KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 17, 2010

Kuigiza filamu nyingi ni kujimaliza-Monalisa


MWIGIZAJI filamu maarufu wa kike nchini, Yvonne Cherly amefichua kuwa, tabia ya kuigiza filamu nyingi kwa muda mfupi imechangia kushuka kwa hadhi ya fani hiyo.
Yvonne, maarufu kwa jina la Monalisa alisema mjini Dar es Salaam wiki iliyopita kuwa, tabia hiyo haiwajengei heshima wasanii wa fani hiyo bali inawamaliza.
"Lazima utafika wakati, wasanii wa aina hiyo watapotea kabisa. Mashabiki watawachoka haraka na hii ni hatari kwa vile itashusha thamani ya filamu zetu. Msanii anapaswa kufanya mambo kwa mpangilio na hii inaleta heshima, si kukurupuka tu,”alisema.
Monalisa, ambaye ni miongoni mwa wasanii waasisi wa fani hiyo hapa nchini alisema, si kazi rahisi kwa mwigizaji filamu kucheza filamu nyingi kwa muda mfupi na zikawa nzuri.
"Unakuta msanii ndani ya mwezi mmoja anaigiza filamu tano, mtu huyo mmoja kila sehemu unamuona anatokea yeye na uhusika unakuta ni uleule, huko ni kujimaliza,"alisema.
"Msanii unakuwa huna kitu kipya, huna ubunifu, ndio maana ukiangalia filamu nyingi za sasa, hazina jipya. Wasanii wanafanya mambo yaleyale kwa sababu mtu anakuwa hana muda wa kupumzika na akili kufikiria kitu kipya,”aliongeza.
"Kila muda anakuwa ‘bize’ na kukazana kuhakikisha anakamilisha kazi alizonazo. Matokeo yake analipua tu na watazamaji hawapati kitu, ambacho wanategemea, ndio maana mwisho wa siku thamani ya mtu inashuka,”alisisitiza.

No comments:

Post a Comment