KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, August 26, 2010

RAGE: Tujenge tabia ya kuwaamini wachezaji wetu


SWALI: Ukiwa Mwenyekiti wa Simba, kumekuwa na tabia kwa baadhi ya viongozi, wanachama na mashabiki wa klabu hiyo na watani wenu wa jadi Yanga kuwatuhumu wachezaji kupokea rushwa kutoka kwa timu pinzani kila inapotokea timu yenu kufungwa na wapinzani wenu wa jadi. Je, unazungumziaje tuhuma za aina hii?
JIBU:Hakika leo umenifurahisha kwa kuniuliza swali hilo. Kwa kweli mimi binafsi na viongozi wenzangu wa Simba tunapinga mawazo ya watu hao, kwani tunapoamua kusajili mchezaji, ina maana kwamba tuna imani naye kwa ajili ya kutufanyia kazi na ni jukumu letu kumlipa mshahara mzuri ili aweze kutufanyia kazi nzuri.
Licha ya jambo hilo, unajua timu kama Simba ina watu wengi, ambao wengine wana uwezo wa kufikiria mambo na wengine hawana, hivyo wapo watu kila kukicha wanafikiria kutaka kukuza migogoro ili waweze kufanikisha malengo yao.
Kwa kweli watu wanaoeneza tuhuma kwamba mchezaji fulani amehongwa, wamekuwa wananikera sana na sio siri wakija kwangu kama hawana ushahidi, lazima nitawachukulia hatua kali. Nina imani ndani ya kikosi cha Simba tabia hizo hazipo na hao wanaoeneza mambo hayo huenda ni wapinzani wetu.
Katika mechi yetu na Simba, tuliona jinsi wachezaji walivyojituma na mpaka hatua ya kupigiana penalti ilipofika, tuliona kabisa kuwa walifanyakazi waliyotumwa na klabu. Kama wangekuwa na ajenda ya kutufungisha, kwanini wasingefanya hivyo mapema katika muda wa dakika 90? Hizo ni kauli za watu, ambao wana nia mbaya na klabu yetu, ambayo kwa sasa imetulia kutokana na kuwepo ushirikiano mkubwa.
SWALI: Kufuatia kuwepo kwa tetesi hizo, ukiwa mwenyekiti wa Simba, unachukua hatua gani ili kukomesha tabia hii?
JIBU: Zipo taratibu tunazopaswa kuzifuata. Siwezi kufanyakazi kwa mazoea. Kama kweli mtu anafanya hivyo, ni vyema akaacha kwani tutamchukulia hatua kali kulingana na sheria kwani zipo sheria kuhusu suala hilo, zinasubiri mtu afanye kosa akumbane nazo. Cha msingi ni kwamba nawaomba wanachama wenzangu wa Simba, kama wapo waliokuwa wakizusha tuhuma hizo, waache mara moja kutamka maneno ya namna hiyo kwani yanavunja moyo wachezaji.
Mimi nasisitiza kwamba wachezaji wetu wanapata matunzo mazuri, mishahara mizuri na kila kitu wanakipata muda wowote wanapokihitaji kwa hiyo watu wanaoeneza uvumi huo pengine ni wapinzani wetu Yanga.
Simba kuna watu wenye heshima zao, inawezekana wapinzani wetu wanataka kutumia njia ya kutugombanisha ili mawazo yao ya kutaka kuchukua ubingwa yaweze kutimia. Hilo tumeligundua na tupo makini sana.
Nawaomba wanachama na wapenzi wa Simba watuamini sisi viongozi wao na wachezaji kwa vile sifikiri kama kuna mchezaji, ambaye anaweza kufanya hivyo. Ni vyema tukajenga imani kwa wachezaji wetu ili waweze kufanyakazi tuliyowapa kwa uaminifu.
SWALI: Uongozi uliopita chini ya Mwenyekiti Hassan Dalali ulileta mafanikio makubwa kwa Simba, ikiwa ni pamoja na kutwaa ubingwa wa ligi kuu kabla haijamalizika. Nini mikakati ya uongozi wako katika ligi ya msimu huu na michuano ya klabu bingwa Afrika?
JIBU: Uongozi umepanga malengo yake. Lakini tupo sambamba na benchi la ufundi la timu yetu ili tuweze kutimiza ahadi na mambo ambayo tumekubaliana. Ninachoweza kusema ni kwamba, tunapaswa kulitetea taji letu na pia kufanya vizuri katika michuano ya Afrika.
Matarajio yetu ni kuhakikisha kwamba tunapata uwezo wa kufanya mazoezi ya nguvu na kuweka kambi hata nje ya Tanzaniai ili tuweze kuwa na timu yenye uwezo mkubwa wa kushinda mashindano mbalimbali itakayoshiriki.
Kwa sasa, mipango yetu inakwenda vizuri. Hata Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kupitia rais wake, Leodegar Tenga limetupongeza na kuwataka wapinzani wetu Yanga watuige.
Na kwa kweli, mafanikio ya Simba yamekuwa yakiigwa na Yanga. Tazama hata tamasha la ‘Simba Day’ tayari nao wameshaanza kuliiga. Hivyo tutaendelea kuwa wabunifu ili tuiweke Simba katika njia sahihi na pia iweze kujitegemea.
SWALI: Baada ya kuingia madarakani, uliahidi kwamba utasimama imara kuhakikisha Simba inajitegemea na kuongeza vyanzo vyake vya mapato, ikiwa ni pamoja na kusaka wadhamini wapya. Je, umefikia wapi hadi sasa?
JIBU: Mambo hadi sasa yanakwenda vizuri na siku chache zijazo tunaweza kuwatangaza wadhamini wengine. Jambo la kwanza, ambalo tunalipigania kwa sasa ni kuhakikisha jengo letu linakuwa safi na linatumika kutuingizia pesa.
Na kama mlivyoweza kuona, tumeshaanza kulifanyia ukarabati mkubwa kwa kulipaka rangi kwa kutumia uwezo wetu wenyewe na kazi hiyo inakwenda vizuri. Pia tumeanza kufunga viyoyozi kwenye vyumba vyote vya jengo hilo na haya kwetu ni maendeleo makubwa, tofauti na miaka iliyopita.
Sambamba na hilo, tumeweza kusajili nembo ya klabu yetu na nimeshatoa siku 90 kwa mtu yeyote, anayeuza vifaa vyenye nembo ya Simba kuacha mara moja kufanya hivyo, vinginevyo hatua kali zitachukuliwa dhidi ya watu hao baada ya muda huo kumalizika.
SWALI: Uongozi wa Simba unayo mikakati yoyote ya kuhamishia kambi ya timu yenu kwenye jengo la klabu badala ya kwenye hoteli za kitalii kwa lengo la kupunguza gharama?
JIBU: Hilo linawezekana, lakini ningependa kuona kwanza kazi ya kulikarabati jengo hilo inakamilika kwa asilimia mia moja. Kama hali itakuwa nzuri, sioni kwa nini tusiweke kambi klabuni. Jambo la kufurahisha ni kuona kwamba kazi hiyo inakwenda vizuri na kazi zote za Simba kwa sasa zinafanyika klabuni.
SWALI: Vipi kuhusu ufuatiliaji wa viwanja vyenu vilivyopo Boko na pale Jangwani?
JIBU: Kazi hiyo inaendelea kwa mafanikio makubwa licha ya kuwepo mabadiliko kidogo ya kiutendaji kwenye Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, kufuatia mabadiliko yaliyofanywa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, William Lukuvi. Nina imani kwamba tukishakamilisha kazi ya kuvipata viwanja hivyo, tutajua la kufanya. Lakini kazi ya kwanza itakuwa ni kusaka wadhamini.
SWALI: Uongozi wako una sera gani kuhusu kuuza wachezaji nje ya nchi kwani kumekuwepo na taarifa kwamba baadhi ya wachezaji wa Simba wanatakiwa kwenda nje ya nchi kufanya majaribio ya kucheza mpira wa kulipwa?
JIBU: Hili ni jambo zuri kwa klabu kwa sababu endapo mchezaji atafuzu majaribio nje, tutapata pesa na mchezaji naye atanufaika kimaisha. Kwa vile sisi ndio wazazi, kama kuna timu inataka kumfanyia majaribio mchezaji wetu, milango ipo wazi kwa kufuata taratibu husika za TFF na mashirikisho ya soka ya kimataifa.
SWALI: Kwa muda mrefu sasa, kumekuwepo na mchezo mchafu, unaofanywa na baadhi ya watu kutengeneza tiketi feki wakati wa mechi mbalimbali kubwa na za kimataifa na kuziuza kwa mashabiki, hivyo kuzikosesha mapato klabu. Klabu yako imekuwa ikichukua hatua gani kupambana na tatizo hili?
JIBU: Ninachoweza kusema ni kwamba mchezo huo kwetu sisi Simba haupo. Nimekuwa nikisikia tu taarifa hizo kupitia kwenye vyombo vya habari kwamba baadhi ya watu walikamatwa na polisi baada ya kukutwa na tiketi hizo. Lakini sipendi kulizungumzia kwa undani zaidi jambo hilo kwa sababu lipo mahakamani. Isipokuwa kwa upande wetu, akikamatwa mtu ametenda jambo hilo, atachukuliwa hatua za kisheria. Kama wapo watu wa Simba wenye tabia hiyo, ni vyema wakaacha mara moja. Tumejipanga vyema kukabiliana na tatizo hilo.
SWALI: Kwa sasa wewe ni mwenyekiti wa chama cha soka mkoani Tabora, ni mwenyekiti wa Simba na sasa umengia katika kinyang’anyiro cha kuwania ubunge wa jimbo la Tabora Mjini kupitia CCM. Je, utamudu vipi kuvitumikia vyeo vyote hivyo kwa wakati mmoja?
JIBU: Naona ndugu yangu unataka kwenda mbele kwa haraka zaidi. Ninachokuomba ni utulie kwanza na baada ya uchaguzi mkuu kumalizika, ndipo nitakapojua nini la kufanya. Lakini kwa sasa mimi bado ni mwenyekiti wa Simba na Tabora na nitaendelea kushirikiana na viongozi wenzangu kuleta maendeleo katika maeneo ninayoongoza.
SWALI: Kutokana na kauli yako, unataka kusema kwamba iwapo utachaguliwa kuwa mbunge, utafikiria kujiuzulu cheo kimoja katika hivyo vitatu?
JIBU: Ninakuomba vuta subira, utaelewa mambo yote. Mimi ni mtu wa vitendo, kwa maana hiyo nitahakikisha Simba inakwenda mbele na hata chama cha soka cha mkoa wa Tabora kinafanyakazi zake vizuri na nina imani msimu huu tunaweza kupandisha timu ikacheza ligi kuu msimu ujao wa 2011/2012.

Kikwete aahidi makubwa kwa wasanii wa Bongo


Na Mwandishi Wetu, Mwanza
RAIS Jakaya Kikwete ameahidi kuinua maisha ya wasanii wa muziki wa kizazi kipya na wacheza filamu nchini ili waweze kunufaika na vipaji vyao.
Kikwete alitoa ahadi hiyo alipokuwa akihutubia mkutano wa hadhara wa kampeni uliofanyika kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini hapa na kuhudhuriwa na maelfu ya watu.
Mgombea huyo urais kwa tiketi ya CCM alisema, angependa kuona katika kipindi chake cha uongozi, wasanii wa muziki na filamu nchini wanafanana kimaisha na wasanii maarufu duniani.
“Ningependa kuona huko mbele wasanii wa muziki wa kisasa wanafanana kimaisha na akina Madonna, marehemu Michael Jackson na wacheza sinema wote mnaowajua duniani,”alisema.
Katika kutekeleza ahadi yake hiyo, Rais Kikwete alisema tayari ameshaagiza mitambo ya studio kwa ajili ya kurekodi muziki yenye thamani ya sh. milioni 50.
Rais Kikwete alisema pia kuwa, tayari amesharekodi nyumba kwa sh. milioni saba kwa mwaka kwa ajili ya kufunga vifaa hivyo vya muziki, ambavyo vitakuwa mali ya wasanii nchini.
Alisema mara baada ya vifaa hivyo kufungwa, atakuja mtaalamu kutoka Uingereza, ambaye kazi yake itakuwa kuwafundisha wasanii jinsi ya kuitumia. Alisema mtaalamu huyo ataifanyakazi hiyo kwa miaka miwili.
“Lakini hatutaishia hapo. Watakapoanza kuimiliki mitambo hiyo, kazi itakayofuata itakuwa usambazaji wa kazi zao. Wasanii wanadhulumiwa na wanaorekodi. Wanatajirika kwa usambazaji,”alisema Rais Kikwete.
Kwa kutambua kuwepo kwa tatizo hilo, Rais Kikwete alisema wamempa kazi mtaalamu mmoja kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuandaa utaratibu mzuri wa usambazaji wa kazi za wasanii na amelipwa sh. milioni 20 kwa ajili ya kazi hiyo.
Kikwete alisema binafsi anakunwa mno na muziki wa wasanii wa kizazi kipya, hasa mashairi yao na midundo ya ala, lakini hawezi kuucheza kwa sababu ya umri.

