KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 17, 2010

CECAFA yapania kupeleka timu Kombe la Dunia 2014


NAIROBI, Kenya
BARAZA la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) limezindua mkakati wa kutaka ipate mwakilishi katika fainali za Kombe la Dunia za mwaka 2014 zitakazofanyika nchini Brazil.
Mkakati huo ulizinduliwa mwanzoni mwa wiki hii mjini Nairobi nchini Kenya, yakiwa ni makubaliano ya pamoja kati ya CECAFA na Kampuni ya East African Breweries (EABL).
Katika kutekeleza mkakati huo, EABL imeamua kudhamini michuano ya soka ya Kombe la Chalenji, inayotarajiwa kufanyika nchini Tanzania kuanzia Novemba 27 hadi Desemba 12 mwaka huu.
Kampuni hiyo imepanga kutumia dola 450,000 za Marekani kwa ajili ya kudhamini michuano hiyo, itakayozishirikisha nchi 12, zikiwemo nchi tatu waalikwa za Ivory Coast, Malawi na Zambia.
CECAFA inataka nchi zilizo wanachama wake kutumia michuano hiyo kama sehemu ya maandalizi ya mashindano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Afrika za mwaka 2012 na pia fainali za Afrika kwa wachezaji wa ndani (CHAN) zitakazofanyika Machi mwakani nchini Sudan.
Nchi wanachama wa CECAFA zinazotarajiwa kushiriki katika michuano hiyo ni Tanzania Bara, Zanzibar, mabingwa watetezi Uganda, Kenya, Rwanda, Burundi, Ethiopia, Sudan na Somalia.
Akitangaza mkakati huo, Katibu Mkuu wa CECAFA, Nicholas Musonye alisema hawatarajii kurudia aibu ya kukosa fainali za mwaka huu za Kombe la Dunia zilizofanyika nchini Afrika Kusini.
“CECAFA ni kanda pekee ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF) yenye mafanikio makubwa na tunapaswa kupata angalau nafasi moja kati ya tano zilizotengwa kwa bara la Afrika katika fainali zijazo za Kombe la Dunia,”alisema.
Musonye alisema baraza lake limepania kuutumia udhamini wa EABL kuyafanya mashindano ya mwaka huu ya Kombe la Chalenji yawe ya aina yake.
“Fedha tutakazozipata kutoka EABL zitapelekwa moja kwa moja kwa timu shiriki ili kuziwezesha zitoe ushindani mkali,” alisema.
Kwa mujibu wa Musonye, fedha hizo zitatumika kuzisafirisha timu kwenda Dar es Salaam, kuzipatia huduma za malazi na chakula pamoja na usafiri wa ndani.
Mshindi wa michuano hiyo atazawadiwa dola 30,000 za Marekani (sh. milioni 35), wa pili dola 20,000 (sh. milioni 25) na wa tatu dola 10,000 (sh.milioni 15)
“Soka katika ukanda wetu kwa sasa inapata sapoti kubwa, mashabiki wetu wana kiu kubwa ya kupata kiwango bora na kutokana na udhamini huu, tutaweza kuandaa mashindano ya kiwango cha juu na hivyo kukuza kiwango cha soka katika ukanda huu,”alisema Musonye.
Katika uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa EABL, Seni Adetu alimkabidhi Musonye kombe litakaloshindaniwa katika michuano hiyo. Kombe hilo litapitishwa katika nchi sita kabla ya kutua Dar es Salaam.
Adetu alisema udhamini wa mwaka huu wa Kombe la Chalenji ni sehemu ya mipango ya muda mrefu ya EABL kukuza soka katika nchi za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati na kuhakikisha mojawapo ya nchi hizo inafuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za mwaka 2014.

No comments:

Post a Comment