KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, August 26, 2010

RAGE: Tujenge tabia ya kuwaamini wachezaji wetu


SWALI: Ukiwa Mwenyekiti wa Simba, kumekuwa na tabia kwa baadhi ya viongozi, wanachama na mashabiki wa klabu hiyo na watani wenu wa jadi Yanga kuwatuhumu wachezaji kupokea rushwa kutoka kwa timu pinzani kila inapotokea timu yenu kufungwa na wapinzani wenu wa jadi. Je, unazungumziaje tuhuma za aina hii?
JIBU:Hakika leo umenifurahisha kwa kuniuliza swali hilo. Kwa kweli mimi binafsi na viongozi wenzangu wa Simba tunapinga mawazo ya watu hao, kwani tunapoamua kusajili mchezaji, ina maana kwamba tuna imani naye kwa ajili ya kutufanyia kazi na ni jukumu letu kumlipa mshahara mzuri ili aweze kutufanyia kazi nzuri.
Licha ya jambo hilo, unajua timu kama Simba ina watu wengi, ambao wengine wana uwezo wa kufikiria mambo na wengine hawana, hivyo wapo watu kila kukicha wanafikiria kutaka kukuza migogoro ili waweze kufanikisha malengo yao.
Kwa kweli watu wanaoeneza tuhuma kwamba mchezaji fulani amehongwa, wamekuwa wananikera sana na sio siri wakija kwangu kama hawana ushahidi, lazima nitawachukulia hatua kali. Nina imani ndani ya kikosi cha Simba tabia hizo hazipo na hao wanaoeneza mambo hayo huenda ni wapinzani wetu.
Katika mechi yetu na Simba, tuliona jinsi wachezaji walivyojituma na mpaka hatua ya kupigiana penalti ilipofika, tuliona kabisa kuwa walifanyakazi waliyotumwa na klabu. Kama wangekuwa na ajenda ya kutufungisha, kwanini wasingefanya hivyo mapema katika muda wa dakika 90? Hizo ni kauli za watu, ambao wana nia mbaya na klabu yetu, ambayo kwa sasa imetulia kutokana na kuwepo ushirikiano mkubwa.
SWALI: Kufuatia kuwepo kwa tetesi hizo, ukiwa mwenyekiti wa Simba, unachukua hatua gani ili kukomesha tabia hii?
JIBU: Zipo taratibu tunazopaswa kuzifuata. Siwezi kufanyakazi kwa mazoea. Kama kweli mtu anafanya hivyo, ni vyema akaacha kwani tutamchukulia hatua kali kulingana na sheria kwani zipo sheria kuhusu suala hilo, zinasubiri mtu afanye kosa akumbane nazo. Cha msingi ni kwamba nawaomba wanachama wenzangu wa Simba, kama wapo waliokuwa wakizusha tuhuma hizo, waache mara moja kutamka maneno ya namna hiyo kwani yanavunja moyo wachezaji.
Mimi nasisitiza kwamba wachezaji wetu wanapata matunzo mazuri, mishahara mizuri na kila kitu wanakipata muda wowote wanapokihitaji kwa hiyo watu wanaoeneza uvumi huo pengine ni wapinzani wetu Yanga.
Simba kuna watu wenye heshima zao, inawezekana wapinzani wetu wanataka kutumia njia ya kutugombanisha ili mawazo yao ya kutaka kuchukua ubingwa yaweze kutimia. Hilo tumeligundua na tupo makini sana.
Nawaomba wanachama na wapenzi wa Simba watuamini sisi viongozi wao na wachezaji kwa vile sifikiri kama kuna mchezaji, ambaye anaweza kufanya hivyo. Ni vyema tukajenga imani kwa wachezaji wetu ili waweze kufanyakazi tuliyowapa kwa uaminifu.
SWALI: Uongozi uliopita chini ya Mwenyekiti Hassan Dalali ulileta mafanikio makubwa kwa Simba, ikiwa ni pamoja na kutwaa ubingwa wa ligi kuu kabla haijamalizika. Nini mikakati ya uongozi wako katika ligi ya msimu huu na michuano ya klabu bingwa Afrika?
JIBU: Uongozi umepanga malengo yake. Lakini tupo sambamba na benchi la ufundi la timu yetu ili tuweze kutimiza ahadi na mambo ambayo tumekubaliana. Ninachoweza kusema ni kwamba, tunapaswa kulitetea taji letu na pia kufanya vizuri katika michuano ya Afrika.
Matarajio yetu ni kuhakikisha kwamba tunapata uwezo wa kufanya mazoezi ya nguvu na kuweka kambi hata nje ya Tanzaniai ili tuweze kuwa na timu yenye uwezo mkubwa wa kushinda mashindano mbalimbali itakayoshiriki.
Kwa sasa, mipango yetu inakwenda vizuri. Hata Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kupitia rais wake, Leodegar Tenga limetupongeza na kuwataka wapinzani wetu Yanga watuige.
Na kwa kweli, mafanikio ya Simba yamekuwa yakiigwa na Yanga. Tazama hata tamasha la ‘Simba Day’ tayari nao wameshaanza kuliiga. Hivyo tutaendelea kuwa wabunifu ili tuiweke Simba katika njia sahihi na pia iweze kujitegemea.
SWALI: Baada ya kuingia madarakani, uliahidi kwamba utasimama imara kuhakikisha Simba inajitegemea na kuongeza vyanzo vyake vya mapato, ikiwa ni pamoja na kusaka wadhamini wapya. Je, umefikia wapi hadi sasa?