BINTI WA MEXICO ASHINDA TAJI LA MISS UNIVERSE 2010


Hellen Dausen

LAS VEGAS, Marekani
MWAKILISHI wa Tanzania katika shindano la Miss Universe 2010, Hellen Dausen juzi alishindwa kung’ara baada ya kutolewa hatua ya awali.
Katika shindano hilo lililofanyika mjini hapa, mrembo Jimena Navarrete (22) wa Mexico aliibuka mshindi baada ya kuwabwaga washiriki wengine 82 kutoka nchi mbalimbali duniani.
Mshindi wa pili alikuwa Yendi Phillipps kutoka Jamaica wakati nafasi ya tatu ilinyakuliwa na Jesinta Campbell kutoka Australia.
Hellen amekuwa mrembo wa nne kutoka Tanzania kushiriki kwenye mashindano hayo na kutolewa hatua za awali. Wa kwanza alikuwa Flaviana Matata mwaka 2007, aliyefuatiwa na Amanda Ole Sululu 2008 na Illuminata Mize mwaka jana.
Jimena alivikwa taji na mshindi wa shindano hilo mwaka jana, Stefania Fernandez wa Venezuela. Amekuwa mrembo wa pili kutoka Mexico kushinda taji hilo tangu mashindano hayo yalipoanzishwa mwaka 1952. Wa kwanza alikuwa Lupita Jones, aliyeshinda taji hilo mwaka 1991.
Mara baada ya kuvikwa taji hilo, Jimena aliweka wazi mipango yake kuhusu kuitangaza Mexico kimataifa.
“Nataka dunia nzima kuifahamu nchi yangu na watu wangu,”alisema Jimena, ambaye asili yake ni Guadalajara.
“Nahisi kwamba watu wote wa Mexico kwa sasa wamepatwa na wazimu kwa furaha,” alisema binti huyo kupitia mkalimani. “Naona fahari na nina hakika nao wanaona fahari kubwa kwa ushindi wangu.”
Mrembo huyo aliyekuwa amevalia gauni refu jekundu lililomfiti vyema mwilini, alipiga picha kadhaa akiwa ameshika bendera ya Mexico kabla ya kupiga picha na mrembo wa kwanza wa nchi hiyo kutwaa taji hilo.
Akizungumzia ushindi huo, Rais wa Mexico, Felipe Calderon alisema ni faraja kubwa kwa watu wa nchi hiyo na utasaidia kuitangaza vyema kimataifa.
“Tumeshinda, idumu Mexico!” Aliandika Jimena kupitia mtandao wa Facebook, ambapo watu 218 walitoa maoni yao kuhusu ushindi wake.
Katika shindano hilo, Jimena na washiriki wenzake walipanda jukwaani wakiwa wamevaa nguo za kitaifa. Baadaye walicheza muziki wakiwa wamevaa nguo za rangi ya fedha zilizonakshiwa kwa rangi nyeusi kabla ya kutangazwa washiriki 15 walioingia fainali.
Washiriki hao 15 walipita jukwaani wakiwa wamevaa nguo za kuogelea huku kundi la muziki la Cirque du Soleil likipiga nyimbo kadhaa za mkongwe Elvis Presley, kikiwemo ‘Viva Las Vegas’.
Kwa ushindi huo, Jimena atakuwa akilipwa mshahara kila mwezi, atapewa nyumba ya kuishi mjini New York, ofa ya masomo ya mwaka mmoja katika shule ya uigizaji sinema na vitu vingine mbalimbali vya thamani.

NEYMAR DA SILVA: Kinda wa Brazil aliyeitolea nje Chelsea





BRASILIA, Brazil
MSHAMBULIAJI nyota na chipukizi wa klabu ya Santos ya Brazil, Neymar da Silva ameitolea nje ofa aliyopewa na klabu ya Chelsea ya England.
Chelsea ilikuwa imejiandaa kuilipa Santos ada ya uhamisho ya pauni milioni 25 za Uingereza, kumpatia mchezaji huyo mkataba wa miaka mitano na malipo ya mshahara wa pauni 55,000 kwa wiki.
Badala yake, Neymar ameamua kuongeza mkataba wa kuichezea klabu yake ya Santos wenye marupurupu mengi zaidi kuliko ule wa awali.
Licha ya shinikizo kutoka kwa familia yake na washauri wake kumtaka ahame, Neymar aliona ilikuwa ni mapema sana kuondoka Brazil na alipatwa na mshtuko kuhusu ofa mpya aliyopewa na Santos.
Santos imemuongezea mshahara Neymar mara tatu zaidi na kufikia pauni 40,000 kwa wiki kutokana na malipo ya udhamini kama ilivyofanya kwa Robinho de Souza, aliyerejea kwenye klabu hiyo kwa mkopo akitokea Manchester City ya England.
Mwanasoka nyota wa zamani wa dunia, Pele, Robinho na Kocha mpya wa timu ya taifa ya Brazil, Mano Menezes kwa nyakati tofauti walimshauri Neymar abaki katika klabu hiyo.
Kadhalika, kocha wa zamani wa timu ya taifa ya Brazil, Mario Zagallo alimtahadharisha chipukizi huyo na kumtaka abaki nchini humo. Zagallo alikaririwa wiki iliyopita akisema kuwa, Neymar hayuko fiti kuweza kukabili mikikimikiki ya ligi kuu ya England, ambako ni wachezaji wachache kutoka Brazil wanaocheza nchini humo.
“Nafikiri ni mapema kwa mchezaji mwenye umri wa miaka 17, 18 au 19 kuondoka Brazil,”alisema Zagallo, ambaye alishinda Kombe la Dunia akiwa na mchezaji wa Brazil mwaka 1958 na 1962 na akiwa kocha mwaka 1970.
“Ni wazi kwamba sikuzote pesa ndicho kishawishi kikubwa kwa wachezaji kutaka kuondoka, lakini kwa suala la Neymar, atakwenda katika mazingira, ambayo si mazuri kwa mwili wake. Anahitajika kuongeza uzito, hivyo ni bora aondoke akiwa na umri wa miaka 21 au 22,”aliongeza.
Menezes, ambaye alimwita Neymar kwa mara ya kwanza katika kikosi cha Brazil, ilipoibwaga Marekani mabao 2-0 wiki iliyopita, aliunga mkono maoni ya Zagallo.
Kufuatia kauli zilizotolewa na wanamichezo mbalimbali, Neymar alisema: “Nimeupokea na kuutafakari kwa makini ushauri niliopewa, lakini uamuzi wa kubaki kwenye klabu ni wa kwangu.”
“Ilikuwa kazi ngumu, lakini nafikiri kwamba Mungu alinipa busara kuamua kipi kilichokuwa bora. Nina furaha kubwa kuwepo hapa na sasa nafikiria kuhusu kushinda mataji zaidi na Santos,” aliongeza.
“Pesa haziwezi kununua furaha yako na nina furaha kuwepo hapa,” alisema mwanasoka huyo, anayeshabihishwa kiuchezaji na mwanasoka nyota wa zamani wa nchi hiyo, Pele.
Santos imeamua kumuongezea mkataba Neymar ili awemo kwenye kikosi hicho hadi baada ya fainali za Kombe la Dunia za mwaka 2014 zinazotarajiwa kufanyika nchini Brazil.
Hata hivyo, wawakilishi wa mwanasoka huyo wameitaka Chelsea kutokukata tamaa kabisa na kuwasilisha maombi mengine ya kumsajili msimu ujao baada ya Santos kumaliza michuano ya Kombe la Libertadores, ambalo haijawahi kulitwaa tangu mwaka 1963.
Baba wa mwanasoka huyo alisema: “Sisi pamoja na rais, tumeamua kuahirisha safari ya kwenda Ulaya ili kumruhusu akue na kuendelea zaidi kisoka hapa.”
Uongozi wa Santos ulimwahidi mchezaji huyo na washauri wake kwamba, si tu utamuongezea mshahara, bali pia utamwajiri ofisa uhusiano kwa ajili ya kumuongezea uelewa wake juu ya mambo mbalimbali, hasa yanayohusu masoko katika nchi za Uingereza, Hispania na Italia.
Klabu hiyo ina ndoto za kumfanya Neymar awe mchezaji wa kwanza katika kizazi cha sasa kutambulika kama mwanasoka bora wa dunia wakati akiendelea kucheza soka nchini Brazil.
Santos pia imeahidi kufanya hivyo kwa mchezaji Paulo Henrique Ganso (20), ambaye kiu yake kubwa ni kujiunga na klabu za Manchester United, Real Madrid na Lyon.
Uamuzi wa Santos kumuongezea mkataba Neymar ni pigo kubwa kwa Chelsea, ambayo imekuwa ikimuwinda kinda huyo kwa miaka miwili iliyopita huku ikijipa matumaini ya kumnyakua baada ya kukutana na baba yake mjini New York mapema mwezi huu.
Kwa sasa, inasubiriwa kuona iwapo Santos itaendelea na tishio lake la kuishtaki Chelsea kwa Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA) kwa kitendo chake cha kumsumbua mchezaji huyo, japokuwa klabu hiyo ya England inaamini haijavunja sheria.
Neymar alizaliwa Februari 5, 1992 mjini Mogi das Cruzes nchini Brazil. Alijiunga na Santos Machi 7, 2009 na kuichezea kwa mara ya kwanza akiwa na umri wa miaka 17, ilipoibwaga Oeste mabao 2-1.
Aliichezea timu hiyo kwa mara ya pili wiki iliyofuata na kuifungia bao lake la kwanza katika mechi dhidi ya Mogi Mirim. Ni mchezaji anayefikiwa kuwa wa aina yake kutokea katika bara la Amerika ya Kusini.
Pele na mwanasoka mwingine nyota wa zamani wa nchi hiyo, Romario walimshinikiza Kocha Dunga amjumuishe kwenye kikosi cha Brazil kilichocheza fainali za mwaka huu za Kombe la Dunia zilizofanyika Afrika Kusini, lakini kocha huyo aligoma.
Hata hivyo, baada ya fainali hizo kumalizika, kocha mpya wa timu hiyo, Menezes aliamua kumjumuisha kwenye kikosi chake kilichocheza mechi ya kirafiki dhidi ya Marekani na kuibuka na ushindi, akiwa amevaa jezi namba 11. Alifunga bao moja kati ya mawili, alipounganisha kwa kichwa krosi ya Andre Santos. Brazil ilishinda mabao 2-0.

