KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 21, 2010

AZAM YAMKANA PHIRI


UONGOZI wa klabu ya Azam umesema, hauna mpango wa kumnyakua Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Phiri katika mzunguko wa pili wa ligi kuu ya Tanzania.
Azam imesema, inauheshimu mkataba wa Phiri na Simba na kusisitiza kuwa, hauwezi kufanya mazungumzo na kocha huyo ama kufikiria kumwajiri wakati bado ana kibarua sehemu nyingine.
Msimamo huo wa Azam umekuja siku chache baada ya baadhi ya vyombo vya habari nchini kuripoti wiki hii kuwa, klabu hiyo imefanya mazungumzo na Phiri kwa lengo la kumwajiri.
Akizungumza kwa njia ya simu kutoka Turiani mjini Morogoro jana, Mratibu wa timu hiyo, Mohamed King alisema hakuna kiongozi yeyote wa klabu hiyo aliyewahi kukutana na kufanya mazungumzo na Phiri.
"Ninachoweza kusema ni kwamba, habari hizo ni za uzushi kwa sababu hazina ukweli wowote. Sisi kama Azam tunaheshimu mkataba kati ya Phiri na Simba,”alisema.
Mratibu huyo alisema, kwa sasa Azam itaendelea kuwa chini ya kocha wake mkuu, Itamar Amorin kutoka Brazil akisaidiwa na Habibu Kondo.
Baadhi ya vyombo vya habari viliripoti kuwa, Phiri huenda akajiunga na Azam siku chache zijazo baada ya kutokea hali ya kutokuelewana kati yake na viongozi wa Simba.
Hata hivyo, habari za uhakika kutoka ndani ya Simba zimeeleza kuwa, mkataba wa Phiri kuinoa timu hiyo unatarajiwa kumalizika mwishoni mwa mwezi ujao.
Naye Ofisa Habari wa Simba, Clifford Ndimbo amesema, taarifa za Phiri kwenda Azam sio za kweli kwa vile mkataba wa kocha huyo unatarajiwa kumalizika Januari mwakani.
"Phiri hawezi kuondoka Simba kwa sababu bado ana mkataba nahajawahi kuzungumza na viongozi wa Azam,"alisema Ndimbo alipozungumza kwa njia ya simu jana kutoka Mwanza.

No comments:

Post a Comment