JIBU: Mambo hadi sasa yanakwenda vizuri na siku chache zijazo tunaweza kuwatangaza wadhamini wengine. Jambo la kwanza, ambalo tunalipigania kwa sasa ni kuhakikisha jengo letu linakuwa safi na linatumika kutuingizia pesa.
Na kama mlivyoweza kuona, tumeshaanza kulifanyia ukarabati mkubwa kwa kulipaka rangi kwa kutumia uwezo wetu wenyewe na kazi hiyo inakwenda vizuri. Pia tumeanza kufunga viyoyozi kwenye vyumba vyote vya jengo hilo na haya kwetu ni maendeleo makubwa, tofauti na miaka iliyopita.
Sambamba na hilo, tumeweza kusajili nembo ya klabu yetu na nimeshatoa siku 90 kwa mtu yeyote, anayeuza vifaa vyenye nembo ya Simba kuacha mara moja kufanya hivyo, vinginevyo hatua kali zitachukuliwa dhidi ya watu hao baada ya muda huo kumalizika.
SWALI: Uongozi wa Simba unayo mikakati yoyote ya kuhamishia kambi ya timu yenu kwenye jengo la klabu badala ya kwenye hoteli za kitalii kwa lengo la kupunguza gharama?
JIBU: Hilo linawezekana, lakini ningependa kuona kwanza kazi ya kulikarabati jengo hilo inakamilika kwa asilimia mia moja. Kama hali itakuwa nzuri, sioni kwa nini tusiweke kambi klabuni. Jambo la kufurahisha ni kuona kwamba kazi hiyo inakwenda vizuri na kazi zote za Simba kwa sasa zinafanyika klabuni.
SWALI: Vipi kuhusu ufuatiliaji wa viwanja vyenu vilivyopo Boko na pale Jangwani?
JIBU: Kazi hiyo inaendelea kwa mafanikio makubwa licha ya kuwepo mabadiliko kidogo ya kiutendaji kwenye Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, kufuatia mabadiliko yaliyofanywa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, William Lukuvi. Nina imani kwamba tukishakamilisha kazi ya kuvipata viwanja hivyo, tutajua la kufanya. Lakini kazi ya kwanza itakuwa ni kusaka wadhamini.
SWALI: Uongozi wako una sera gani kuhusu kuuza wachezaji nje ya nchi kwani kumekuwepo na taarifa kwamba baadhi ya wachezaji wa Simba wanatakiwa kwenda nje ya nchi kufanya majaribio ya kucheza mpira wa kulipwa?
JIBU: Hili ni jambo zuri kwa klabu kwa sababu endapo mchezaji atafuzu majaribio nje, tutapata pesa na mchezaji naye atanufaika kimaisha. Kwa vile sisi ndio wazazi, kama kuna timu inataka kumfanyia majaribio mchezaji wetu, milango ipo wazi kwa kufuata taratibu husika za TFF na mashirikisho ya soka ya kimataifa.
SWALI: Kwa muda mrefu sasa, kumekuwepo na mchezo mchafu, unaofanywa na baadhi ya watu kutengeneza tiketi feki wakati wa mechi mbalimbali kubwa na za kimataifa na kuziuza kwa mashabiki, hivyo kuzikosesha mapato klabu. Klabu yako imekuwa ikichukua hatua gani kupambana na tatizo hili?
JIBU: Ninachoweza kusema ni kwamba mchezo huo kwetu sisi Simba haupo. Nimekuwa nikisikia tu taarifa hizo kupitia kwenye vyombo vya habari kwamba baadhi ya watu walikamatwa na polisi baada ya kukutwa na tiketi hizo. Lakini sipendi kulizungumzia kwa undani zaidi jambo hilo kwa sababu lipo mahakamani. Isipokuwa kwa upande wetu, akikamatwa mtu ametenda jambo hilo, atachukuliwa hatua za kisheria. Kama wapo watu wa Simba wenye tabia hiyo, ni vyema wakaacha mara moja. Tumejipanga vyema kukabiliana na tatizo hilo.
SWALI: Kwa sasa wewe ni mwenyekiti wa chama cha soka mkoani Tabora, ni mwenyekiti wa Simba na sasa umengia katika kinyang’anyiro cha kuwania ubunge wa jimbo la Tabora Mjini kupitia CCM. Je, utamudu vipi kuvitumikia vyeo vyote hivyo kwa wakati mmoja?
JIBU: Naona ndugu yangu unataka kwenda mbele kwa haraka zaidi. Ninachokuomba ni utulie kwanza na baada ya uchaguzi mkuu kumalizika, ndipo nitakapojua nini la kufanya. Lakini kwa sasa mimi bado ni mwenyekiti wa Simba na Tabora na nitaendelea kushirikiana na viongozi wenzangu kuleta maendeleo katika maeneo ninayoongoza.
SWALI: Kutokana na kauli yako, unataka kusema kwamba iwapo utachaguliwa kuwa mbunge, utafikiria kujiuzulu cheo kimoja katika hivyo vitatu?
JIBU: Ninakuomba vuta subira, utaelewa mambo yote. Mimi ni mtu wa vitendo, kwa maana hiyo nitahakikisha Simba inakwenda mbele na hata chama cha soka cha mkoa wa Tabora kinafanyakazi zake vizuri na nina imani msimu huu tunaweza kupandisha timu ikacheza ligi kuu msimu ujao wa 2011/2012.

No comments:

Post a Comment