MARIAM CHOKORAA: Mwimbaji na mcheza shoo wa bendi ya Manchester

WACHEZA shoo wa bendi ya Manchester United wakiwa katika picha ya pamoja
MARIAM Chokoraa

KWA mashabiki wa muziki wa dansi waliowahi kuhudhuria maonyesho ya bendi ya Manchester yenye maskani yake Mbagala, Dar es Salaam, jina la Mariam Hassan si geni kwao. Ni mmoja wa waimbaji na wacheza shoo wanaoing’arisha bendi hiyo kutokana na uwajibikaji wake jukwaani.
Sauti yake ni maridhawa na yenye mvuto wa aina yake. Huimba kwa hisia na madoido ya aina yake. Lakini huvutia zaidi pale anapojumuika na wacheza shoo wa bendi hiyo kulishambulia jukwaa.
Licha ya kuwa na mwili uliojaa, ana uwezo wa kuuchezesha anavyotaka, akifuatisha mipigo ya ala na hivyo kuwafanya mashabiki watamani kumkodolea macho hadi mwisho wa onyesho.
Huyo ndiye Mariam, mwimbaji na mcheza shoo aliye maarufu zaidi kwa jina la Mariam Chokoraa, kufuatia kuolewa na mwimbaji nyota wa bendi ya Twanga Pepeta International, Khalid Chokoraa kabla ya kutengana.
Mariam (27) alifunga ndoa na Chokoraa mwaka 1999 na kuzaa naye mtoto mmoja wa kiume. Alikutana na Chokoraa walipokuwa mjini Tanga kwa shughuli za muziki kabla ya kuhamia naye katika bendi ya Extra Bongo mwaka 2003.
Mwanamuziki huyo hapendi kuzungumzia sana ndoa yake na Chokoraa na sababu za kuvunjika kwake. Kwake hiyo imebaki kuwa historia. Ni mambo ya zamani, hapendi na hataki kuyakumbuka.
Akizungumza na BURUDANI wiki iliyopita mjini Dar es Salaam, Mariam alisema alianza kujihusisha na muziki kwa kucheza shoo katika promosheni za vinywaji mbalimbali mjini Tanga.
Alisema ni katika promosheni hizo, aliweza kukutana na Chokoraa na hatimaye wakaangukia katika dimbwi la mapenzi kabla ya kufunga ndoa na kuwa mume na mke.
Je, Mariam ndiye aliyeimbwa na Chokoraa katika kibao chake cha ‘Kuachwa’, alichokirekodi kwa kushirikiana na Charles Baba, Kalala Junior na Jose Mara?
Mariam hapendi kulizungumzia jambo hilo. Pia hayuko tayari kukubali ama kukataa ukweli juu ya kibao hicho.
“Nisingependa kuzungumzia jambo hilo, kama unaweza ni bora umuulize Chokoraa mwenyewe,”alisema mwanadada huyo.
Akiwa Extra Bongo, Mariam alikuwa akishiriki kucheza shoo kwenye maonyesho mbalimbali ya bendi hiyo kabla ya kuvunjika. Akaamua kubisha hodi Bicco Stars, ambako nako hakudumu muda mrefu kutokana na bendi hiyo kusambaratika.
Baada ya kuvunjika kwa Bicco Stars, mwanamama huyo aliamua kupumzika kwa muda shughuli za muziki huku akitafakari nini cha kufanya. Wakati huo, tayari Mariam alishakuwa ameachana na mumewe Chokoraa.
“Nilisimama shughuli za muziki kwa muda mrefu kabla ya kujiunga na SOT Band ya Tanga na baadaye Manchester Band, ambako ndiko niliko hadi sasa,”alisema Mariam.
Alisema ujio wake ndani ya bendi ya Manchester ulikuwa na neema kubwa kwa vile baada ya miezi michache tangu alipojiunga nayo, alikabidhiwa wadhifa wa kuwa kiongozi mkuu baada ya kiongozi wa zamani, kutimuliwa kwa makosa ya utovu wa nidhamu.
“Japokuwa nipo na bendi hii kwa miezi michache, naamini ina uwezo wa kufika mbali kwa sababu viongozi wake ni waelewa, wapo imara na wanawathamini sana wanamuziki wao,”alisema.
Mariam alisema uchanga wao katika fani, kujituma na ari ya kupata mafanikio ni miongoni mwa mambo yanayowafanya wafanyekazi zao kwa umakini mkubwa ili waweze kupata mafanikio zao. Kwa sasa, bendi hiyo inajiandaa kuipua albamu yao ya kwanza, itakayokwenda kwa jina la ‘Urithi wa baba’. Albamu hiyo itakuwa na vibao sita na Mariam ameshiriki kuimba baadhi ya nyimbo.
Licha ya uchanga wake katika fani ya muziki, Mariam alisema havutiwi na tabia ya wanamuziki kuhamahama kutoka bendi moja hadi nyingine kwa kile alichadai kuwa, kunachangia kuua vipaji vyao.
Alisema ni kweli kwamba kuhama kwa wanamuziki kunalenga kutafuta maslahi mazuri zaidi, lakini alisisitiza ni vyema wadumu na bendi zao kwa muda mrefu.
“Sina hakika sana kama wanamuziki wengi wanaohama huwa wakitafuta maslahi kwa sababu wengine hurudi tena kulekule walikotoka. Sasa kama uliondoka katika bendi kwenda kutafuta maslahi, kwa nini unarudi tena kulekule?”Alihoji.
Aliwataka wanamuziki nchini waepuke tamaa kwa madai kuwa, ndiyo inayosababisha wahame kutoka bendi moja hadi nyingine. Alisema binafsi amekuwa akihamahama kutokana na bendi alizopitia kutoweka.
Ametoa mwito pia kwa wanamuziki nchini kuacha majungu na kuchukiana bila sababu. Alisema tabia za aina hiyo zimekuwa zikichangia bendi nyingi kusambaratika.
Mariam anavutiwa sana na uimbaji wa mwanamuziki Luiza Mbutu wa Twanga Pepeta International. Alisema anapenda siku moja afikie uwezo wa mwimbaji huyo mkongwe kwa wanawake hapa nchini.
Kiongozi huyo wa bendi ya Manchester alizaliwa miaka 27 iliyopita katika familia ya watoto wanne ya Mzee Hassan na Mama Mary. Katika familia yao, hakuna mtoto mwingine anayejihusisha na fani ya muziki. Alisoma shule ya msingi ya Girole ya Korogwe mkoani Tanga na kuishia darasa la saba. Hakuweza kuendelea na masomo ya sekondari kutokana na familia yake kutokuwa na uwezo wa kumuendeleza kielimu.

Thursday, August 19, 2010

SIMBA PWAAAAAA!

RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Leodegar Tenga (kulia) akikabidhi Ngao ya Hisani kwa nahodha wa Yanga, Fred Mbuna mara baada ya timu hiyo kuishinda Simba kwa penalti 3-1 katika mechi iliyochezwa jana kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. (Picha na Bashir Nkoromo).

SHABIKI maarufu wa Yanga kwa jina la Shabani Ramadhani 'Mpogoro' akikimbia uwanjani kwa furaha mara baada ya timu hiyo kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Simba katika mechi ya kuwania Ngao ya Hisani iliyochezwa jana kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. (Picha na Bashir Nkoromo).


KOCHA Mkuu wa Simba, Patrick Phiri (kushoto) akitoa maelekezo kwa wachezaji wake, Emmanuel Okwi na Mohamed Banka wakati wa pambano hilo. (Picha zote na Emmanuel Ndege).


KIPA wa Simba, Ally Mustapha 'Barthez' akipatiwa huduma na daktari wa timu hiyo baada ya kugongana na mchezaji Kenneth Asamoah wa Yanga wakati wa pambano hilo huku wachezaji wenzake wakipeana ushauri.

BEKI Juma Jabu wa Simba (kushoto) akimkwatua mshambuliaji Nsa Job wa Yanga wakati wa pambano hilo.


KOCHA Kostadin Papic wa Yanga akifuatilia pambano hilo kwa makini


KIKOSI cha Yanga kilichomenyana na Simba jana



KIKOSI cha Simba kilichomenyana na Yanga jana.

MABINGWA wa soka wa Tanzania Bara, Simba jana walianza vibaya msimu mpya wa ligi kuu ya Vodacom baada ya kuchapwa mabao 3-1 na Yanga katika mechi ya kuwania Ngao ya Hisani iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mshindi wa pambano hilo ilibidi apatikane kwa njia ya penalti tano tano baada ya timu hizo mbili kongwe nchini kumaliza dakika 90 zikiwa suluhu.
Dalili za Simba kufungwa zilianza kuonekana mapema baada ya kupoteza penalti tatu mfululizo zilizopigwa na Emmanuel Okwi, Uhuru Selemani na Amri Kiemba wakati Yanga ilipoteza penalti moja iliyopigwa na Ernest Boakye.
Penalti zilizoiwezesha Yanga kutoka uwanjani kifua mbele, zilifungwa na Geofrey Bonny, Stephano Mwasika na Isaack Boakye. Penalti pekee ya Simba ilifungwa na kiungo wake, Mohamed Banka.
Hii ni mara ya pili kwa Yanga kuishinda Simba katika mechi ya kuwania Ngao ya Hisani. Mara ya kwanza ilikuwa mwaka 2001 wakati Yanga ilipoichapa Simba mabao 2-1.
Ushindi huo pia ulikuwa wa kulipiza kisasi kwa Yanga kufuatia kuchapwa mabao 4-3 na Simba katika mechi ya mwisho ya ligi kuu iliyochezwa kwenye uwanja huo Aprili 18 mwaka huu.
Mwaka jana, Yanga ilishindwa kutamba katika mechi nyingine ya kuwania ngao hiyo baada ya kuchapwa idadi hiyo ya mabao na Mtibwa Sugar ya Morogoro.
Kwa kawaida, mechi ya kuwania Ngao ya Hisani huchezwa kila mwaka kabla ya kuanza kwa ligi hiyo, inayotarajiwa kuzishirikisha timu 12 msimu huu. Ligi hiyo inatarajiwa kuanza keshokutwa.
Timu hizo zililianza pambano hilo kwa tahadhari kubwa huku kila upande ukiusoma mwingine. Katika dakika hizo za mwanzo, kila timu ilifanya mashambulizi ya kushtukiza na kuwa makini katika kuokoa mipira ya hatari.
Yanga nusura ipate bao dakika ya tatu wakati Athumani Iddi ‘Chuji’ kupokea pande safi kutoka kwa Nsa Job, lakini shuti lake liliokolewa na kipa Ally Mustapha.
Simba ilijibu mapigo dakika ya 39 wakati Emmanuel Okwi alipowatoka mabeki wawili wa Yanga na kufumua shuti kali lililotoka sentimita chache nje ya lango.
Dakika mbili baadaye, Nsa alipata nafasi nzuri ya kuifungia bao Yanga baada ya kuwazidi mbio mabeki Juma Jabu na Juma Nyoso wa Simba, lakini shuti lake lilitoka nje ya lango. Timu hizo zilikwenda mapumziko zikiwa suluhu.
Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote mbili kufanya mabadiliko ya wachezaji. Yanga iliwapumzisha Kenneth Asamoah na Chuji, ambao nafasi zao zilichukuliwa na Jerry Tegete na Geofrey Bonny. Simba iliwaingiza Amri Kiembe na Shija Mkina kuchukua nafasi za Jerry Santo na Nico Nyagawa.
Katika kipindi hicho, kasi ya mchezo iliongezeka kwa kila timu huku zikishambuliana kwa zamu, lakini umaliziaji mbovu ulikuwa kikwazo kwa timu zote mbili kupata mabao.
Abdi Kassim ‘Babi’ angeweza kuifungia Yanga bao dakika ya 54 alipofumua shuti kali akiwa nje kidogo ya eneo la hatari la Simba, lakini lilimbabatiza beki Nyoso na kuwa kona, ambayo haikuzaa matunda.
Dakika moja baadaye, beki Jabu wa Simba alipanda mbele kusaidia mashambulizi na kutoa pande safi kwa Okwi, lakini wakati akijiandaa kufunga, kipa Yaw Berko wa Yanga alitokea na kuudaka mpira miguuni kwake.
Kipa Mustapha wa Simba alidhihirisha kuwa ni moto wa kuotea mbali dakika ya 71 baada ya kupangua shuti kali la Nsa kabla ya beki Joseph Owino kutokea na kuondosha mpira kwenye eneo la hatari.
Simba itaijutia nafasi aliyopata Uhuru dakika ya 82 alipopewa pasi akiwa ndani ya 18, lakini shuti lake lilidakwa na kipa Berko wa Yanga. Okwi naye alipoteza nafasi mbili nzuri za kufunga dakika ya 83 na 88 baada ya mashuti yake kutoka nje ya lango.
Katika pambano hilo lililochezeshwa na mwamuzi Ramadhani Kibo Ibada kutoka Zanzibar, wachezaji sita walionyeshwa kadi za njano kwa makosa ya kucheza rafu mbaya. Wachezaji hao ni Nadir, Isaack na Ernest Boakye wa Yanga na Santo na Mussa wa Simba.
Akizungumza baada ya pambano hilo, Kocha Mkuu wa Yanga, Kostadin Papic alisema anashukuru timu yake kupata ushindi na kwamba sasa anaelekeza akili yake katika michuano ya ligi kuu.
Papic alisema amefurahishwa na kiwango kilichoonyeshwa na timu yake na kwamba pambano lilikuwa gumu. Alisema atarekebisha dosari zilizojitokeza kwa wachezaji wake kabla ya kuanza ligi keshokutwa.
Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Phiri alisema wamekubali kushindwa na kuongeza kuwa, kipigo hicho kilikuwa cha bahati mbaya kwa timu yake, iliyotawala sehemu kubwa ya pambano hilo.
SIMBA: Ally Mustapha, Haruna Shamte, Juma Jabu, Juma Nyoso, Joseph Owino, Jerry Santo/Amri Kiemba, Nico Nyagawa/Shija Mkina, Mohamed Banka, Mussa Hassan/ Patrick Ochan, Emmanuel Okwi, Uhuru Selemani.
YANGA: Yaw Berko, Shadrack Nsajigwa/ Fred Mbuna, Stephano Mwasika, Nadir Haroub, Isaack Boakye, Ernest Boakye, Nurdin Bakari, Athumani Iddi/Geofrey Bonny, Kenneth Asamoah/ Jerry Tegete, Nsa Job, Abdi Kassim/Yahya Tumbo.




