KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 17, 2010

RAGE: Siondoki Simba ng'o


MWENYEKITI wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage amesema, kamwe hawezi kujiuzulu uongozi wa klabu hiyo kutokana na kuchaguliwa kwake kuwa mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini kwa tiketi ya CCM.
Akihojiwa na kituo cha televisheni cha TBC 1 kutoka mjini Dodoma wiki hii, Rage alisema katiba ya Simba haimzuii kushika nyadhifa mbili kwa wakati mmoja.
Rage alisema, kwa mujibu wa katiba ya Simba, mwenyekiti asipokuwepo, makamu wake ndiye anayeshika majukumu yake ikiwa ni pamoja na kuendesha vikao vya uongozi na mikutano ya wanachama.
“Hivyo hata kama sintakuwepo Dar es Salaam kwa sababu ya shughuli za Bunge, hiyo haisababishi shughuli za klabu kushindwa kuendelea kwa sababu yupo makamu mwenyekiti,”alisema.
Akitoa mfano, Rage alisema wapo baadhi ya wabunge, ambao pia ni viongozi wa taasisi mbalimbali na wamekuwa wakitekeleza majukumu yao yote mawili bila ya kuwepo kwa mwingiliano ama athari yoyote.
Aliwataja baadhi ya wabunge hao kuwa ni pamoja na Kepteni mstaafu John Komba, ambaye ni mbunge wa Jimbo la Mbinga Magharibi kwa tiketi ya CCM na pia Mkurugenzi Mtendaji wa kikundi cha sanaa za maonyesho cha TOT Plus.
Hata hivyo, Rage alisema anatarajia kukutana na viongozi wenzake wa kamati ya utendaji ya Simba mwishoni mwa wiki hii ili kujadili suala hilo kabla ya kulitolea uamuzi wa mwisho.
Wakati huo huo, Rage alithibitisha kuwa, wamekata rufani kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kupinga adhabu iliyotolewa kwa kipa Juma Kaseja.
TFF ilitangaza kumfungia Kaseja kucheza mechi tatu na pia kumtoza faini ya sh. 500,000 kwa tuhuma za kukataa kumpa mkono Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Abbas Kandoro, ambaye alikuwa mgeni rasmi wa mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara, kati ya Simba na Yanga, iliyochezwa Oktoba 16 mwaka huu.
Hata hivyo, TFF imekuwa ikijikanganya kuhusu adhabu hiyo baada ya gazeti moja la kila siku kuchapisha picha iliyomwonyesha Kaseja akipeana mkono na Kandoro wakati wa mechi hiyo.
Kaimu Katibu Mkuu wa TFF, Sunday Kayuni alikaririwa akisema kuwa, taarifa hiyo ilitolewa kimakosa kwa vile Kaseja hakugoma kupeana mkono na Kandoro bali wachezaji wa Yanga.

No comments:

Post a Comment