAA ZA MAONYESHO NCHINI, MZEE SMALL AMEFARIKI.

KWA MUJIBU WA HABARI HIZO, MZEE SMALL AMEFARIKI USIKU WA KUAMKIA LEO KATIKA HOSPITALI YA TAIFA MUHIMBILI, AMBAKO ALIKUWA AMELAZWA AKIPATIWA MATIBABU.

MZEE SMALL ATAKUMBUKWA KUTOKANA NA MCHANGO WAKE KATIKA KUKUZA NA KUENDELEZA SANAA ZA MAONYESHO NCHINI.

MBALI NA KUPITIA KATIKA VIKUNDI MBALIMBALI MAARUFU, ALIWAHI KUMILIKI KUNDI LAKE LA SANAA LILILOKUWA LIKIJULIKANA KWA JINA LA AFRO DANCE. KUNDI HILI LILIWAHI KUFANYA MAONYESHO NCHINI UJERUMANI MIAKA YA 1990.

MZEE SMALL PIA NI MMOJA WA WAANZILISHI WA BONGO MOVIE BAADA YA KUTAMBA KATIKA MAIGIZO YA KWENYE STEJI.

MUNGU AIWEKE ROHO YAKE MAHALI PEMA.

TFF YATUMA RAMBIRAMBI MSIBA WA MWANAKATWE

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha aliyekuwa Katibu Mkuu wake (wakati huo ikiitwa FAT), Kanali mstaafu Ali Hassan Mwanakatwe kilichotokea leo asubuhi (Juni 7 mwaka huu) katika Hospitali Kuu ya Jeshi (GMH) Lugalo jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa binti wa marehemu, Sophia, baba yake alianguka bafuni nyumbani kwake Mbezi Beach ambapo alikimbizwa katika Hospitali ya Lugalo ambapo ndipo umauti ulipomfika wakati madaktari wakimpatia matibabu.

Kanali Mwanakatwe alichaguliwa kuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Mpira wa Miguu Tanzania (FAT) katika uchaguzi uliofanyika mwaka 1993 mjini Kibaha mkoani Pwani.

Baada ya kuondoka FAT, aligombea nafasi ya Katibu Mkuu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) na kufanikiwa kushinda katika uchaguzi uliofanyika mwaka 1997.

Msiba huo ni mkubwa katika fani ya mpira wa miguu nchini na Afrika kwa ujumla kwani, Kanali Mwanakatwen enzi za uhai wake alitoa mchango mkubwa akiwa kiongozi, na mkufunzi wa utawala wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF). Pia aliwahi kuwa Kamishna wa CAF.

TFF tunatoa pole kwa familia ya marehemu Kanali Mwanakatwe, DRFA, na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.
Taratibu za mazishi zinaendelea kufanywa na familia yake nyumbani kwake Mbezi Beach karibu na hoteli ya Giraffe wakati ndugu wakisubiriwa kutoka mikoani. TFF tunasubiri taratibu hizo ili tujipange jinsi ya kushiriki katika msiba huo.
Sisi sote ni waja wake Mola. Hakika kwake tutarejea.

GEBO PETER KUZIKWA MOROGORO


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha mchezaji wa zamani wa timu ya Simba na Taifa Stars, Gebo Peter kilichotokea usiku wa kuamkia leo (Juni 6 mwaka huu) katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) jijini Dar es Salaam.

Gebo aliyezaliwa mwaka 1961, pia aliwahi kuchezea timu za Sigara ya Dar es Salaam, CDA ya Dodoma na kombaini ya Mkoa wa Dar es Salaam (Mzizima United). Hadi mauti yanamkuta alikuwa akijishughulisha na biashara, kubwa ikiwa ya vifaa vya michezo.

Msiba huo ni mkubwa katika familia ya mpira wa miguu nchini kwani, Gebo enzi za uhai wake alitoa mchango mkubwa akiwa mchezaji na baadaye kiongozi katika timu ya Manyema ya jijini Dar es Salaam.

TFF tunatoa pole kwa familia ya marehemu Gebo Peter, klabu ya Manyema na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.

Msiba upo nyumbani kwao Vingunguti karibu na Kanisa Katoliki ambapo taratibu za mazishi zinaendelea kufanywa na familia.

Marehemu ambaye ameacha mjane na watoto watatu anatarajiwa kuzikwa kesho (Juni 7 mwaka huu) nyumbani kwao Kigurunyembe, mjini Morogoro.

