KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, November 18, 2010

Sikinde yazuiwa kufanya maonyesho DDC Kariakoo

Kisa? Ukumbi wakodishwa kwa mmiliki mpya

BENDI ya muziki wa dansi ya Mlimani Park Orchestra ‘Sikinde’ imezuiwa kufanya maonyesho kwenye ukumbi wa DDC Kariakoo wa mjini Dar es Salaam.
Uamuzi huo umefikiwa na mmiliki mpya wa ukumbi huo, ….ambaye alishinda tenda ya kuuendesha baada ya Shirika la Uchumi na Maendeleo la Dar es Salaam (DDC) kuamua kuukodisha.
Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Dar es Salaam juzi, kiongozi wa bendi hiyo, Habibu Abbas ‘Jeff’ na Katibu, Hamisi Milambo walisema walitimuliwa kwenye ukumbi huo kuanzia wiki mbili zilizopita.
Kwa mujibu wa Jeff, awali mmiliki huyo aliwaita na kuwaeleza kwamba, atawaruhusu kuendelea na maonyesho yao ya kila Jumapili kwenye ukumbi huo kwa sababu lengo la kila upande ni kufanya biashara.
“Lakini tulishangaa kuona kuwa, baada ya siku moja alituita tena na kutueleza kuwa, hawezi kuturuhusu kufanya maonyesho hayo kama hatutamlipa sh. 200,000 kwa kila onyesho,”alisema.
“Tulishangazwa na uamuzi huo kwa sababu tangu mwanzo, uongozi wa DDC ulituruhusu kufanya maonyesho yetu bure kwenye ukumbi huo licha ya kwamba kwa sasa bendi inajiendesha kwa kujitegemea. Hatuelewi ni makubaliano gani yaliyofikiwa kati ya mmiliki huyo na uongozi wa DDC,”aliongeza.
Kwa upande wake, Milambo alisema wanahisi hiyo ni hujuma iliyoandaliwa na uongozi wa DDC baada ya kutokea hali ya kutokuelewana kati yao, baada ya baadhi ya wanamuziki wa bendi hiyo kufungua kesi ya kupinga kupunguzwa kazini.
“Tulimuomba mmiliki huyo atupunguzie malipo ya ukumbi kwa sababu uwezo wetu kwa sasa ni mdogo kwa sababu tunajiendesha wenyewe. Tulikuwa tayari kumlipa sh. 50,000 kila wiki, lakini aligoma katakata,”alisema.
Milambo alisema kilichowasikitisha zaidi ni kauli za dharau, ambazo zimekuwa zikitolewa na mmiliki huyo, ikiwa ni pamoja na kuwabeza kuwa hawawezi kumfanya lolote na kwamba hawana chao kwenye ukumbi huo.
Kwa mujibu wa Milambo, awali uongozi wa DDC pia ulitaka kuwatimua kufanya mazoezi kwenye ukumbi wa Mlimani kabla ya baadhi ya viongozi wa serikali kuingilia kati na kuuzuia kufanya hivyo.
Milambo na Jeff wameviomba vyombo vya serikali kuingia kati suala hilo ili kuinusuru bendi hiyo kongwe nchini kusambaratika kwa vile kutoweka kwake kutadhoofisha maendelezo ya muziki nchini.
“Bendi pekee kongwe zilizosalia hapa nchini hivi sasa ni Sikinde na Msondo Ngoma. Mojawapo ikitoweka, ni sawa na kusema utambulisho wa muziki wa Tanzania nao utatoweka,”alisema Jeff.
Juhudi za kumtafuta mmiliki mpya wa ukumbi huo pamoja na Meneja Mkuu wa DDC hazikuweza kufanikiwa kwa vile jana ilikuwa siku ya mapumziko kikazi.

No comments:

Post a Comment