Makocha wazawa, wageni nani zaidi?





WAKATI michuano ya soka ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara inatarajiwa kuanza mwishoni mwa wiki hii, vita kali inatarajiwa kuibuka kati ya makocha wazawa na wale wa kigeni.
Kuibuka kwa vita hiyo kunatokana na makocha takriban wa timu zote 12 zitakazoshiriki ligi hiyo, kila mmoja kujigamba kwamba timu yake itafanya vizuri na kuibuka na ubingwa.
Tambo za makocha hao zimekuja, kufuatia usajili uliofanywa na kila timu pamoja na maandalizi yaliyofanywa na makocha wanaozifundisha, ambapo makocha wazawa wamepania kukata ngebe za wageni.
PATRICK PHIRI-SIMBANi kocha aliyeiwezesha Simba kupata mafanikio makubwa msimu uliopita, baada ya kutwaa ubingwa kabla ya ligi kumalizika na pia bila kufungwa mechi hata moja.
Phiri pia amekuwa gumzo kubwa kwa mashabiki wa soka nchini kutokana na staili yake ya ufundishaji na pia uwezo wake wa kubadili mchezo uwanjani kadri mchezo unavyoendelea.
Kama ilivyo kawaida yake, kocha huyo raia wa Zambia aliwapa wasiwasi mkubwa viongozi na mashabiki wa Simba baada ya kuchelewa kurejea nchini kutoka mapumziko kwa kisingizio cha matatizo ya kifamilia.
Katika msimu huu, Phiri ataongezewa nguvu na makocha watatu, akiwemo Syllersaid Mziray, Selemani Matola na Amri Said, ambaye alikuwa msaidizi wake msimu uliopita. Pia yupo kocha mpya wa makipa, Haroun Amour kutoka Oman.
Kikosi cha Simba msimu huu kinajivunia wachezaji wake wapya, Amir Maftah, Abdulrahim Humud, Shija Mkina, Rashid Gumbo, Gilla Joshua, Patrick Ochan, Kelvin Chale na Mbwana Samatta.
Katika kikosi hicho, wamo wachezaji watano wa kigeni walioichezea msimu uliopita. Wachezaji hao ni Joseph Owino, Hillary Echesa, Jerry Santo na Emmanuel Okwi.
Wachezaji wengine wa Simba wanaotarajiwa kuonekana katika ligi hiyo msimu huu ni Juma Kaseja, Ali Mustapha, Ramadhan Shamte, Salum Kanoni,Amir Maftah,Kelvin Yondan, Juma Nyoso,David Naftali na Mohamed Banka.
Wengine ni Nico Nyagawa,Uhuru Seleman, Amri Kiemba, Mussa Hassan 'Mgosi',Mohamed Kijuso,Kelvin Chale na Juma Jabu.
Akizungumzia ligi hiyo, Phiri alisema lengo lake ni kuendeleza rekodi ya msimu uliopita ya kushinda mechi zote na kutwaa ubingwa kabla ya ligi kumalizika.
Phiri alisema licha ya kuchelewa kuripoti kambini, hana wasiwasi na kikosi chake kwa vile hakina mabadiliko makubwa na kina uwezo mkubwa wa kutetea taji lake.
KOSTADIN PAPIC-YangaNi kocha aliyeanza kuinoa Yanga msimu uliopita, akichukua nafasi ya Dusan Kondic, aliyefungasha virago baada ya mzunguko wa kwanza kumalizika.
Papic amelieleza gazeti la Burudani kuwa, ana hakika kikosi chake kilichosheheni nyota watatu kutoka Ghana, kina uwezo mkubwa wa kulirejesha taji la ligi hiyo kutoka kwa mahasimu wao Simba.
Kocha huyo kutoka Serbia alisema, ameshazifanyiakazi dosari zote zilizojitokeza kwenye kikosi chake msimu uliopita, hivyo hawatarajii kurudia makosa.
Katika kikosi cha Yanga msimu huu, wamo wachezaji watatu wapya kutoka Ghana, Isaac Boakye, Ernest Boakye na Kenneth Asamoah, ambaye ndiye tegemeo kubwa kwa ufungaji wa magoli. Pia yumo kipa Ivan Knezevic kutoka Serbia.
Wachezaji wengine wapya waliosajiliwa na Yanga msimu huu ni Salum Telela, Stephen Mwasita, Abuu Ubwa Zuberi, Chacha Marwa, Nsa Job, Yahya Tumbo na Sunday Seme.
Mbali na sura hizo mpya, kikosi hicho pia kitakuwa na wachezaji walioichezea msimu uliopita. Wachezaji hao ni Yaw Berko kutoka Ghana, Nelson Kimathi,Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Mohamed Mbegu, Nurdin Bakari, Geofrey Bonny, Kigi Makasi, Abdi Kassim, Shamte Ally, Jerry Tegete, Iddi Mbaga, Razack Khalfan na Fred Mbuna.
ITAMAR AMORIM-AZAM
Kocha huyo kutoka Brazil ameendelea kukiimarisha kikosi chake kwa kusajili wachezaji nyota kadhaa wapya na hivyo kukifanya kiwe tishio na pia kutabiriwa kutwaa ubingwa.
Miongoni mwa nyota hao wapya ni pamoja na mshambuliaji Mrisho Ngasa kutoka Yanga, kiungo Ramadhani Chombo ‘Redondo’ na mshambuliaji Jabir Azizi kutoka Simba. Itamar alisema wiki hii kuwa, wamefanya maandalizi mazuri kwa ajili ya ligi hiyo, ikiwa ni pamoja na kucheza mechi kadhaa za kirafiki kwa lengo la kupima uwezo wa wachezaji wake.
Alisema mechi hizo zimemwezesha kupata kikosi cha kwanza, ambacho ana hakika kina uwezo mkubwa wa kuweka rekodi ya kutwaa ubingwa wa ligi hiyo msimu huu.
Kocha huyo wa zamani wa viungo wa timu ya taifa, Taifa Stars alisema, kikosi chake kimeimarika zaidi msimu huu kuliko msimu uliopita na ametoa onyo kwa vigogo Simba na Yanga kujiandaa kupata upinzani mkali.
Wachezaji waliosajiliwa na Azam kwa ajili ya msimu huu wa ligi ni pamoja Aggrey Morris, Ally Manzi, Daudi Mwasongwe, Erasto Nyoni,Faraj Hussein, Ibrahim Mwaipopo, Ibrahim Shikanda, Jackson Chove na Jamal Mnyate.
Wengine ni John Bocco,Kally Ongala, Luckson Kakolaki, Malika Mdeule, Mau Ally, Mohammed Binslum, Patrick Mafisango, Salum Swedi, Sami Haji ,Tumba Swedi na kipa Vladmir Niyonkuru kutoka Burundi.
Licha ya hayo,kocha huyo ameeleza kuwa ana imani kubwa kikosi chake kitakuwa moto wa kuotea mbali kutokana na kuongeza nguvu katika sehemu zote ambazo msimu uliopita zilikuwa na matatizo na kuwaomba waamuzi kuchezesha kwa haki.
FRED FELIX MINZIRO-JKT RUVUKocha Fred Felix Minziro ametamba kuwa, kikosi chake kimefanya maandalizi kabambe kwa ajili ya ligi hiyo na kina uwezo wa kuwa kiboko ya vigogo vya soka nchini, Simba na Yanga.
Minziro amesema cheche za timu hiyo zimeshaanza kuonekana katika mechi kadhaa za kirafiki walizocheza, ambapo alitamba wachezaji wake walionyesha uwezo wa juu.
JKT Ruvu inaundwa na wachezaji wengi chipukizi, ambao baadhi yao ni waajiriwa wa Jeshi la Kujenga Taifa na wengine ni raia wa kawaida.
Minziro amesajili kikosi cha timu hiyo kupitia usaili alioufanya kwa wachezaji waliojitokeza kwenye mazoezi yaliyofanyika kwenye uwanja wa jeshi uliopo Mlandizi mkoani Pwani.
“Kikosi changu kimesheheni wachezaji wengi wenye umri mdogo, lakini kitakuwa moto wa kuotea mbali kwenye ligi. Nawatahadharisha wapinzani wetu, hasa Simba na Yanga wajiandae kupata vipigo,”alitamba.
Minziro alisema lengo lake ni kuwaonyesha makocha wa kigeni kwamba, hata makocha wazawa nao wana uwezo wa kuonyesha maajabu katika ligi hiyo. TOM OLABA- MTIBWANi kocha aliyekabidhiwa jukumu la kuinoa Mtibwa Sugar baada ya Salum Mayanga kupangiwa majukumu mengine kwenye kiwanda cha Sukari cha Mtibwa kilichopo Turiani mjini Morogoro.
Olaba, ambaye ni raia wa Kenya, aliwahi kuifundisha Mtibwa mwanzoni mwa miaka ya 2000 kabla ya kuondoka na kwenda Zanzibar, ambako alikuwa kocha mkuu wa Miembeni.
Mratibu wa Mtibwa, Jamal Bayser amesema wameamua kumrejesha kocha huyo kwa lengo la kuiongezea nguvu zaidi timu hiyo. Alisema licha ya kuchelewa kuanza kazi, ana hakika Olaba ana uwezo wa kuifikisha mbali timu hiyo.
Olaba atakuwa akisaidiwa na mchezaji wa zamani wa timu hiyo, Mecky Maxime, ambaye kwa sasa ndiye aliyeachiwa jukumu la kuinoa Mtibwa baada ya Mayanja kurejea kiwandani.
Tumaini kubwa la Mtibwa katika ligi hiyo msimu huu litakuwa kwa washambuliaji wake wapya, Thomas Maurice, Yona Ndabila, Boban Zilintusa.
Makocha Jackson Mayanja wa Kagera Sugar, Peter Mhina wa Majimaji, John Simkoko wa Polisi Dodoma, Choki Abeid wa Toto African, Dan Koroso wa AFC na Charles Kilinda wa JKT Ruvu nao kila mmoja amejigamba kuwa timu yake itafanya vizuri msimu huu.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti, makocha hao walisema, wamefanya maandalizi ya kutosha na kilichobaki ni ligi hiyo kuanza kutimua vumbi.
Makocha hao walisema hakuna anayependa kuiona timu yake iishuka daraja, hivyo watapigana kufa na kupona ili kuhakikisha wanabaki kwenye ligi hiyo msimu ujao.
Wametoa tahadhari kwa waamuzi waliopangwa kuchezesha ligi hiyo, kuepuka kuzipendelea timu kubwa, badala yake waheshimu na kuzingatia sheria zote 17 za soka ili washindi wapatikane kutokana na uwezo wao.
000000
RATIBA YA MECHI ZA UFUNGUZI LIGI KUU TANZANIA BARA
TAREHE MECHI UWANJA MKOA
Agosti 21, 2010 Lyon vs Simba Uhuru Dar
Polisi Dom vs Yanga Jamhuri Dodoma AFC vs Azam S. Abeid Arusha Majimaji vs Mtibwa Majimaji Ruvuma Toto vs Ruvu S CCM Kirumba Mwanza Kagera vs JKT Ruvu Kaitaba Kagera


Wednesday, August 18, 2010

Lyon yaigeuka Simba

KLABU ya African Lyon imesema itawazuia wachezaji wake, Mbwana Samatta na Rashid Gumbo kuichezea Simba msimu huu kwa vile klabu hiyo haijakamilisha taratibu za kuwahamisha.
Mmoja wa viongozi wa Lyon, ambaye hakupenda jina lake litajwe gazetini alisema jana kuwa, hawatambui iwapo wachezaji hao wamesajiliwa na Simba.
Kiongozi huyo alisema, wanachotambua ni kwamba Gumbo na Samatta bado ni wachezaji halali wa Lyon hadi hapo Simba itakapofuata taratibu katika kuwasajili.
Aliongeza kuwa, uongozi wa Simba umetangaza kuwasajili wachezaji hao kinyemela bila kufuata taratibu za uhamisho zilizowekwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Kwa mujibu wa kiongozi huyo, Gumbo na Samatta kila mmoja ana mkataba wa kuichezea Lyon kwa miaka mitatu na mikataba yao imesajiliwa na inatambuliwa na TFF.
“Tutawazuia wachezaji hao kuichezea Simba katika michuano ya ligi kuu, inayotarajiwa kuanza Jumamosihadi taratibu za usajili zitakapofuatwa,”alisema.
Simba na Lyon zimepangwa kukata utepe wa michuano ya ligi hiyo msimu huu katika mechi itakayochezwa Jumamosi kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Alipoulizwa jana kuhusu suala hilo, Makamu Mwenyekiti wa Simba,Godfrey Nyange ‘Kaburu’ alisema waliwasajili wachezaji hao kwa kufuata taratibu zote ndio sababu wameidhinishwa na TFF.
Kaburu alisema madai hayo yaliyotolewa na Lyon hayana msingi na kuongeza kuwa, yamelenga kuuchafua uongozi wa Simba.
Naye Ofisa Habari wa TFF, Florian Kaijage alisema masuala yote yanayohusu ligi na usajili wa wachezaji, yatatolewa ufafanuzi leo wakati wa kikao cha kamati ya utendaji ya shirikisho hilo.
Kaijage alisema kikao hicho pia kitajadili ajira ya katibu mkuu wa shirikisho hilo ili kujaza nafasi ya Fredrick Mwakalebela, aliyemaliza mkataba wake.