Bwana alitoa, na Bwana ametwaa. Jina lake lihimidiwe. Amina
 

TAIFA STARS KUINGIA KAMBINI JUNI 11



Kikosi cha Taifa Stars kinaingia tena kambini Jumatano (Juni 11 mwaka huu) ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mechi ya raundi ya pili ya michuano ya Afrika dhidi ya Msumbiji itakayochezwa Julai 20 mwaka huu jijini Dar es Salaam.

Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager itakuwa na kambi ya siku tatu jijini Dar es Salaam ikijumuisha wachezaji 28. Kwa mujibu wa programu ya Kocha Mart Nooij, Stars itaingia tena kambini Juni 24 mwaka huu.

Wachezaji wanaotakiwa kuripoti kambini ni Deogratias Munishi, Aishi Manula, Benedictor Tinoko, Kelvin Yondani, Said Moradi, Nadir Haroub, Joram Nason, Shomari Kapombe, Oscar Joshua, Edward Charles, Aggrey Morris na Pato Ngonyani.
Wengine ni Mwinyi Kazimoto, Frank Domayo, Amri Kiemba, Erasto Nyoni, Jonas Mkude, Said Juma, Haruna Chanongo, Himid Mao, Said Ndemla, John Bocco, Simon Msuva, Kelvin Friday, Ramadhan Singano, Khamis Mcha, Mrisho Ngasa na Mwegane Yeya.

HATUJAFUTA MATUMIZI YA TIKETI ZA ELEKTRONIKI-TFF



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea taarifa za kutolewa
wito bungeni wa kulitaka litumie tiketi za elektroniki katika kukusanya
mapato.

Tunataka ieleweke wazi kwa umma wa Watanzania kuwa si nia yetu
kuchelewesha matumizi ya uingiaji mpirani kwa tiketi za elektroniki. Ieleweke
kuwa mfumo wa kuingia kwenye mbuga, KCMC, mipakani ni tofauti na uingiaji
mpirani.

Katika mpira wa miguu wanaingia maelfu ya watu katika kipindi kifupi. Kwa kuzingatia umuhimu wa kulinda usalama wa watazamaji na miundombinu ya viwanja ndio maana tulisitisha matumizi ya tiketi za elektroniki hadi tujihakikishie usalama wa matumizi yake.

Tunafanya jitihada kwa karibu na mzabuni benki ya CRDB ili kuhakikisha mfumo huu unaanza kutumika mara moja.

Kwa niaba ya sekta ya michezo tunatoa wito kwa Serikali kushusha au kuondoa kodi kubwa zinazotozwa kwenye vifaa vya michezo, hasa vinavyotumiwa na watoto kuanzia umri wa miaka 6-12, ili watoto wetu waweze kuvipata kirahisi toka kwa wazazi wao ili waweze kujifunza kucheza michezo kisasa tangu wakiwa wadogo.

HATMA YA WAMBURA KUGOMBEA SIMBA KESHO



Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) inakaa Jumatatu (Juni 9 mwaka huu) kusikiliza rufani moja inayopinga uamuzi wa Kamati ya Uchaguzi ya Simba.

Michael Wambura amewasilisha rufani yake TFF akipinga uamuzi wa Kamati ya Uchaguzi ya Simba iliyomwengua katika kinyang’anyiro cha kuwania urais katika uchaguzi wa klabu hiyo unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu.

Kamati hiyo inayoongozwa na Wakili Julius Lugaziya itakutana saa 5 asubuhi kwenye hoteli ya Courtyard iliyopo Upanga, jijini Dar es Salaam.

NYOTA WAWILI COPA WAENDA BRAZIL
Wachezaji wawili waliochaguliwa kwenda kwenye kambi ya Copa Coca-Cola ya Dunia nchini Brazil wamekabidhiwa bendera tayari kwa safari hiyo inayofanyika leo (Juni 4 mwaka huu).

Hafla ya kukabidhi bendera hiyo kwa Ali Shabani Mabuyu na Juma Yusuf imefanyika leo katika hoteli ya Hyatt Regency jijini Dar es Salaam. Naibu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo katika Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Juliana Yassoda ndiye alikabidhi bendera.

Wakati Mabuyu kutoka Ilala alikuwa mchezaji bora wa michuano ya Copa Coca-Cola kwa vijana wenye umri chini ya miaka 15 kwa mwaka 2013/2014, Yusuf kutoka Zanzibar ndiye aliyeibuka mfungaji bora katika michuano hiyo.

