KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 17, 2010

NYOSHI: Hakuna bendi kama FM Academia



RAIS wa bendi ya muziki wa dansi ya FM Academia, ‘Wazee wa Ngwasuma’, Nyoshi El Saadat, ametamba kuwa, bendi yake ndiyo inayoongoza kwa kuwa na mashabiki wengi mikoani kuliko bendi zingine.
Akizungumza na Burudani mjini hapa wiki iliyopita, Nyoshi alisema, bendi nyingi maarufu nchini, zinapata mashabiki wengi zinapofanya maonyesho Jijini Dar es Salaam, lakini hali huwa tofauti zinapokwenda mikoani.
Nyoshi alitoa majigambo hayo wakati bendi hiyo ilipokuwa ikifanya onyesho la uzinduzi wa albamu yake mpya ya ‘Vuta nikuvute’, lililofanyika kwenye ukumbi wa Benjamin Mkapa.
Katika onyesho hilo lililohudhuriwa na mashabiki lukuki, bendi hiyo ilifanikiwa kukonga nyoyo zao kutokana na vibao vyao vipya 11 vilivyopigwa kwa mpangilio wa kuvutia.
“FM Academia kila tunapokwenda kwenye mkoa wowote hapa Tanzania, tunaongoza kwa kupata mashabiki wengi. Bendi zingine nyingi zinapata mashabiki zinapokuwa Dar es Salaam, zikitoka kwenda mikoani, hazipati kitu,”alisema Nyoshi.
Aliongeza kuwa, kinachoifanya bendi hiyo kuwa ‘matawi ya juu’ ni kudumu kwa muda mrefu, wasanii wake kufanyakazi kwa umoja, kuwa na nidhamu ndani na nje ya jukwaa na uwajibikaji wa pamoja.
Kwa mujibu wa Nyoshi, albamu hiyo ni bora na akiwa kiongozi, ameshiriki kutunga nyimbo mbili, ‘Jasmini’ na ‘Ushirikiano wa Tanzania na nchi jirani’.
Alizitaja baadhi ya nyimbo zingine zilizomo kwenye albamu hiyo kuwa ni ‘Shida yangu’ na ’Mgeni’, ambazo zimerekodiwa kwenye studio za Metro za mjini Dar es Salaam.
Baadhi ya mashabiki waliohudhuria onyesho hilo walikiri kuwa, bendi ya FM Academia inafahamu vyema kukidhi kiu ya mashabiki wake na wanamuziki wake wana nidhamu ya hali ya juu wanapokuwa stejini.

No comments:

Post a Comment