Maproo wa Yanga hatarini kuikosa ligi

SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), huenda likawazuia wachezaji wapya watano wa kigeni kuichezea Yanga katika msimu huu wa ligi kuu ya Tanzania Bara.
TFF itafikia uamuzi huo iwapo Yanga itashindwa kuwalipa haki zao wachezaji wake wanne iliowaacha kwenye usajili wa msimu huu kabla ya mikataba yao kumalizika.
Wachezaji wa kigeni wa Yanga waliopo hatarini kuzuiwa kucheza ligi hiyo, inayotarajiwa kuanza keshokutwa ni Yaw Berko, Isaack Boakye, Kenneth Asamoah, Ernest Boakye na Ivan Knezevic.
Habari kutoka ndani ya TFF zimeeleza kuwa, shirikisho hilo limepanga kuwakutanisha wachezaji walioachwa kwenye usajili na uongozi wa Yanga ili kufikia muafaka wa malipo yao.
Kwa mujibu wa habari hizo, kikao hicho kimepangwa kufanyika leo kwenye ofisi za shirikisho hilo, ambapo TFF itawakilishwa na Kaimu Katibu Mkuu, Sunday Kayuni na baadhi ya wanasheria wake.
Wachezaji walioachwa na Yanga kabla ya mikataba yao kumalizika ni Wisdom Ndlovu, John Njoroge, Ali Msigwa na Steven Marashi.
Ndlovu na wenzake waliwasilisha malalamiko TFF wakipinga kuachwa dakika za mwisho huku mikataba yao na Yanga ikiwa haijamalizika.
“TFF imeitaka Yanga kumalizana na wachezaji hao kabla ya ligi kuanza Jumamosi, vinginevyo wachezaji wake wapya watano wa kigeni watazuiwa kucheza ligi,”kimesema chanzo cha habari.
Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako alithibitisha jana kuhusu kuwepo kwa kikao hicho na kuongeza kuwa, anaamini suala la wachezaji hao litamalizwa siku chache zijazo.

FERGUSON: Nilimsajili Bebe bila kumuona


LONDON, England
KOCHA Mkuu wa Manchester United, Sir Alex Ferguson amefichua kuwa, Bebe ni mchezaji wa kwanza kwake kumsajili bila hata kumuona akicheza kwenye televisheni.
Ferguson alimsajili Bebe (20) wiki iliyopita kutoka klabu ya Vitoria de Guimaraes ya Ureno. Usajili wake uliigharimu Manchester United pauni milioni 7.4 za Uingereza.
Usajili wa Bebe umewashtua mashabiki wengi wa soka wa England, hasa ikizingatiwa kuwa, alidumu na klabu ya Vitoria kwa wiki tano.
Kabla ya kujiunga na Vitoria, mshambuliaji huyo chipukizi alikuwa akiichezea klabu ya daraja la tatu ya Estrela da Amadora.
Ferguson hakuwahi kupata nafasi ya kumuona Bebe akicheza kupitia DVD, lakini alimtuma Mtendaji Mkuu wa Manchester United, David Gill kwenda Ureno kukamilisha usajili wa mchezaji huyo.
“Sikuwahi kumuona kwenye video, ni mara ya kwanza. Kwa kawaida, kama ilivyokuwa kwa Javie (Hernandez) na Chris (Smalling), niliona video zao kadhaa kabla ya kuwasajili,”alisema kocha huyo mwenye umri wa miaka 68.
“Baadhi ya wakati unapaswa kuwaamini wafanyakazi wako na wafuatiliaji wetu wa vipaji nchini Ureno walitushauri tufanye haraka kumsajili,”aliongeza. “Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa klabu zingine na ni hapo unapaswa kufanya maamuzi ya haraka katika maisha yako na sijisikii vibaya kuhusu hilo. Pia nilizungumza na Carlos Queiroz (msaidizi wake wa zamani) kuhusu Bebe,” alisema Ferguson.
Naye Bebe alisema ana hakika atamvutia kocha huyo kwa sababu ana uwezo mkubwa uwanjani ikiwa ni pamoja na kuwa na kasi, kupiga mashuti na kufunga mabao.
Mbali na Manchester United, Bebe pia alikuwa akiwaniwa na klabu za Real Madrid ya Hispania na Benfica ya Ureno kabla ya kuzidiwa kete na Ferguson.
Wakati Manchester United ikimsajili Bebe, mahasimu wao Manchester City walifanikiwa kuwanyakua wachezaji Mario Balotelli kutoka AC Milan ya Italia na James Milner wa Aston Villa.
Ferguson ameuponda usajili wa Manchestet City kwa madai kuwa wamiliki wake wamekuwa wakitumia fedha nyingi kusajili wachezaji kiholela.
Wamiliki wa Manchester United walikaririwa hivi karibuni wakisema kuwa, bado Ferguson analo fungu la kutosha kwa ajili ya usajili wa wachezaji wapya. Usajili wa Bebe umeifanya klabu hiyo hadi sasa iwe imetumia pauni milioni 25 kusajili wachezaji wapya msimu huu.
Ferguson pia alitumia kiasi kidogo cha pesa kusajili wachezaji wapya msimu uliopita baada ya kumuuza Cristiano Ronaldo kwa pauni milioni 80 kwa klabu ya Real Madrid.


Santos yamwekea ngumu Neymar kuhamia Chelsea

KLABU ya Santos ya Brazil imemuomba mshambuliaji wake nyota, Robinho de Souza kumshawishi mchezaji mwenzake, Neymar afute mpango wake wa kujiunga na Chelsea ya England.
Mbali na Robinho, klabu hiyo pia imemuomba mwanasoka nyota wa zamani wa nchi hiyo, Pele na Waziri wa Michezo wa Brazil, Orlando Silva kuingilia kati suala la mchezaji huyo.
Tayari Kocha Mkuu wa sasa wa timu ya taifa ya Brazil, Mano Menezes na kocha wa zamani wa timu hiyo, Mario Zagallo wameshamtahadharisha chipukizi huyo na kumtaka abaki nchini humo. Mchezaji huyo mwenye kipaji ameonekana kuchanganyikiwa kuhusu mustakabali wake, kufuatia vyombo kadhaa vya habari kuripoti kuhusu uhamisho wake.
Akizungumza na vyombo vya habari juzi, kuhusu ushauri aliopewa na Zagallo na Menezes, Neymar alisema hadi sasa haelewi iwapo atabaki nchini humo ama ataondoka.
“Kuna mambo mengi ambayo bado hayajawa wazi. Lakini siwezi kuondoka nikaenda mahali na kusugua benchi. Bila shaka nitautafakari kwa makini ushauri wa Mano na Zagallo. Inawezekana ni mapema mno kuondoka,”alisema.
Maneno yake hayo yameipa matumaini makubwa klabu ya Santos, ambayo viongozi wake wamepanga kukutana na baba wa mchezaji huyo pamoja na wakala wake, Wagner Ribeiro.
Kuna habari kwamba, Santos inataka kumuongezea mkataba Neymar ili aendelee kubaki kwenye klabu hiyo. Mkataba wa sasa wa Neymar unatarajiwa kumalizika mwaka 2014.
Chelsea ilitenga kitita cha pauni milioni 17 kwa ajili ya kumsajili mshambuliaji huyo, lakini Santos ilizitolea nje pesa hizo. Kufuatia kukataliwa kwa ofa hiyo, Chelsea imeongeza dau na kufika pauni milioni 25.
Santos, ambayo imetishia kuishtaki Chelsea kwa Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA), imesisitiza kuwa haiwezi kumuuza mchezaji huyo chini ya pauni milioni 30, ambacho ni kiwango chake cha kuvunja mkataba.
Zagallo alikaririwa wiki hii akisema Neymar hayuko fiti kuweza kukabili mikikimikiki ya ligi kuu ya England, ambako ni wachezaji wachache kutoka Brazil wanaocheza nchini humo.
“Nafikiri ni mapema kwa mchezaji mwenye umri wa miaka 17, 18 au 19 kuondoka Brazil,”alisema Zagallo, ambaye alishinda Kombe la Dunia akiwa na mchezaji wa Brazil mwaka 1958 na 1962 na akiwa kocha mwaka 1970.
“Ni wazi kwamba sikuzote pesa ndicho kishawishi kikubwa kwa wachezaji kutaka kuondoka, lakini kwa suala la Neymar, atakwenda katika mazingira, ambayo si mazuri mwili wake. Anahitajika kuongeza uzito, hivyo ni bora aondoke akiwa na umri wa miaka 21 au 22,”aliongeza.
Menezes, ambaye alimwita Neymar kwa mara ya kwanza katika kikosi cha Brazil, ilipoibwaga Marekani mabao 2-0 wiki iliyopita, aliunga mkono maoni ya Zagallo.

JUMBE: Naiheshimu Sikinde, ndiyo iliyonifundisha ujanja

MWANAMUZIKI wa zamani wa bendi ya muziki wa dansi ya Mlimani Park Orchestra, Hussein Jumbe amesema kamwe hawezi kuidharau na kuidhihaki bendi hiyo kwa sababu ndiyo iliyomfikisha alipo sasa.
Akizungumza mjini Dar es Salaam hivi karibuni, Jumbe alisema alipata umaarufu na ujanja wa kimuziki akiwa Mlimani Park, maarufu kwa jina la Sikinde, hivyo anaiheshimu pamoja na kuwaheshimu wanamuziki wake.
Jumbe alikuwa akijibu swali aliloulizwa na mwandishi wa habari hii kuhusu uamuzi wake wa kufanya maonyesho ya pamoja na bendi hiyo hivi karibuni.
Mwimbaji huyo mwenye sauti maridhawa, ambaye kwa sasa anamiliki bendi yake ya Talent, alishiriki kwenye maonyesho mawili ya Sikinde yaliyofanyika kabla ya kuanza kwa mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhan.
Katika maonyesho hayo, Jumbe alitia fora na kuwa kivutio kwa mashabiki baada ya kupewa nafasi ya kuimba vibao vya ‘Adha ya chumba kimoja’, ‘Nipeni pole’, ‘Kijakazi’, ‘Naomi,’ ‘Mwanangu Isaya,’ ‘Nachechenea’ na ‘Kumbuka fadhila’.
“Sikinde ni nyumbani kwangu, ndiko nilikojifundishia ujanja na ndiyo iliyonifikisha hapa nilipo, ndiyo iliyonilea, hivyo sija ujanja kwa Sikinde,”alisema mwanamuziki huyo, ambaye pia aliwahi kuimbia bendi ya Msondo Ngoma.
“Kuna watu waliotaka kunigombanisha na wanamuziki wenzake kama vile Shabani Dede na Hassan Bitchuka, lakini ukweli ni kwamba sina matatizo nao, nawaheshimu na wao wananiheshimu,” aliongeza.
Jumbe alisema ataendelea kushirikiana na bendi hiyo kila itakapomuihitaji kwa vile bado anaipenda na anaweza kurudi wakati wowote.
Kwa upande wake, Dede alisema Jumbe ni mwanamuziki mwenzao na kwamba hawana matatizo naye kwa sababu Sikinde ni nyumbani kwake.
Dede alisema kamwe Jumbe hakuwahi kutimuliwa katika bendi hiyo kama baadhi ya vyombo vya habari vilivyoripoti hivi karibuni, bali alitoka mwenyewe kwenda kutafuta maisha Msondo Ngoma.
“Ndio maana unaona leo tuko pamoja naye na tutaendelea kuwa naye wakati wa maonyesho ya sikukuu ya Iddi,”alisema.