Wachezaji hao watakuwa katika kambi hiyo itakayokuwa katika Jiji la Sao Paulo kwa siku kumi ambapo watafundishwa masuala mbalimbali ya mpira wa miguu. Pia watashuhudia mechi ya ufunguzi ya Fainali za Kombe la Dunia katika ya wenyeji Brazil na Croatia itakayochezwa Juni 12 mwaka huu.

Wednesday, June 4, 2014

DK. FENELLA KUZINDUA SIKU YA MSANII TANZANIA


WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo Dk. Fenella Mukangara keshokutwa anatarajiwa kuzindua Siku ya Msanii Tanzania katika sherehe zitakazofanyika katika hoteli ya Sea Cliff Dar es Salaam.

Akizungumza jana mjini Dar es Salaam, Ofisa Habari wa Mradi wa Siku ya Msanii Tanzania, Petter Mwendapole, alisema Dk. Mukangara amepewa jukumu hilo kutokana wizara yake kuhusika moja kwa moja sanaa.

“Waziri amekubali jukumu la kuwa mgeni rasmi kwa sababu wizara yake ndio mama wa wasanii, na anaelewa matatizo ya wasanii na amekubali kuwa kulibeba jukumu hilo na atakuwepo na timu nzima ya wizara,” alisema.

Mkurugenzi wa Masoko wa Basata wa Vivian Shaluwa alisema siku ya Msanii ilibuniwa mwaka 2004 lakini Tanzania iliamua kuichukua na kuianzisha mwaka 2008 lakini baada ya mchakato wa muda mrefu, kampuni ya Haak Neel imepewa jukumu la kusimamia kazi hiyo.

“Siku ya Msanii itahusisha sanaa mbalimbali kuanzia urembo, muziki wa dansi, uchoraji, unenguaji, lakini pia siku ya Msanii ambayo tamati yake itakuwa Oktoba 25 itakuwa na tuzo za aina mbalimbali kutambua mchango wao,” alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Haak Neel Production, Godfrey Katula alisema kampuni yake imejiandaa vyema kusimamia shughuli hiyo na kuwataka wadau mbalimbali kuhakikisha wanatumia vyema siku ya Msanii katika kutambulisha kazi.

“Haak Neel imejipanga kushirikiana na wasanii katika kutambua siku yao, tumeona kuna siku ya wanawake duniani, kuna Mei Mosi, kwa ajili ya wafanyakazi, kuna siku ya ukimwi kwa hiyo hii ni heshima kwa wasanii kutambuliwa kwa siku yao.”

Mbali na viongozi wa BASATA, Kamati ya Siku ya Msanii inahusisha wasanii kutoka sekta mbalimbali za sanaa ambao ni pamoja na Philemon Mwasanga, Asia Idarous, Kimera Billa, Abdul Salvador, Adrian Nyangamale, Sulemani Ling’ate.

AZAM YAZIMWAGIA MAMILIONI TIMU ZA LIGI KUU


KAMPUNI ya Azam Media imetangaza kuwa tayari imeshatuma fedha kwa Bodi ya Ligi kwa ajili ya msimu wa ligi wa Vodacom kwa mwaka 2014/ 2015.


Fedha hizo zimetolewa mapema zaidi kwa ajili ya kusaidia maandalizi mapema kwa timu kama ilivyokubaliwa kwenye mkataba wa miaka mitatu ya udhamini wao katika ligi hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari jana katika ofisi za Azam zilizopo Tazara, Dar es salaam, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Azam Media, Rhys Torrington, alisema kuwa kampuni hiyo inavutiwa na aina nzuri ya ushirikiano kati yake na bodi ya Ligi.

Alisema kuwa kupitia bodi hiyo Azam imepiga hatua kubwa katika kufanikisha adhma yake ya kuifanya Ligi hiyo ya Vodacom kuwa ya kuvutia zaidi.

“Ligi hii tunataka kuifanya kuwa ni moja kati ya ligi zinazovutia na kuonesha ushindani barani Afrika, ingawaje ninajua kuwa kuna mengi ambayo yanatakiwa kuendelea kufanywa ili kuipa nguvu zaidi ligi hii”alisema Torrington.

