KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 24, 2010

Kuliacha Kombe la Chalenji liondoke, itakuwa aibu nyingine kwa Tanzania

Kuliacha Kombe la Chalenji liondoke, itakuwa aibu nyingine kwa Tanzania
MICHUANO ya soka ya Kombe la Tusker Chalenji imepangwa kuanza mwishoni mwa wiki hii hadi Desemba 12 mwaka huu mjini Dar es Salaam, ikizishirikisha timu za mataifa tisa kutoka Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA).
Mbali na nchi hizo tisa wanachama wa baraza hilo, michuano hiyo pia itazishiriki nchi zingine tatu, ambazo zimealikwa. Nchi hizo ni Ivory Coast, Malawi na Zambia.
Kwa mujibu wa CECAFA, nchi wanachama wa baraza hilo zitakazoshiriki katika michuano ya mwaka huu, ambayo imepangwa katika makundi matatu tofauti ni wenyeji Tanzania Bara, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Somalia, Zanzibar, Ethiopia na Sudan.
CECAFA imesema uamuzi wa kuzialika Ivory Coast, Malawi na Zambia umelenga kuongeza ushindani na pia kukuza soka katika nchi za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, hasa ikizingatiwa kuwa, viwango vya nchi hizo vipo juu ikilinganishwa na nchi nyingi zinazounda baraza hilo.
Katibu Mkuu wa CECAFA, Nicholas Musonye alisema, kwa mara ya kwanza, michuano ya mwaka huu itadhaminiwa na Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL), ambayo itatoa zawadi za jumla ya dola za Marekani 60,000 kwa washindi watatu wa kwanza.
Mbali na kutoa zawadi kwa washindi, Musonye alisema SBL pia itazigharamia timu shiriki usafiri wa ndege wa kwenda na kurudi, chakula na malazi kwa muda wote wa mashindano. Kampuni hiyo itatumia dola 450,000 za Marekani kudhamini michuano hiyo.
Uamuzi wa SBL kudhamini michuano hiyo unastahili kupongezwa, hasa ikizingatiwa kuwa, utaongeza hamasa na ushindani kwa timu shiriki, huku kila moja ikipania kushinda ili ipate zawadi tatu za kwanza za pesa.
Lakini ili michuano hiyo iwe na msisimko na ushindani wa kweli, ni vyema CECAFA ihakikishe kuwa, waamuzi walioteuliwa kuchezesha mechi za michuano hiyo wanafuata na kuheshimu sheria zote 17, badala ya kuchezesha kwa upendeleo kwa lengo la kuzibeba baadhi ya timu.
Hii ni kwa sababu imekuwa ikitokea mara kwa mara, baadhi ya waamuzi wanaoteuliwa kuchezesha michuano hiyo, wamekuwa wakizibeba baadhi ya timu kwa lengo la kuzikomoa timu zingine na hivyo kuharibu kabisa maana nzima ya ushindani.
Lakini kikubwa nilichokilenga kwenye safu hii wiki hii ni kutoa changamoto kwa timu za Tanzania Bara na Zanzibar, kuutumia vyema uenyeji wa michuano hiyo kuhakikisha kombe hilo linabaki nyumbani.
Sababu na uwezo wa timu hizo kulibakisha kombe nyumbani zipo. Ni kwa sababu zinaundwa na wachezaji wengi wenye uzoefu wa michuano ya kimataifa na pia zitakiwa zikicheza kwenye uwanja wa nyumbani, mbele ya maelfu ya mashabiki wake.
Kuliruhusu kombe hilo liondoke nyumbani kama ilivyokuwa miaka kadhaa iliyopita ni aibu na fedheha kubwa kwa Taifa na hali hiyo itawavunja nguvu mashabiki wengi wa soka hapa nchini.
Itakuwa ni sawa na ilivyotokea kwa Simba mwaka 1993 wakati ilipofuzu kucheza fainali za Kombe la CAF, ambapo ilifanikiwa kutoka suluhu na Stella Abidjan ya Ivory Coast mjini Abidjan, lakini ikachapwa mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Ilikuwa siku ya simanzi kubwa kwa mashabiki wa Simba na Watanzania kwa jumla.
Ikumbukwe kuwa, kwa mara ya mwisho, Tanzania Bara ilitwaa kombe hilo mwaka 1994 michuano hiyo ilipofanyika nchini Kenya wakati Zanzibar ililitwaa mwaka 1996 michuano hiyo ilipofanyika nchini Uganda.
Tangu wakati huo, Tanzania Bara na Zanzibar zimekuwa zikishiriki kwenye michuano hiyo kama wasindikizaji, na mbaya zaidi wakati mwingine zimekuwa zikitolewa hatua za awali.
Kwa kuzingatia rekodi hizo, wakati umefika kwa wawakilishi wetu hawa kuhakikisha kuwa, kombe hilo linabaki nchini, si tu kwa ajili ya kurejesha imani kwa mashabiki, bali pia kudhihirisha kuwa, kiwango chetu cha soka nchini kipo juu kama nchi zingine za ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati.
Lakini ili hayo yote yawezekane, timu hizo mbili zinapaswa kucheza kwa kujituma, ikiwa ni pamoja na wachezaji wake kufuata na kuheshimu mafunzo ya makocha wao badala ya kila mchezaji kucheza kwa kutumia kipaji chake.
Kauli ya Kocha Jan Poulsen wa Tanzania Bara kwamba ataitumia michuano hiyo kutengeneza kikosi imara cha Taifa Stars kwa ajili ya michuano ya kufuzu kucheza fainali za Afrika za mwaka 2012 haifai kupewa nafasi kwa sababu watanzania wanataka kuona kombe linabaki nyumbani na si kuitumia michuano hiyo kama mazoezi.
Ni wazi kuwa, iwapo Tanzania Bara na Zanzibar zitashiriki katika michuano hiyo zikiwa na dhamira ya dhati ya kutwaa ubingwa, lengo hilo litatimia kwa vile katika soka, lolote linawezekana. Cha muhimu ni wachezaji kucheza kwa kujituma huku wakiweka mbele utaifa.

No comments:

Post a Comment