MWASITI: Sikutegemea kufika hapa nilipo


MSANII nyota wa kike wa muziki wa bongo fleva nchini, Mwasiti Almasi amekiri kuwa, kibao chake cha kwanza cha ‘Nalivua pendo’ndicho kilichompandisha chati na kumpatia umaarufu mkubwa kimuziki.
Akihojiwa katika kipindi cha televisheni cha Mambo Yoyo cha ITV mwishoni mwa wiki iliyopita, Mwasiti alisema kibao hicho kimetungwa na mtayarishaji maarufu wa muziki nchini, aliyemtaja kwa jina la Abuu.
Mwasiti alisema alitunga kibao hicho tangu mwaka 2007, lakini alifanikiwa kukirekodi mwaka jana baada ya mashairi yake kupitiwa na kuandikwa upya na Abuu.
Alisema mtayarishaji huyo wa muziki, ambaye hapendi kujulikana kwa watu wengi, amekuwa akimpatia msaada mkubwa katika kuandika na kuhariri maishairi ya nyimbo zake.
Mwasiti alisema baada ya kibao hicho kuanza kutamba kwenye vituo mbalimbali vya radio na televisheni nchini, hakuamini masikio yake kwa vile hakuwa na matumaini hayo.
“Wanawake wengi walikuwa wakinipigia simu kunipongeza wakisema, ‘afadhali umewaeleza ukweli watu wenye tabia hiyo’,” alisema mwasiti.
Kufuatia kutamba kwa kibao hicho, Mwasiti alisema alianza kupata mialiko mingi ya kutumbuiza kwenye hafla mbalimbali ikiwa ni pamoja na safari ya kimuziki nchini Ethiopia.
Alisema alikwenda katika nchi hiyo akiwa na wasanii Joseph Haule ‘Profesa Jay’ na Richard kutoka kundi la Tanzania House of Talent (THT) kwa ajili ya kushiriki kwenye kongamano la tano la maendeleo ya Afrika lililoandaliwa na Umoja wa Mataifa.
Kabla ya kwenda Ethiopia, Mwasiti alisema yeye na wasanii wenzake hao watatu walitunga na kurekodi kibao kimoja cha ‘Songa mbele’, ambacho walikiimba kwa lugha ya Kiswahili na Kimasai.
Mbali na Abuu, amemtaja mtu mwingine, ambaye amekuwa akimsaidia kupitia mashairi yake, kuyarekebisha na kumpa ushauri kuwa ni mama yake mzazi.
“Wakati niliporekodi kibao cha ‘Nalivua pendo’, mama hakuamini kama mashairi yale ni ya kwangu. Aliniambia haiwezekani Mwasiti, huyu siye wewe,”alisema Mwasiti.
Mwasiti alisema wakati mwingine mama yake amekuwa akimshauri kupunguza makali ya maneno katika mashairi yake kila alipoyaona mazito ama yana mwelekeo usiovutia.
Alivitaja vibao vingine vilivyompandisha chati kuwa ni ‘Niambie’, ‘Yelele Mama’ na ‘Daima milele’, ambavyo alivirekodi akiwa katika kundi la Tanzania House of Talent (THT).
Alimtaja msanii Judith Wambura ‘Lady JayDee’ kuwa ndiye aliyemvutia na kumfanya ajitose katika fani hiyo kabla ya kurekodi naye kibao chake cha pili.
Alisema licha ya JayDee kuwa msanii maarufu na nyota nchini, anapenda kuwasaidia wasanii wanaochipukia na kuwapa misaada ya aina mbalimbali ili wapate mafanikio.
“Namkubali sana JayDee. Amenisaidia sana. Hana maringo na ana moyo wa kupenda kuwasaidia wasanii wengine,”alisema.
Mwasiti hajawahi kupokea tuzo yoyote ya muziki hapa nchini, lakini aliwahi kupata tuzo ya mwanamuziki bora wa kike wa Tanzania iliyotolewa mwaka jana nchini Kenya.
Alisema kushindwa kwake kupata tuzo hapa nchini hakumkatishi tamaa kwa vile anaamini yeye ni mmoja wa wasanii wanaokubalika kwa mashabiki, lakini bado hajapata bahati hiyo.
Alisema wasanii wote waliowahi kushinda tuzo za muziki hapa nchini ni wazuri kutokana na muziki wao, japokuwa washindi wa tuzo hizo hujulikana mapema.
Mbali na kufanya vizuri hapa nchini, Mwasiti amewahi kupanda jukwaani na baadhi ya wanamuziki nyota wa Afrika kama vile Angelique Kidjo wa Benin na Zola wa Afrika Kusini.
Mwasiti alimemshukuru Mungu kutokana na mafanikio aliyoyapata hadi sasa kwa vile wapo wasanii wengi wa muziki huo, ambao bado hawajapata njia ya kutokea hadi sasa.
”Nimepata nafasi ya kufanya mahojiano na kituo Cha televisheni cha Afrika Kusini cha Chanel O na video ya wimbo wangu wa ”Niambie’ imeonekana kukubalika na wengi,” anasema binti huyo.
Tayari Mwasiti amesharekodi vibao vinane kwa ajili ya albamu yake binafsi, itakayojulikana kwa jina la ‘Niambie’. Alisema albamu hiyo inaandaliwa chini ya usimamizi wa kundi la THT.
Amewataka wasanii zaidi wenye vipaji na nia ya kweli ya kuutumia muziki kama mwelekeo halisi wa maisha yao, kujitokeza kwa wingi na kujiunga na kundi la THT kwa sababu si mahala pa kupotezea muda, bali ni kazi mtindo mmoja.

Hellen Dausen kuwania taji la Miss Universe 2010 J'pili


MWAKILISHI wa Tanzania katika shindano la kumsaka ‘Miss Universe 2010’, Hellen Dausen mwishoni mwa wiki hii anatarajiwa kuwa mmoja wa warembo 83 kutoka sehemu mbalimbali duniani watakaowania taji hilo.
Hellen atapanda ulingoni na warembo wengine wanane kutoka Afrika, kuwania taji hilo kwenye shindano litakalofanyika kwenye ukumbi wa Mandalay Bay Events Center uliopo mjini Las Vegas.
Mshindi wa shindano hilo la 59 anatarajiwa kuvikwa taji la mrembo wa mwaka jana, Stefania Fernandez kutoka nchini Venezuela, ambaye alimvua taji Dayana Mendoza mwaka juzi.
Hellen anakuwa Mtanzania wa nne kuwania taji hilo tangu mwaka 2007 wakati mashindano hayo yalipoanzishwa hapa nchini na mwanadada Maria Sarungi.
Mtanzania wa kwanza kushiriki katika fainali hizo alikuwa Flaviana Matata mwaka 2007, ambaye alifanikiwa kuingia katika hatua ya 15 bora.
Alifuatiwa na Amanda Ole Sululu mwaka 2008 kabla ya Illuminata Mize mwaka jana. Washiriki hao wawili wote walitolewa hatua za awali.
Shindano la ‘Miss Universe’ ndilo kongwe kuliko mashindano yote ya urembo duniani. Lilianzishwa mwaka 1952.
Mbali na Hellen, warembo wengine kutoka Afrika wanaotarajiwa kuwania taji hilo ni Jurema Femaz wa Angola, Tirelo Ramasedi wa otswana, Domia Hammed wa Misri na Awurama Simpson wa Ghana.
Waafrika wengine wataopanda jukwaani kuwania taji hilo ni Dalysha Doorga wa Mauritius, Ngozi Odalonu wa Nigeria, Nicole Flint wa Afrika Kusini na Alice Musukwa wa Zambia.
Tayari washiriki wa shindano hilo wameshashindana katika hatua za awali, ambazo zilihusisha mavazi ya ufukweni na kuonyesha vipaji vyao katika michezo mbalimbali.

Monday, August 16, 2010

Pinto mwenyekiti mpya TASWA

CHAMA cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (Taswa), leo kimefanya uchaguzi wa viongozi watakaokaa madarakani kwa miaka mitatu katika uchaguzi uliofanyika ukumbi wa manispaa Kinondoni, Dar es Salaam. Mwenyekiti alichaguliwa Juma Pinto ambaye ni Mkurugenzi wa gazeti la JamboLeo,alipata kura 61 dhidi ya kura 11 za Mhariri wa gazeti la SpotiStarehe, Juma Pinto na kura nane za Mpoki Bukuku wa gazeti la Mwananchi. Mtangazaji wa Redio One, Maulid Kitenge aliibuka Makamu Mwenyekiti baada ya kupata kura 37 dhidi ya kura 31 za mtangazaji wa Clouds FM, Shafii Dauda na kura 11 za mtangazaji wa Star TV aliyekuwa akitetea wadhifa huo, Tom Chilala. Katibu Mkuu alichaguliwa Mhariri wa Michezo wa gazeti la HabariLeo, Amir Mhando aliyepata kura 78 za ndiyo, ambapo kura moja ilimkataa. Kura 79 zilipigwa na hakuwa na mpinzani, wakati Katibu Msaidizi ilienda kwa George John aliyepata kura 41 dhidi ya kura 38 za Nasongelya Kilyinga. Mhazini ilienda kwa Sultani Sikilo aliyepata kura 45 dhidi ya 32 za Dina Ismail, wakati Mhazini Msaidizi ni Mohammed Mkangara aliyepata kura 78 za ndiyo na moja ilimkataa. Wajumbe sita wa Kamati ya Utendaji walioshinda ni Zena Chande, Elius Kambili, Salum Jaba, Grace Hoka, Tulo Chambo na Onesmo Kapinga.

Warembo wa Miss Tanzania waripoti kambini

WASHIRIKI wa shindano la mwaka huu la kumtafuta mrembo wa Tanzania wakiwa kwenye basi tayari kwa kwenda kambini kwenye hoteli ya Girraffe mjini Dar es Salaam.

Thursday, August 12, 2010




(PICHA YA JUU) Mchezaji Eto Mlenzi wa timu ya soka ya taifa ya wanawake, Twiga Stars akiwa na mchezaji wa Seattle Sounders ya Marekani mara baada ya timu hizo kupambana mwishoni mwa wiki iliyopita katika mechi ya kirafiki . Katika mechi hiyo, iliyochezwa mjini Washington, Twiga Stars ilichapwa mabao 4-2.

(PICHA YA CHINI) Kipa wa Twiga Stars, Fatuma Omary akitia saini kitabu cha mmoja wa mashabiki waliohudhuria mechi kati ya timu hiyo na Seattle Sounders.