Alisema kuwa kwa kutambua hilo ndio maana Azam Media imehakikisha kuwa klabu zote zinapata fedha mapema ili kusaidia suala zima la maandalizi.

Akizungumzia mikakati ya baadae ya Azam Media alisema kuwa inatarajia kuanza kuonesha soka la mitaani (street soccer) mbalimbali moja kwa moja (live) itakayokuwa ikiendelea kwenye nchi za Kenya na Uganda.

Alisema kuwa kwa sasa Azam Media imeanza kujikita katika nchi za Kenya, Uganda na Malawi ambapo itakuwa ikiuza ving’amuzi vyake katika nchi hizo.

Aliongeza kuwa pia katika kuhakikisha kuwa inatoa mwanya zaidi wa vipindi vizuri na vya kuvutia inaendelea na vipindi vya michezo vya Morning Trumpet, sport@8 pamoja na Kwetu House.

Kwa upande wake Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya ligi, Mr Silas Mwakibinga alisema kuwa kwa hatua hiyo ya Azam ya kuhakikisha upatikanaji wa fedha hizo kwa wakati ni nzuri na itasaidia kuzipatia timu muda mzuri wa kujiandaa.

Alisema kuwa bodi yake inavutiwa sio tu na utangazaji wa vipindi unaofanywa na Azam bali pia hata nia yao ya kuendeleza soka la Tanzania.

Azam Media ilisaini mkataba wa miaka mitatu na wenye thamani ya TSHS 5,560,800,000 kuonesha mechi za live na za kurekodi mechi za Ligi Kuu na fedha hizo zinalipwa kwa awamu tatu.

TFF YATUMA RAMBIRAMBI MSIBA WA KIONGOZI FAM



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha Mwakilishi wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Mara (FAM) katika Mkutano Mkuu wa TFF, William Chibura kilichotokea leo asubuhi (Juni 3 mwaka huu) katika Hospitali ya Mkoa wa Mara mjini Musoma.

Chibura aliyezaliwa mwaka 1969 alikuwa mjumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF akiwakilisha klabu za Mkoa wa Mara kupitia FAM. Aliwahi kuichezea Musoma Shooting, na baadaye kuwa kiongozi katika klabu hiyo na ile ya Polisi Mara iliyoko Ligi Daraja la Kwanza (FDL).

Hadi mauti yanamkuta alikuwa kiongozi wa Butiama FC, na mwakilishi wa klabu Chama cha Mpira wa Miguu Wilaya ya Butiama (MUFA) kwenye Mkutano Mkuu wa FAM.

Msiba huo ni mkubwa katika fani ya mpira wa miguu nchini kwani, Chibura enzi za uhai wake alitoa mchango mkubwa katika mchezo huu tangu akiwa mchezaji na baadaye kiongozi.

TFF tunatoa pole kwa familia ya marehemu Chibura, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Mara (FAM), Jeshi la Polisi Tanzania na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.

Taratibu za mazishi zinaendelea kufanywa na familia yake kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi Tanzania- Mkoa wa Mara, kwani marehemu Chibura alikuwa mtumishi wa jeshi hilo. TFF tunasubiri taratibu hizo ili tujipange jinsi ya kushiriki katika msiba huo.

Bwana alitoa, na Bwana ametwaa. Jina lake lihimidiwe. Amina.

Sunday, June 1, 2014

TAIFA STARS YASONGA MBELE AFRIKA




Na Mwandishi Wetu, Harare


TIMU ya soka ya Taifa, Taifa Stars imesonga mbele katika michuano ya awali ya kuwania ubingwa wa Afrika baada ya kutoka sare ya mabao 2-2 na Zimbabwe.

Katika mechi hiyo ya marudiano iliyochezwa mjini Harare, mabao ya Taifa Stars yalifungwa na beki Nadir Haroub 'Cannavaro' na mshambuliaji Thomas Ulimwengu.

Sare hiyo imeiwezesha Stars kusonga mbele kwa ushindi wa jumla wa mabao 3-2, kufuatia ushindi wa bao 1-0 ilioupata wiki mbili zilizopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Zimbabwe ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya tatu kabla ya Cannavaro kusawazisha dakikaya 21 baada ya kuunganisha wavuni kwa kichwa mpira wa kona uliopigwa na Simon Msuva. Mabao hayo yalidumu hadi mapumziko.

