KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 17, 2010

Amini aamua kutoka kivyake


MSANII chipukizi wa muziki wa kizazi kipya nchini, Amini kutoka kundi la THT amedokeza kuhusu mbinu anazotumia kimuziki ili kujiweka kwenye matawi ya juu.
Amini, ambaye kwa sasa anatamba kwa kibao chake cha ‘Unikimbie’, alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, anazo nguzo kuu tatu, ambazo amekuwa akizitekeleza kwa lengo la kutimiza azma yake hiyo.
Msanii huyo anayechipukia alisema, amekuwa akitekeleza nguzo hizo kila anapokuwa kwenye maandalizi ya kutoa nyimbo mpya, ndiyo sababu zimekuwa zikiwavutia mashabiki wengi wa muziki huo.
"Kabla sijatunga wimbo wowote, ninakuwa makini katika kuhakikisha nimetuliza kichwa changu, kwani ninakuwa nimetenga muda muafaka wa kuifanyakazi hiyo ipasavyo," alisema Amini, ambaye ni miongoni mwa wasanii chipukizi wanaong'ara kwa sasa.
Aliitaja nguzo yake ya kwanza kuwa ni kukiamini kila anachokifikiria na kukifanyiakazi mara moja kwa kuandaa melodi nzuri kwa ajili ya kuwavutia mashabiki wake.
"Pia ninahakikisha nakuwa makini ninapoutengeneza wimbo wangu na baada ya kumaliza, ninarudia mwanzo mpaka mwisho kwa usahihi na baada ya hapo, ninahakikisha vibwagizo vya wimbo wangu vimekaa sawa," alisema Amini.
Aliitaja nguzo yake ya pili kuwa ni namna anavyoweza kuandaa maneno mazuri ya wimbo na kuongeza kuwa, huo ndio msingi bora wa kuzifanya nyimbo zake zikubalike na mashabiki.
Kwa mujibu wa Amini, nguzo yake ya tatu ni kuhakikisha anafuata misingi yote ya uimbaji na kuongeza kuwa, hilo ndilo lililomwezesha kufika alipo sasa.
"Nipo makini katika kufuata misingi ya uimbaji kwani ninajua namna ya kupanda na kushuka ninapotengeneza wimbo na ninahakikisha sitoki nje ya biti," alisisitiza.
Msanii huyo asiyekuwa na makeke alisema, ametoka mbali kimuziki na anazidi kukua taratibu na kujifunza mengi katika fani hiyo na hilo linamsaidia kujijenga vizuri.
Albamu ya pamoja aliyoifanya kwa kushirikiana na msanii Barnabas, ndiyo iliyomwezesha kuwa matawi ya juu na kwa sasa anajiandaa kupakua albamu ya peke yake, ambayo ameshaanza kuiandaa.
"Nilitoka na Barnabas kwa awamu ya kwanza kwa sababu kila mmoja alifahamika kwa nafasi yake, lakini hivi sasa nimeshaanza kuandaa albamu yangu mwenyewe,”alisema.
“Ninatumia muda mwingi hivi sasa katika kuandaa albamu yangu hii kwa sababu nataka iwe kwenye chati ya juu kimuziki. Nimepanga kuikamilisha albamu hii mwanzoni mwa mwaka 2011," alisema Amini.
Alizitaja baadhi ya nyimbo zake, zinazotarajiwa kuwemo kwenye albamu hiyo kuwa ni pamoja na 'Kumanya', 'Tumetoka mbali', 'Anavuruga', 'Subira', 'Mapenzi ya nani duniani' na 'Unikimbie'.

No comments:

Post a Comment