KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, November 25, 2010

Yanga yagonga mwamba kwa Lyon

JARIBIO la klabu ya Yanga kumtoa kwa mkopo kipa Ivan Knezevic kwa ajili ya kupata nafasi ya kumuongeza mshambuliaji Davies Mwape, limegonga mwamba, kufuatia timu ya African Lyon kugoma kumsajili kipa huyo.

Mabingwa hao wa zamani wa ligi kuu ya Vodacom walipanga kumpeleka kwa mkopo kipa huyo African Lyon, lakini timu hiyo imesisitiza haimuhitaji mzungu huyo kutoka Serbia.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi katika Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam juzi, mmiliki na meneja mkuu wa African Lyon, Rahim Kangezi alisema wanahitaji wachezaji wazawa zaidi.

“Sisi wenyewe tunatafuta wachezaji wa ndani ili wakifanya vizuri tuwauze, sasa kwa nini tumchukue kipa wa Yanga, ambaye ni mzungu?” Alihoji Kangezi.

Alisema hawana mpango na mchezaji yeyote wa kigeni na waliopo kwenye timu hiyo waking’ara, watawauza nje na ‘biashara’ hiyo inaanzia kwa wachezaji Mbwana Samatta na Hamis Thabiti, ambao wanapelekwa Benfica ya Ureno.

Alisema wachezaji hao walitarajiwa kuondoka jana nchini kwenda kufanya majaribio katika klabu hiyo, huku Jona Kajuna na beki Meshack Abel wakipelekwa Marekani kutafutiwa timu.

“Wachezaji wote wanne wanaondoka Jumatano (jana) na watakuwepo katika nchi hizo kufanya majaribio,” alisema Kangezi.

Kangezi pia alikanusha madai kuwa, Simba imemrejesha Meshack kwa maelezo kwamba, mchezaji huyo anakwenda nje kujaribu bahati yake na kamwe hawezi kukubali kurejea Msimbazi, ambako alikuwepo misimu miwili iliyopita kabla ya kuhamishwa Lyon kwa mkopo.

No comments:

Post a Comment