Kipa Deogratius Munish 'Dida' aliibuka shujaa wa Taifa Stars, kufuatia kuokoa mipira mingi ya hatari iliyopigwa kwenye lango la timu yake, ikiwa ni pamoja na kuwavaa washambuliaji wa Zimbabwe bila woga.

Taifa Stars ilipata bao la pili dakika ya 46 kupitia kwa Ulimwengu, aliyetumia vyema uzembe wa mabeki wa Zimbabwe waliojisahau.

Zimbabwe ilisawazisha dakika ya 54 baada ya kufanya shambulizi la kushtukiza kwenye lango la Taifa Stars. Bao hilo lilifungwa na Denver Mukamba.

Katika kipindi hicho cha pili, Kocha Mart Nooij alifanya mabadiliko kwa kuwaingiza Mrisho Ngassa, Frank Domayo na Said Mourad kuchukua nafasi za Simon Msuva, Amri Kiemba na Thomas Ulimwengu.

Taifa Stars: Deo Munishi ‘Dida’, Shomary Kapombe, Oscar Joshua, Nadir Haroub
‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Mwinyi Kazimoto, Simon Msuva/Said Mourad dk78,
Amri Kiemba/Frank Domayo dk62, John Bocco, Thomas Ulimwengu/Mrisho Ngassa
dk88 na Erasto Nyoni.

WAGOMBEA SITA WAENGULIWA UCHAGUZI WA SIMBA




KAMATI ya Uchaguzi ya klabu ya Simba, imewaengua wagombea sita kuwania nafasi walizoomba katika uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika Juni 29 mwaka huu.

Wagombea walioenguliwa ni Selemani Dewji, Ahmed Mlanzi, Emmanuel Kazimoto, George Wakuganda, Omari Omari, Ramson Ritiginga na Salim Jaza waliokuwa wakiwania nafasi ya ujumbe.

Mbali na kuenguliwa kwa wagombea hao, wengine watano wamejitoa kutokana na sababu mbalimbali. Wagombea hao ni Asha Kigundula, Juma Pinto na Hussein Simba, waliokuwa wakiwania nafasi ya ujumbe.

Wengine ni Joseph Itang'are 'Kinesi' na Emmanuel Mayange waliokuwa wakiwania nafasi ya makamu wa rais.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Damas Ndumbaro, alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, wagombea walioenguliwa ni kutokana na kutokidhi katiba ya Suimba ibara ya 26 (6).

Alisema wagombea hao wamekosa sifa, ambayo inaelezwa katika ibara hiyo, ambayo inamtaka mgombea kuwa mwanachama wa klabu hiyo kwa kipindi kisichopungua miaka mitatu.

Ndumbaro alisema wagombea wengine walikosa sifa, ambayo ipo katika ibara ya 26 (2), ya kuwa na elimu ya sekondari na wengine hawakuwa na vyeti hivyo.

Alisema wagombea waliojiengua walitoa sababu mbalimbali, ambazo kamati yake iliridhika nazo, zikiwemo za kifamilia.

Kwa mujibu wa Ndumbaro, licha ya mchujo uliofanywa na kamati yake, upo uwezekano mkubwa idadi ya wagombea kupungua baada ya uchunguzi unaofanywa na taasisi mbalimbali kwa baadhi ya wagombea kukamilika.

Alisema uchunguzi huo unafanywa na Kamati ya Maadili ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA).

Wagombea waliopitishwa katika mchujo huo wa awali ni Andrew Tupa na Evans Aveva (rais). Wengine ni Bundala Kabulwa, Geofrey Nyange 'Kaburu', Jamhuri Kihwelo na Swedy Nkwabi (makamu wa rais).
Wajumbe ni Ally Suru, Abdulhamidi Mshangama, Alfred Lia, Ally Chaurembo, Amina Poyo, Asha Muhaji, Chano Karaha, Collin Frisch, Damian Manembe, Hamisi Mkoma, Ibrahim Masoud, Iddi Mkambala, Iddi Noor, Jasmin Badour, Juma Musa, Maulid Abdalla, Rodney Chiduo, Saidi Kubenea, Saidi Pamba, Daidi Tully na Yassin Mwete.

MANJI, SANGA WAONGEZEWA MWAKA MMOJA YANGA, MAXIMO ANUKIA KUWA KOCHA



Mkutano Mkuu wa marekebisho ya baadhi ya vipengele kwenye Katiba ya Yanga umefanyika na kumalizika salama na furaha kwenye Ukumbi wa Bwalo la Polisi -Oysterbay huku wanachama wakipitisha kipengele cha kuundwa kwa kamati ya maadili.

