KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 17, 2010

Uongozi Yanga wamtikisa Manji


UONGOZI wa klabu ya Yanga umeeleza kukerwa na kitendo cha mfadhili wao, Yusuf Manji kuwapigisha kura wachezaji wa timu hiyo kuhusu utendaji kazi wa viongozi na Kocha Kostadin Papic.
Habari za uhakika kutoka ndani ya klabu hiyo zimeeleza kuwa, kitendo cha Manji kuteta na wachezaji na kuwataka wamueleze utendaji kazi wa viongozi, hakikubaliki kwa vile kimelenga kuwadhalilisha.
Kwa mujibu wa habari hizo, tayari baadhi ya viongozi wameanza kuhoji uhalali wa Manji kuwataka wachezaji wafanye hivyo wakati wenye mamlaka hayo ni wanachama wa klabu hiyo.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa, viongozi wa klabu hiyo walikutana wiki iliyopita kwa ajili ya kumjadili mfadhili huyo kuhusu kitendo chake hicho, lakini haikuweza kufahamika mara moja uamuzi waliofikia.
“Hatuwezi kuvumilia kumuona Manji akitudhalilisha kiasi hiki na hana uwezo wa kuwahoji wachezaji kuhusu utendaji wetu wa kazi. Yeye siye aliyetuchagua, yeye ni mfadhili tu, wenye jukumu hilo ni wanachama,”alisema mmoja wa viongozi wa juu wa klabu hiyo, ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini.
Kiongozi huyo pia alieleza kushangazwa kwao na kauli ya Manji kuwataka Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Davis Mosha na Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano, Seif Ahmed kutafuta kocha atakayechukua nafasi ya Papic na pia kumrejesha mshambuliaji Mrisho Ngasa aliyesajiliwa na Azam FC.
“Sisi tunadhani Manji sasa amefika mbali na kuna kitu anachotaka kifanyika ndani ya Yanga. Lakini sisi kama viongozi tunamuomba atuheshimu kwa sababu tumechaguliwa na wanachama kikatiba na ndiyo wenye uwezo wa kuhoji utendaji wetu wa kazi,”alisema.
Kiongozi huyo alisema kitendo cha Manji kuingilia kati jukumu hilo huenda kimelenga kuzusha mgogoro ndani ya klabu hiyo, ambao unaweza kuathiri mwenendo wa timu katika michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara, ambayo kwa sasa ipo kwenye mapumziko. Manji alikutana na wachezaji wote wa Yanga wiki mbili zilizopita katika ofisi za Kampuni ya Quality Group zilizopo kwenye barabara ya Nyerere, Jijini Dar es Salaam.
Katika kikao hicho, Manji aliwataka wachezaji wapige kura kuhusu uwezo wa Kocha Papic, utendaji wa viongozi wa klabu na mchango wa kila mchezaji kwa timu. Awali, utata ulikuwa umeigubika klabu hiyo kuhusu hatma ya Kocha Papic baada ya kuondoka nchini wiki mbili zilizopita na kurejea kwao Serbia kwa mapumziko.
Kocha huyo, ambaye mkataba wake wa kuinoa timu hiyo unatarajiwa kumalizika Aprili mwaka huu, alikuwa ameweka mgomo baridi wa kukinoa kikosi cha timu hiyo kutokana na kuchelewa kusaini mkataba mpya.
Mgomo huo aliufanya kabla ya mchezo kati ya Yanga na Toto African ya Mwanza, uliofanyika hivi karibuni katika Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro. Katika mechi hiyo, Yanga ilishinda mabao 2-0.

No comments:

Post a Comment