IVO MAPUNDA: Sina bifu na Kaseja




MMOJA wa makipa wanaotarajiwa kung’ara katika michuano ya soka ya mwaka huu ya ligi kuu ya Vodacom ni Ivo Mapunda wa African Lyon ya Dar es Salaam. Katika makala hii ya ana kwa ana, iliyoandikwa na Mwandishi Wetu, Athanas Kazige, kipa huyo wa zamani wa Yanga na timu ya taifa, Taifa Stars, anaelezea mikakati yake mbalimbali katika ligi hiyo.
SWALI: Kumekuwepo na taarifa kwamba umekuwa na bifu kwa muda mrefu na kipa Juma Kaseja wa Simba hata kufikia kutozungumza naye. Je, kuna ukweli wowote kuhusu jambo hili?
JIBU: Ukweli ni kwamba sina bifu lolote na kipa huyo kwani tuna mahusiano mazuri na mara nyingi huwa tunakuwa pamoja. Nina hakika hao wanaoeneza taarifa hizo wana malengo yao ya kutaka kutugombanisha.
Kuna wakati tulicheza pamoja katika timu ya Taifa Stars na tulishirikiana vizuri bila ya matatizo yoyote. Ninashangazwa sana na watu wanaoeneza uvumi huo. Mbali na hayo, naamini hizo ni siasa za mpira, kila mtu anaweza kuongea chochote kile ambacho anakiona kifanaa, lakini napenda kukuhakikishia kwamba sina ugomvi au bifu na Kaseja.
SWALI: Kocha mpya wa Taifa Stars, Jan Paulsen kutoka Denmark ametua nchini na tayari ameanza kukinoa kikosi cha timu hiyo kwa ajili ya mashindano ya kimataifa. Una maoni gani kuhusu ujio wa kocha huyo?
JIBU: Napenda kueleza bayano kuwa, kocha wa zamani wa Stars, Marcio Maxio alifanya mambo mengi mazuri hapa kiasi cha kuifanya Tanzania iwe gumzo ulimwenguni. Lakini yapo machache mabaya aliyoyafanya kama binadamu, inabidi asamehewe.
Binafsi nina imani kwamba Poulsen anaweza kutufikisha mbali zaidi kisoka kutoka pale alipoishia Maximo. Jambo la msingi ni kumpa ushirikiano kocha huyo ili aweze kutimiza malengo yake.
Ushirikiano huo unaweza kutolewa na wachezaji, viongozi, mashabiki na wadau wote wa soka kwa jumla, wakiwemo viongozi wa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kwa upande wangu, namshukuru sana Maximo kwa kuniita na kunipa nafasi ndani ya kikosi hicho. Niliweza kupata mafanikio makubwa nikiwa Taifa Stars, ikiwa ni pamoja na kusajiliwa na Yanga, St.Georges ya Ethiopia na African Lyon, ninayoendelea kuichezea hadi sasa.
SWALI: Unazungumziaje kuhusu uendeshaji soka nchini, unaofanywa na TFF (Shirikisho la Soka Tanzania)?
JIBU: Napenda kuwapongeza viongozi wote wa TFF kwa kujitahidi kusaka maendeleo ya mchezo huo kwani tayari dira au mwelekeo wetu umeanza kujionyesha. Iwapo wataongeza juhudi zaidi, naamini tunaweza kufika mbali.
Sikatai kwamba zipo kasoro chache za kiuendeshaji kwa baadhi ya viongozi wa shirikisho hilo, lakini ukweli unabaki palepale kwamba wameweza kufanya mambo makubwa kinyume na ilivyokuwa zamani, ambapo kila kukicha tulikuwa tukishuhudia malumbano na mapinduzi ya uongozi ndani ya TFF, hali iliyochangia kudorola kwa maendeleo ya mchezo huo.
Kasoro zilizopo sasa ndani ya TFF ni chache na iwapo zitafanyiwakazi na viongozi wa juu, naamini Tanzania itapiga hatua kubwa kimaendeleo nap engine kutimiza ndoto za kucheza tena fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika.
Jitihada kubwa zinapaswa kuwekezwa katika mashindano ya vijana wa umri mbalimbali kwa sababu huko ndiko kwenye chimbuko la wanasoka wa baadaye wa Taifa Stars na klabu za Tanzania.
SWALI: Michuano ya ligi kuu ya Vodacom imepangwa kuanza Agosti 21 mwaka huu. Nini matarajio yako katika ligi hiyo?
JIBU: Nina hamu kubwa na ligi hiyo ili niweze kuonyesha uwezo wangu wa kucheza soka. Nimetumia muda mwingi kufanya mazoezi ili niwe fiti. Lakini kikubwa ni kwamba lengo langu ni kurudi tena kwenye kikosi cha Taifa Stars. Nataka kumshawishi Kocha Paulsen anirejeshe tena kwenye timu hiyo. Naamini kwa uwezo wa Mola, nitarejea tena kwenye timu hiyo.
SWALI: Kwa nini unakuwa na imani hiyo wakati msimu uliopita ulishindwa kuonyesha uwezo wako na kumshawishi Maximo akurejeshe kwenye timu hiyo?
JIBU: Zipo sababu nyingi zilizochangia mimi kushindwa kuonyesha makali yangu. Baadhi ya sababu hizo ni matatizo yaliyokuwa yakinikabili ya kudai haki zangu katika timu ya St.Georges baada ya kukatishiwa mkataba wangu pamoja na mambo mengine ya kifamilia.
SWALI:Hivi sasa una umri wako ni miaka 26. Nini matarajio yako katika mchezo wa soka, hasa katika msimu ujao wa ligi kuu?
JIBU: Kama nilivyosema awali, mawazo yangu bado yapo katika timu ya Taifa Stars. Nataka niendelee kuitumikia nchi yangu katika michuano ya kimataifa hadi pale nitakapostaafu kabisa kucheza mchezo huu. Imani yangu kubwa ni kwamba bado nina uwezo wa kuichezea Taifa Stars. Sidhani kama umri nilionao sasa ni kigezo cha mimi kuishiwa uwezo ama kushindwa kutimiza malengo yangu.
SWALI:Umejifunza nini kutokana na fainali za mwaka huu za Kombe la Dunia zilizofanyika hivi karibuni nchini Afrika Kusini?
JIBU: Nimejifunza mambo mengi sana, ikiwa ni pamoja na mbinu za kisasa za kudaka mipira. Kupitia fainali hizo, niliweza kuwashuhudia makipa wa nchi mbalimbali wakionyesha ufundi wa hali ya juu katika kulinda milango yao.
SWALI: Usajili wa wachezaji kwa ajili ya msimu huu wa ligi umeshamalizika. Je, kuna timu yoyote kubwa iliyokufuata kwa lengo la kukusajili?
JIBU: Zipo baadhi ya timu za nje ya nchi zilizoonyesha nia ya kutaka kunisajili, lakini mambo hayakuweza kukaa vizuri. Kwa upande wa hapa nchini, hakuna timu yoyote iliyyonyesha nia ya kunisajili.
SWALI: Unajisikiaje kuichezea timu ya African Lyon badala ya Simba au Yanga?
JIBU: Swali lako zuri sana ndugu yangu. Unajua unapokuwa unachezea timu kama Simba au Yanga, unakuwa mtu mwenye wakati mgumu kutokana na viongozi, wanachama na mashabiki kutokuwa na imani na wachezaji wao. Siku zote wanataka timu yao ishinde. Ikifungwa, inakuwa ni balaa kubwa.
Licha ya jambo hilo, timu hizo zina wapenzi wengi. Unakuwa maarufu na kujulikana kila kona, lakini timu inapofanya vibaya na bahati mbaya umechangia kufungwa, hapo utapata tabu sana, wewe pamoja na familia yako.

RATIBA YA LIGI ZA ULAYA

LIGI KUU ENGLAND
Jumamosi, Agosti 14, 2010
Tottenham v Man CityAston
Villa v West Ham
Blackburn v Everton
Bolton v Fulham
Sunderland v Birmingham
Wigan v Blackpool
Wolverhampton v Stoke
Chelsea v West Brom

Jumapili, Agosti 15, 2010
Liverpool v Arsenal

Jumatau, Agosti 16, 2010
Man Utd v Newcastle

Jumamosi, Agosti 21, 2010
Arsenal v Blackpool
Birmingham v Blackburn
Everton v Wolverhampton
Stoke v Tottenham
West Brom v Sunderland
West Ham v Bolton
Wigan v Chelsea

Jumapili, Agosti 22, 2010
Newcastle v Aston Villa
Fulham v Man Utd

Jumatatu, Agosti 23, 2010
Man City v Liverpool

Jumamosi, Agosti 28, 2010
Blackburn v Arsenal
Blackpool v Fulham
Chelsea v Stoke
Tottenham v Wigan
Wolverhampton v Newcastle
Man Utd v West Ham

Jumapili, Agosti 29, 2010
Bolton v Birmingham
Liverpool v West Brom
Sunderland v Man City
Aston Villa v Everton

La Liga:
Jumapili, Agosti 29, 2010
Atletico Madrid v Sporting Gijon
Deportivo La Coruna v Real Zaragoza
Espanyol v Getafe
Hercules v Athletic Bilbao
Levante v Sevilla
Malaga v Valencia
Mallorca v Real Madrid
Osasuna v Almeria
Racing Santander v Barcelona
Real Sociedad v Villarreal

Jumapili, Septemba 12, 2010
Almeria v Real Sociedad
Athletic Bilbao v Atletico Madrid
Barcelona v Hercules
Getafe v Levante
Real Madrid v Osasuna
Real Zaragoza v Malaga
Sevilla v Deportivo La Coruna
Sporting Gijon v Mallorca
Valencia v Racing Santander
Villarreal v Espanyol

Jumapili, Septemba 19, 2010
Atletico Madrid v Barcelona
Deportivo La Coruna v Getafe
Espanyol v Almeria
Hercules v Valencia
Levante v Villarreal
Malaga v Sevilla
Mallorca v Osasuna
Racing Santander v Real Zaragoza
Real Sociedad v Real Madrid
Sporting Gijon v Athletic Bilbao

Jumatano, Septemba 22, 2010
Almeria v Levante
Athletic Bilbao v Mallorca
Barcelona v Sporting Gijon
Getafe v Malaga
Osasuna v Real Sociedad
Real Madrid v Espanyol
Real Zaragoza v Hercules
Sevilla v Racing Santander
Valencia v Atletico Madrid
Villarreal v Deportivo La Coruna

Jumapili, Septemba 26, 2010
Athletic Bilbao v Barcelona
Atletico Madrid v Real Zaragoza
Deportivo La Coruna v Almeria
Espanyol v Osasuna
Hercules v Sevilla
Levante v Real Madrid
Malaga v Villarreal
Mallorca v Real Sociedad
Racing Santander v Getafe
Sporting Gijon v Valencia

Serie A:
Jumamosi, Agosti 28, 2010
Udinese v Genoa
Roma v Cagliari

Jumapili, Agosti 29, 2010
AC Milan v Lecce
Bari v Juventus
Bologna v Inter Milan
Chievo v Catania
Fiorentina v Napoli
Palermo v Cagliari
Parma v Brescia
Roma v Cesena
Sampdoria v Lazio
Udinese v Genoa

Jumapili Septemba 12, 2010
Brescia v Palermo
Cagliari v Roma
Catania v Parma
Cesena v AC Milan
Genoa v Chievo
Inter Milan v Udinese
Juventus v Sampdoria
Lazio v Bologna
Lecce v Fiorentina
Napoli v Bari

Jumapili, Septemba 19, 2010
AC Milan v Catania
Bari v Cagliari
Cesena v Lecce
Chievo v Brescia
Fiorentina v Lazio
Palermo v Inter Milan
Parma v Genoa
Roma v Bologna
Sampdoria v Napoli
Udinese v Juventus

Jumatano, Septemba 22, 2010
Bologna v Udinese
Brescia v Roma
Cagliari v Sampdoria
Catania v Cesena
Genoa v Fiorentina
Inter Milan v Bari
Juventus v Palermo
Lazio v AC Milan
Lecce v Parma
Napoli v Chievo

Jumapili, Septemba 26, 2010
AC Milan v Genoa
Bari v Brescia
Catania v Bologna
Cesena v Napoli
Chievo v Lazio
Fiorentina v Parma
Juventus v Cagliari
Palermo v Lecce
Roma v Inter Milan
Sampdoria v Udinese

Bundesliga:
Ijumaa, Agosti 20, 2010
Bayern Munich v Wolfsburg

Jumamosi, Agosti 21, 2010
Borussia M'gladbach v Nuremberg
Cologne v FC Kaiserslautern
Hannover 96 v Eintracht Frankfurt
SC Freiburg v St Pauli
TSG Hoffenheim v Werder Bremen
Hamburg v Schalke 04

Jumapili, Agosti 22, 2010
Mainz v VfB Stuttgart
Borussia Dortmund v Bayer Leverkusen

Ijumaa, Agosti 27, 2010
FC Kaiserslautern v Bayern Munich

Jumamosi, Agosti 28, 2010
Eintracht Frankfurt v Hamburg
Nuremberg v SC Freiburg
Schalke 04 v Hannover 96
Werder Bremen v Cologne
Wolfsburg v Mainz
St Pauli v TSG Hoffenheim

Jumapili, Agosti 29, 2010
Bayer Leverkusen v Borussia M'gladbach
VfB Stuttgart v Borussia Dortmund

Ijumaa, Septemba 10, 2010
Mainz v FC Kaiserslautern

Jumamosi, Septemba 11, 2010
Borussia Dortmund v Wolfsburg
Borussia M'gladbach v Eintracht Frankfurt
Hamburg v Nuremberg
Hannover 96 v Bayer Leverkusen
SC Freiburg v VfB Stuttgart
Bayern Munich v Werder Bremen

Jumapili, Septemba 12, 2010
TSG Hoffenheim v Schalke 04
Cologne v St Pauli

Jumamosi, Septemba 18, 2010
Bayer Leverkusen v Nuremberg
Bayern Munich v Cologne
Eintracht Frankfurt v SC Freiburg
Kaiserslautern v TSG Hoffenheim
Schalke 04 v Borussia Dortmund
St Pauli v Hamburg
VfB Stuttgart v Borussia M'gladbach
Werder Bremen v Mainz
Wolfsburg v Hannover 96

Jumatano, Septemba 22, 2010
Bayer Leverkusen v Eintracht Frankfurt
Borussia Dortmund v FC Kaiserslautern
Borussia M'gladbach v St Pauli
Hamburg v Wolfsburg
Hannover 96 v Werder Bremen
Mainz v Cologne
Nuremberg v VfB Stuttgart
SC Freiburg v Schalke 04
TSG Hoffenheim v Bayern Munich

Jumamosi, Septemba 25, 2010
Bayern Munich v Mainz
Cologne v TSG Hoffenheim
Eintracht Frankfurt v Nuremberg
FC Kaiserslautern v Hannover 96
Schalke 04 v Borussia M'gladbach
St Pauli v Borussia Dortmund
VfB Stuttgart v Bayer Leverkusen
Werder Bremen v Hamburg
Wolfsburg v SC Freiburg