Mwenyekiti wa klabu ya Yanga SC Yusuf Manji amewaongoza wanachama hai wapatao 1,560 kupitisha kipengele hicho kipya kwa ajili ya maslahi na faida ya Wana Yanga kwani bila kufanya hivyo timu isingeweza kuruhusiwa kushiriki Ligi Kuu msimu ujao.

Aidha katika mkutano huo Manji amewatoa hofu wanachama kwa kuwaambia kuwa usajili unaendelea kufanyika na nafasi zilizobakia ni nne tu hivyo pindi utakapokamilika basi wataweka wazi kila kitu.

Kuhusu nafasi ya Kocha Mkuu Manji amesema Kamati ya Mashindano imemkabidhi mapendekezo yao na kwa sasa yupo kwenye mazungumzo na Marcio Maximo aliyewahi kuwa kocha mkuu wa timu ya Taifa Tanzania kuja kukinoa kikosi cha Jangwani.

Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini Mama Fatma Karume aliongoza kikao cha waachama kilichomuomba Bw Manji kuendelea na uongozi ambapo mwenyeikti alitoka nje na kamati yake ya utendaji na pindi waliporejea walikubali ombi hilo na kusema watafuata taratibu za kikatiba.

Mwisho kupitia mkutano mkuu wa leo wa wanachama umeazimia kuwaongezea muda wa mwaka mmoja Mwenyekiti Yusuf Manji pamoja na Makamu wake Clement Sanga ili waweze kukamilisha masuala ya katiba na kuweza kuandaa mkutano wa uchaguzi baada ya katiba kupitishwa na TFF

MWASISI WA BONGO MOVIE AFARIKI KATIKA AJALI






Taarifa zilizotufikia hivi punde zinasema mongozaji wa filamu maarufu nchini George Otieno Tyson (Pichani) amefariki dunia kwa ajali ya gari huko Morogoro.

Taarifa hizi ambazo zimethibitishwa na watu wa karibu yake zinasema kuwa, mauti haya yamemfika baada ya gari walilokuwa wakisafiria kupata ajali na kupinduka walipokuwa wameenda kwa ajili ya kipindi cha The mboni show ambacho yeye alikuwa ndiye muongozaji mkuu.

Wasanii na mastaa mbalimbali nchini wameoneshwa masikitiko yako juu ya kifo hichi ikikumbukwa kuwa ni siku tano tu zimepita tangu mwigizaji Rachel Haule alipotutoka.

Batuli: - Niongee nini, niseme nini Mwenyezi Mungu tusamehe sie waja wako, Yarabbi eeeeeh Mola wng, R.I.P My brother, My shemeji, My director......Eeeeeh Mola mpokee George Tyson wetu, Poleni wasanii wenzangu, Poleni team nzima ya the mboni show thembonishow Pole Monalisa wangu

Rose Ndauka: Ki ukweli sina LA kusema ila asante baba wa mbinguni kwa kila jambo. ...mola mpokee ndugu yetu, kwa mikono salama na umlaze pema peponi ameen.....R.I.P George Tyson.

Agness Masogange: R.I.P George tyson mm siamin bado jmn E Mungu tuhurumie waja wako!

Flaviana Matata : This is very sad aisee,Rest In Peace Tyson.Mungu kakupenda zaidi, - monalisa pole sana dadangu,Mwenyezi Mungu awatie nguvu

Wema Sepetu - Kwa mara ya tatu bila hata kupumzika week... tunamzika mwenzetu mwingine... George Tyson.... Dah... Im just speechless.. RIP brother... Dah sijui Da Mboni wangu ana hali gani aisee.... Pole dada akee ... Mungu akupe nguvu wewe pamoja na team yote ya @thembonishow .... Pigo kubwa tena kwa wasanii.... Tunaisha tu jamani.

Aunty Ezekiel - Mungu wang Naomba useme na sisi jaman Mungu baba tuone sisi jaman Naumia siwezi elezea jaman RIP Tyson wang jaman Rip director .....Nakosa lakusema

Mohamed Mwikongi : Hakika yametufika, A film director George Otieno Tyson naye hatunae tena duniani.

George Tyson aliwahi kuwa mume wa mwigizaji Monalisa na kuweza kuzaa naye mtoto mmoja. Mung ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi.

