KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 17, 2010

SPUTANZA yaandaa tuzo ya mwanasoka bora

CHAMA cha Wanasoka wa Zamani nchini (SPUTANZA) kimesema kitaandaa tuzo maalumu kwa ajili ya mchezaji bora wa michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara msimu wa 2010-2011.
Katibu Mkuu wa SPUTANZA, Said George alisema wiki iliyopita mjini Dar es Salaam kuwa, chama chake kimeamua kujitosa kutoa tuzo hiyo kwa lengo la kuipa hadhi zaidi.
Saidi alisema, japokuwa zipo tuzo za wanamichezo bora zinazotolewa kila mwaka na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo nchini (TASWA), wameona ni bora waitengenishe tuzo hiyo na za michezo mingine.
"Hatupingi kuwepo kwa tuzo za TASWA, isipokuwa tuzo ya mchezaji bora wa soka ina hadhi yake. Tunaanza kuitoa kwa mara ya kwanza ligi hii itakapomalizika na wachezaji ndio watakaopendekeza mshindi,"alisema.
Katibu Mkuu huyo wa SPUTANZA alisema, kwa kuanzia watatoa tuzo ya mchezaji bora wa mwaka, mshindi wa pili na wa tatu nakuwataka wahisani mbalimbali kujitokeza kudhamini tuzo hizo.
Wakati huo huo, SPUTANZA imelitaka Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kuvunja mara moja kamati ya kusimamia maadili na hadhi ya wachezaji kwa madai kuwa, imeshindwa kufanyakazi iliyokusudiwa,badala yake imeundwa kwa maslahi binafsi.
Saidi alisema kamati hiyo, ambayo inaongozwa na Wakili Alex Mgongolwa, ambaye ni mnazi mkubwa wa Yanga, imekumbwa na mgongano wa kimaslahi kwa watendaji wake kugubikwa na upenzi badala ya kutenda haki.
"Ni wazi kuwa, Yanga haikufuata taratibu wakati ikivunja mkataba na wachezaji wake wanne, na ni muda mrefu sasa sakata hili halijapatiwa ufumbuzi,”alisema Saidi.
“Na sasa ni usajili wa dirisha dogo, fursa ya wao kupata timu ya kuchezea ni finyu kwa vile uongozi wa Yanga haujawalipa madai yao wanayostahili, "aliongeza.
Alisema chama chake kimeiomba TFF kuzuia usajili wa nyongeza wa Yanga kwa ajili ya mzunguko wa pili wa ligi kuu hadi suala la wachezaji hao litakapopatiwa ufumbuzi.
Saidi alisema wachezaji hao wanne wa Yanga waliaochwa kwenye usajili wa msimu huu, walifuata taratibu zote katika kudai haki zao, lakini wamekuwa wakipigwa danadana isiyokuwa na mwisho.
Wachezaji, ambao Yanga imevunja mikataba yao bila kuwalipa haki zao ni Steven Malashi, John Njoroge, Wisdom Ndhlovu na Ally Msigwa. Mikataba ya wachezaji hao ilitakiwa kumalizika mwaka 2012.
Marashi anaidai Yanga sh. milioni 37.5, Ndhlovu anadai sh.milioni 82, Msigwa sh. milioni 89.7 na Njoroge sh. milioni 44.

No comments:

Post a Comment