KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 24, 2010

Q-Chilla avunja ukimya




BAADA ya ukimya wa muda mrefu, msanii nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Abubakar Katwila amesema anatarajia kuibuka na albamu mpya hivi karibuni.

Akihojiwa katika kipindi cha Bongo Planet kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha East Africa mwishoni mwa wiki iliyopita, msanii huyo alisema albamu hiyo itajulikana kwa jina la ‘Machoni’.

Abubakar, maarufu kwa jina la Q-Chilla alisema, amerekodi vibao vilivyomo kwenye albamu hiyo kwa kuwatumia watayarishaji tofauti wa muziki kwa lengo la kuvipa ladha tofauti.

Q-Chilla alisema ukimya wake wa muda mrefu ulitokana na mitihani mbalimbali iliyomkuta katika maisha yake, ambayo alikiri kwamba imempa fundisho kubwa.

“Najua watu wamesema mengi, unaweza kunichukulia vyovyote upendavyo, lakini mitihani ipo na kwangu ni changamoto, watu wasubiri vitu tofauti,”alisema.

Msanii huyo aliyewahi kung’ara kwa kibao chake cha ‘Aseme’ amekiri kuwa, ushindani katika muziki wa kizazi kipya hivi sasa umekuwa mkali, lakini hauwezi kufikia enzi zao.

Alisema wakati alipoanza kutamba katika muziki huo, ushindani ulikuwa mkali zaidi na kila wasanii walipopanda wasanii, vita ya kuwapa mashabiki burudani safi ilikuwa kubwa.

“Enzi zile kila nilipopanda stejini na kuimba, watu walikuwa wakilia. Ilikuwa ukipanda stejini na kumuona msanii huyu na yule, vita inakuwa kali,”alisema.

Akizungumzia hali ya muziki huo kwa sasa, Q-Chilla alisema ushindani upo, wasanii wanafanya vizuri na muziki unakua, lakini pia kuna aina fulani ya upendeleo kwa baadhi ya wasanii.

“Hii ndiyo sababu iliyonifanya nitulie na kuandika zaidi kwa sababu sipaswi kujiona nimebaki peke yangu, haipendezi, mtanichoka haraka,”alisema.

“Kukaa kwangu kimya kwa muda mrefu kumewafanya muwe na hamu na mimi, nahitajika,”aliongeza.

Hata hivyo, Q-Chilla alieleza wasiwasi wake kuwa, muziki wa sasa haudumu kwa muda mrefu kwa vile ni mwepesi na hauna ujumbe wa maana kwa jamii.

“Leo hii mimi nikisimama jukwaani na kuimba ‘Aseme’ na atokee msanii wa sasa aimbe wa kwake, bado mimi nitachukua kijiji changu,”alisema.

No comments:

Post a Comment