FAMILIA YA AMINA NGALUMA YAISHUKURU JAMBO SURVIVOR





FAMILIA ya aliyekuwa mwimbaji mahiri nchini marehemu Amina Ngaluma ‘Japanese’, imeishukuru bendi ya Jambo Survivor ya Thailand kwa ushirikiano mkubwa iliyoutoa mpaka kufanikisha kuletwa Dar es Salaam kwa mwili wa mwimbji huyo na hatimaye kuzikwa.

Pia imewashukuru wadau wa muziki na Watanzania kwa ujumla kwa ushirikiano mkubwa na kuwafariji wakati wote wa kipindi kigumu cha kuondokewa na mpendwa wao aliyezikwa Mei 24 mwaka huu Kitunda, Machimbo Dar es Salaam.

Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana na mume wa mwimbaji huyo, Rashid Sumuni ilisema hawana cha kuwalipa badala yake Mwenyezi Mungu ndiye atakayejua cha kuwalipa.

“Mimi binafsi na familia ya Mzee Ngaluma, tunaishukuru bendi ya Jambo Survivor ya Thailand chini ya kiongozi wake Hassan Shaw kwa juhudi zao walizofanya mpaka kuuleta mwili hapa nyumbani.

“Hatuna tatizo nao na tunawatakia kila la heri katika kazi zao, juhudi walizofanya wakati wanataka kuokoa uhai wa mke wangu alipougua ghafla tunazithamini sana, pia msaada wao kwetu kuuleta mwili Dar es Salaam ni kubwa na tunautambua,” alisema Sumuni.

Pia alisema masuala yote yanayohusiana na msiba huo wasemaji ni familia na kueleza kuwa hwatahusika na mtu mwingine yeyote atakayekuwa anatoa kauli ambazo hakutumwa na familia yao.

“Tunawashukuru mashabiki wa Amina, wdau wa muziki na Watanzania wote waliokuwa nasi bega kwa bega wakati wa msiba. Sote tumuombee mwenzetu dua njema,” alisema Sumuni.

Ngaluma aliyepata kung’ara na bendi mbalimbali nchini, alifariki dunia Mei 15 mwaka huu kwa shinikizo la damu akiwa Thailand alikokuwa akifanya shughuli za muziki katika bendi ya Jambo Survivor.

Wakati wa uhai wake alitamba na bendi mbalimbali zikiwemo African Revolution ‘Tamtam’, Double M Sound ‘Mshikemshike’ na TOT Plus zote za Dar es Salaam.

Pia alipigia makundi ya Arusha Sangoma, Sayari Band na Less Mwenge yote ya Arusha na Mangelepa na Sky Sound za Kenya na amepata kufanya kazi Omani na Dubai na kutunga vibao mbalimbali vilivyopendwa na mashabiki.

WANAMICHEZO BORA TASWA KUPEWA TUZO JUNI 27


Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), kinatarajia kutoa tuzo za Wanamichezo Bora wa Tanzania wa mwaka 2013, Juni 27 mwaka huu.

TASWA inaomba radhi kutokana na kushindwa kufanya tuzo mwaka jana na hiyo ilitokana na sababu mbalimbali ikiwemo wadhamini kujitoa dakika za mwisho.

Kutokana na hali hiyo, TASWA kwa kushirikiana na Kamati Maalum ya Kusimamia Tuzo hizo imeanza tena mchakato wa kuwazawadia wanamichezo waliofanya vizuri kuanzia Januari 2013 hadi Aprili 2014.

Kamati imevipa jukumu vyama vya michezo mbalimbali kupendekeza majina ya wanamichezo wao waliofanya vizuri kwa kipindi hicho, isipokuwa kwa mpira wa miguu wa wanaume jukumu hilo limekabidhiwa kwa wahariri wa habari za michezo Tanzania.

Kutokana na hali hiyo, naomba upendekeze majina ya wanasoka bora watano wa Tanzania unaoona wanafaa kuwania tuzo hiyo kwa mwaka 2013/2014. Itapendeza ukitaja katika mapendekezo yako sababu zako kwa nini unafikiri anafaa kuwania tuzo hiyo.

Baada ya Kamati ya Tuzo kupitia majina yote, hatua itakayofuata itateua matatu yaliyopendekezwa sana na kuyarudisha kwa wahariri ili yapigiwe kura kuchagua mmoja.