Ligue One
Jumamosi, Agosti 14, 2010
Brest v Auxerre
Lorient v Nice
Monaco v Montpellier
Nancy v Rennes
St Etienne v Sochaux
Valenciennes v Marseille
Arles v Lens

Jumapili, Agosti 15, 2010
Bordeaux v Toulouse
Caen v Lyon
Lille v PSG

Jumamosi, Agosti 21, 2010
Lens v Monaco
Lyon v Brest
Marseille v Lorient
Nice v Nancy
Rennes v St Etienne
Toulouse v Arles
Auxerre v Valenciennes

Jumapili, Agosti 22, 2010
Montpellier v Caen
Sochaux v Lille
PSG v Bordeaux

Jumamosi, Agosti 28, 2010
Arles v Rennes
Lorient v Lyon
Nancy v Toulouse
St Etienne v Lens
Valenciennes v Montpellier
Caen v Brest

Jumapili, Agosti 29, 2010
Lille v Nice
Monaco v Auxerre
Sochaux v PSG
Bordeaux v Marseille

Jumamosi, Septemba 11, 2010
Auxerre v Caen
Brest v Lorient
Lens v Lille
Lyon v Valenciennes
Marseille v Monaco
Montpellier v Nancy
Nice v Bordeaux
PSG v Arles
Rennes v Sochaux
Toulouse v St Etienne

Jumamosi, Septemba 18, 2010
Arles v Marseille
Bordeaux v Lyon
Lille v Auxerre
Lorient v Caen
Monaco v Toulouse
Nancy v Brest
PSG v Rennes
Sochaux v Nice
St Etienne v Montpellier
Valenciennes v Lens

Jumamosi, Septemba 25, 2010
Auxerre v Nancy
Brest v Valenciennes
Caen v Bordeaux
Lens v PSG
Lorient v Monaco
Lyon v St Etienne
Marseille v Sochaux
Montpellier v Arles
Nice v Rennes
Toulouse v Lille

Madega akabidhi Yanga sh. milioni 199.7


MWENYEKITI wa Yanga, Lloyd Nchunga (kushoto) akipokea baadhi ya hati na nyaraka mbalimbali za klabu hiyo kutoka kwa mwenyekiti wa zamani, Iman Madega wakati wa makabidhiano yaliyofanyika jana makao makuu ya klabu hiyo mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam. (Picha na Emmanuel Ndege).

MWENYEKITI wa zamani wa klabu ya Yanga, Imani Madega ameukabidhi uongozi mpya chini ya Mwenyekiti Llyord Nchunga akaunti nne za klabu hiyo zenye jumla ya sh. milioni 199.7.
Mbali na kiasi hicho cha fedha, Madega pia amemkabidhi Nchunga mabasi matatu, nyaraka mbalimbali za klabu na daftari lenye jumla ya majina ya wanachama 7,000 wa Yanga.
Makabidhiano hayo yalifanyika jana mchana makao makuu ya klabu hiyo yaliyopo mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam na kushuhudiwa na Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako. Katika makabidhiano hayo, Madega pia alimpatia Nchunga hati za majengo mawili ya klabu hiyo, hati za mabasi matatu, likiwemo moja aina ya Mitsubishi, ambalo linadaiwa sh. 500,000.
Yanga inazo akaunti nne katika benki ya CRDB tawi la Vijana. Akaunti hizo ni kwa ajili ya usajili wa wachezaji, mishahara ya wachezaji na benchi la ufundi na akaunti ya klabu.
Moja ya akaunti hizo inazo sh. milioni 197,869, nyingine inazo sh. milioni moja, nyingine inazo sh. 795,629 wakati akaunti ya klabu haina pesa.
Madega pia alimkabidhi Nchunga nyaraka zinazohusu madeni ya klabu hiyo, likiwemo deni la sh. milioni 6.6 la hoteli ya Tamal, deni la sh. milioni 10 la Kampuni ya All Sports, deni la sh. milioni 5.6 la hoteli ya Valley View na deni la dola 30,000 za Marekani, ambalo Yanga inadaiwa na Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA).
Yanga inadaiwa kiasi hicho kikubwa cha fedha na CECAFA kufuatia kugomea pambano lake la kutafuta mshindi wa tatu wa michuano ya Kombe la Kagame dhidi ya Simba mwaka 2008.
Akizungumza katika hafla hiyo, Madega alimpongeza Nchunga na viongozi wenzake wapya kwa kushinda katika uchaguzi mkuu wa klabu hiyo uliofanyika Julai 18 mwaka huu.
Alisema nyenzo alizomkabidhi Nchunga ni kwa ajili ya kazi za Yanga hivyo anapaswa kuzitunza na kuzifanyiakazi kama alivyofanya yeye na viongozi wenzake waliopita.
Madega alisema wakati uongozi wake ulipoingia madarakani mwaka juzi, alikabidhiwa katiba na kitabu chenye orodha ya wanachama 800, lakini sasa idadi hiyo imeongezeka na kufika 7,000.
Mwenyekiti huyo wa zamani wa Yanga alimshukuru mfadhili mkuu wa klabu hiyo, Yussuf Manji kwa kuisaidia kwa hali na mali. Pia aliishukuru Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) na Kampuni ya African Medical Clinic. Alitamba kuwa, chini ya uongozi wake, Yanga iliweza kutwaa ubingwa wa ligi kuu mara mbili pamoja na Kombe la Tusker, hivyo alimtaka Nchunga ahakikishe wanafuata nyayo zao ili kuijengea heshima klabu hiyo.

Simba, Yanga presha tupu

HOMA ya pambano la watani wa jadi wa soka Simba na Yanga imeenza kupanda baada ya timu hizo kwenda kujichimbia kambini Bagamoyo mkoani Pwani na katika visiwa vya Zanzibar.
Simba na Yanga zinatarajiwa kupambana Aprili 18 mwaka huu katika mechi maalumu ya kuwania Ngao ya Hisani, itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Mechi hiyo ni maalumu kwa ufunguzi wa ligi kuu ya Vodacom.
Habari kutoka ndani ya klabu hizo zimeeleza kuwa, Simba iliondoka mjini Dar es Salam juzi kwenda kuweka kambi Zanzibar kwa ajili ya kujiandaa na pambano hilo wakati Yanga imekwenda kujichimbia Bagamoyo.
Mbali na kulikimbia jiji, viongozi wa klabu hizo wamekuwa wakiwatuma ‘mashushu’ wao kwenda kuwachunguza wachezaji wao waliopo kwenye kambi ya kikosi cha timu ya taifa, Taifa Stars iliyopo kwenye hoteli ya F & J Annex mjini Dar es Salaam.
Kazi ya mashushu hao ni kuchunguza mienendo ya wachezaji na kutoa taarifa kwa uongozi, hasa zinazohusu tuhuma za kupokea rushwa kutoka upande wa upinzani.
Viongozi wa klabu hizo wamekuwa na wasiwasi kwamba, upande mwingine unaweza kwenda kuwarubuni wachezaji wao ili wacheze chini ya kiwango katika mechi hiyo.
Uchunguzi huo pia ulikuwa ukifanywa na mashushu hao kwenye mazoezi ya timu hiyo yaliyokuwa yakifanyika aidha kwenye uwanja wa Karume na Uhuru, Dar es Salaam.
Viongozi wa klabu hizo wamepanga kuwachukua wachezaji wao mara baada ya mechi ya kirafiki ya kimataifa kati ya Taifa Stars na Kenya, iliyochezwa jana kwenye Uwanja wa Uhuru.
Wachezaji wa Yanga waliopo kwenye kikosi cha Taifa Stars ni Shadrack Nsajigwa, Stephano Mwasika, Nurdin Bakari, Athumani Idd,Kigi Makasi, Abdi Kassim, Jerryson Tegete na Nadir Haroub Canavaro.
Wachezaji wa Simba waliomo kwenye timu hiyo ni Juma Kaseja, Salum Kanoni, Abdulrahim Humud, Uhuru Seleman, Mussa Hassan 'Mgosi’, Kelvin Yondani na Juma Jabu.

Stars, Harambee hakuna mbabe


Na Deusdedit Undole
TIMU ya soka ya taifa, Taifa Stars jana ilishindwa kuutumia vyema uwanja wake wa nyumbani baada ya kulazimishwa kutoka sare ya bao 1-1 na Kenya, Harambee Stars.
Katika mechi hiyo ya kirafiki ya kimataifa, iliyochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam, Harambee ilijipatia bao hilo la pekee kipindi cha kwanza kupitia kwa mshambuliaji wake nyota, MacDonald Mariga kabla ya Stars kusawazisha kipindi cha pili kupitia kwa Mrisho Ngasa.
Mariga, anayecheza soka ya kulipwa katika klabu ya Inter Milan ya Italia, aliifungia Harambee bao la kuongoza dakika ya 14 kwa shuti la mpira wa adhabu, nje kidogo ya eneo la hatari.
Mwamuzi Oden Mbaga wa Tanzania aliamuru ipigwe adhabu hiyo baada ya beki Kelvin Yondani wa Stars kumwangusha Dennis Oliech katika eneo hilo.
Harambee ililianza pambano hilo kwa kasi na nusura ipate bao dakika ya 11 wakati Mariga allipofumua shuti kali nje kidogo ya eneo la hatari, lakini lilipanguliwa na kipa Shabani Kado wa Stars na kuwa kona, ambayo haikuzaa matunda.
Katika dakika za mwanzo za mechi hiyo, Harambee Stars ililisakama mara kwa mara lango la Stars, hasa washambuliaji wake, Oliech na Mariga, ambao walikuwa mwiba mkali kwa mabeki wa Tanzania.
Stars ingeweza kufunga bao dakika ya 39 wakati Mussa Hassan ‘Mgosi’ alipopewa pasi na Uhuru Selemani akiwa ndani ya 18,lakini shuti lake lilipaa juu ya lango. Timu hizo zilikwenda mapumziko Harambee ikiwa mbele kwa bao 1-0.
Bao la kusawazisha la Stars lilifungwa na Mrisho Ngasa dakika ya 57 baada ya mabeki wa Harambee kuzembea kumkaba wakidhani ameotea.
Oliech angeweza kuiongezea bao Harambee dakika ya 66, lakini shuti lake lilipanguliwa kifundi na kipa Kado wa Stars na kuwa kona, ambayo haikuzaa matunda.
Mgosi itabidi aijutie nafasi aliyoipata dakika ya 75 baada ya kupewa pasi safi na Ngasa na kubaki ana kwa ana na kipa Obungu wa Harambee, lakini shuti lake lilitoka nje.
Stars: Shabani Kado, Idrisa Rajabu/ Stephano Mwasika, Shadrack Nsajigwa, Kelvin Yondani/ Aggrey Morris, Nadir Haroub, Nurdin Bakari, Abdi Kassim,Abdulrahim Humud, Jabir Azizi/Athumani Iddi, Uhuru Selemani/Selemani Kassim, Jerry Tegete/Mussa Hassan, Mrisho Ngasa.
Harambee: Wilson Obungu, Julius Owino, George Owino, Lloyd Wahome, Edgar Ochieng, Patrick Ooko/ Paul Welle, MacDonald Mariga, George Odhiambo/Anthony Kimani, Dennis Oliech, John Barasa/Allan Wanga, Kelvin Omondi/ James Stuma.

Mwakalebela afikishwa mahakamani



KATIBU Mkuu wa zamani wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Fredrick Mwakalebela amefikishwa mahakamani na kusomewa shtaka la tuhuma za kutoa rushwa wakati wa mchakato wa upigaji kura za maoni kwa wagombea wa Chama cha Mapinduzi.
Mwakalebela alisomewa shtaka hilo jana na Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Prisca Mpela mbele ya hakimu wa mahakama ya wilaya ya Iringa, Festo Lwila.
Hata hivyo, Mwakalebela hakuwepo mahakamani kutokana na kuomba udhuru na kesi yake imepangwa kutajwa Agosti 17 mwaka huu.
Kiongozi huyo wa zamani wa TFF, aliyekuwa akiwania kuteuliwa kuwa mgombea wa Jimbo la Iringa Mjini, anatuhumiwa kutoa rushwa ya pesa taslimu sh. 100,000 kwa Mwenyekiti wa kijiji cha Mkoga, Hassan Luhanga, ambazo alitakiwa kuzigawa kwa wanachama wa CCM 30 ili wamchague katika kura za maoni.
Lwila aliieleza mahakama kuwa, kutoa rushwa ni kinyume cha sheria namba 11 ya mwaka 2007 kifungu cha 15 (1) (b), kinachokwenda sambamba na sheria ya gharama za uchaguzi namba 16 ya mwaka 2010 kifungu namba 21 (1) (a) na kifungu cha 24 (8).