KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, January 13, 2011

JENNIFER, Nyota inayochipukia katika filamu


KWA kumtazama tu, mtoto Hanifa Daudi anaonekana kuwa mpole, mwenye aibu na asiye na makeke. Ni mtoto anayependa kuwa karibu na watoto wenzake, wakicheza na kufanya hili na lile. Hivyo ndivyo ilivyo kawaida kwa watoto.
Lakini hali hubadilika anapokuwa akitekeleza majukumu yake ya uigizaji wa filamu, akiigiza matukio mbalimbali yanayohusu filamu husika. Huwa akiwasilisha vyema uhusika wake kiasi cha kuifanya filamu yoyote anayoigiza iwe na mvuto wa aina yake.
Hivyo ndivyo ilivyo katika filamu za ‘This is it’ na ‘Uncle JJ’ zilizotungwa, kutayarishwa na kuongozwa na mwigizaji nyota nchini, Steven Kanumba ambaye ndiye aliyevumbua kipaji cha Hanifa. Ni mwigizaji chipukizi mwenye kipaji cha aina yake.
Kipaji alichonacho katika tasnia hiyo ndicho kilichomwezesha Hanifa, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Jennifer, kuibuka na tuzo ya mwigizaji bora kupitia filamu ya ‘This is it’ iliyotolewa na Min Zanzibar International Film Festival (MIN-ZIFF) mwishoni mwa mwaka jana.
Katika filamu ya ‘This is it’, Jennifer ameigiza kama mtoto mlozi au mshirikina. Filamu hiyo pia ilishinda tuzo ya filamu bora na kupata nafasi ya kuingia katika shindano la Panafrican Film and Television Festival (FESPACO) litakalofanyika baadaye mwaka huu mjini Ouagadougou- Burkina Faso.
Kufuatia kushinda tuzo hiyo, Kampuni ya Steps Entertainment Co Ltd, ambayo inajihusisha na kutengeneza na kusambaza filamu nchini, nayo iliamua kumzawadia Jennifer tuzo maalumu ya kumpongeza katika hafla iliyofanyika hivi karibuni mjini Dar es Salaam.
Akizungumzia ushindi wa Jennifer katika tuzo hiyo, Kanumba alisema binafsi anampongeza kwa hatua aliyofikia akiwa bado na umri mdogo na kwamba anajivunia mafanikio yake hayo.
Kanumba alisema alivumbua kipaji cha Jennifer mwanzoni mwa mwaka 2010 kupitia kampuni yake baada ya kuendesha zoezi la kusaka watoto wenye vipaji vya uigizaji filamu, ambao hawakuwahi kuonekana kwenye luninga.
“Nilifanikiwa kuwapata watoto zaidi ya 40, ambao niliwafundisha na kuwachuja mpaka akapatikana Jennifer na Patrick, ambao chini ya uangalizi wa wazazi wao, niliingia nao makubaliano ya kutocheza filamu yoyote nje ya kampuni yangu,”alisema Kanumba.
“Pia nilihakikisha maendeleo yao shuleni yanapanda na tulikubaliana kwamba, mtoto atakayeshika namba tano kushuka chini, namuondoa kwenye kampuni yangu. Niliwapa changamoto ya kushika nafasi ya kwanza hadi ya nne na nashukuru kwamba wametimiza matakwa yangu,”aliongeza.
“Kwa mihula miwili sasa, Jennifer anaongoza kwa kushika namba moja na hivi karibuni kabla ya kwenda naye Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, alishika nafasi ya pili darasani wakati Patrick amekuwa akishika nafasi ya tatu, ambayo si mbaya,” alisema Kanumba. Jennifer ni mtoto wa Daudi Kibavu na mama yake ni Rose Mogella. Ni mwanafunzi wa shule ya msingi ya Upanga mjini Dar es Salaam, umri wake ni miaka 11 na mwaka huu ameingia darasa la sita.
Binti huyo mwenye sura yenye mvuto hakushinikizwa na mtu yeyote kujitosa kwenye fani hiyo. Amekuwa akiipenda na mara nyingi alikuwa akimsumbua mama yake, akimtaka ampatie nafasi hiyo kwenye kituo chochote cha televisheni.
Ndoto za Jennifer zilianza kutimia baada ya anti yake, Maya Mrisho kumpeleka kwa Kanumba kwa ajili ya majaribio na hatimaye akafanikiwa kupata nafasi ya kucheza filamu zake mbili. Wakati huo Kanumba alikuwa ametoa tangazo la kutafuta watoto 40 wenye vipaji kwa ajili ya kuwafanyia usaili.
Jennifer anaamini kuwa, alipata nafasi hiyo kwa sababu ana uwezo mkubwa wa uigizaji ndio sababu aliweza kushika vyema mafunzo waliyopewa na Kanumba.
Binti huyo anasema alipopewa nafasi ya kuigiza kama mtoto mshirikina, hakuogopa kwa sababu anafahamu huo ni uigizaji tu, na yeye si mshirikina.
Anamshukuru Kanumba kuwa ndiye aliyemsaidia na kumwezesha kuubeba uhalisia wa nafasi aliyotakiwa kuigiza kutokana na mafunzo aliyompatia.
Jennifer anaamini kuwa, yeye ni mtoto wa kawaida popote anapokuwa, japokuwa wapo baadhi ya watoto wenzake, ambao huwa wakimshangaa.
“Kila ninapopita mitaani, watoto wengi hupenda kuniita kwa jina la Jennifer! Jennifer!” Anasema binti huyo, ambaye nyota yake imeanza kung’ara vyema katika fani ya filamu.
Kwa sasa, Jennifer amekuwa mwigizaji maarufu nchini kutokana na kucheza filamu hizo mbili, lakini anaamini hilo haliwezi kumwathiri katika masomo yake. Amesisitiza kuwa, maendeleo yake kimasomo hadi sasa ni mazuri.
Ndoto za Jennifer si kuishia kwenye fani ya uigizaji pekee kwani angependa kujihusisha na taaluma nyingine, ambayo bado hawezi kuiweka wazi kwa sasa.
Jennifer anapenda watoto wenzake wote nao wapate nafasi ya kusoma kwa ajili ya maendeleo na maisha yao ya baadaye na kusisitiza kuwa, asiyependa kwenda shule, hawezi kuwa rafiki yake.
Pia amewataka wazazi kutowakataza watoto wao kuonyesha vipaji vyao kwa vile vinaweza kuwanufaisha katika maisha yao ya baadaye badala ya kutegemea elimu ya darasani pekee.
Kwa upande wake, mama wa Jennifer amekiri kuwa, kipaji cha uigizaji amezaliwa nacho na kuongeza kuwa, kimechangiwa na baba yake mzazi, ambaye naye ni mpenzi wa fani hiyo.
Rose haamini kuona binti yake huyo kwa sasa ni muigizaji bora chipukizi na ameweza kuibuka na tuzo ya ZIFF. Anasema kutoamini kwake huko ndiko kulikomfanya atokwe na machozi siku Jennifer alipopabidhiwa tuzo hiyo.
Mama huyo wa Jennifer anasema kama si mzazi mwenzake Daudi, huenda binti huyo asingekuwepo duniani hivi sasa kwa sababu alipata uja uzito wake akiwa shuleni na kutokana na woga na kufukuzwa nyumbani na wazazi wake, alitaka kuuharibu.
“Lakini tazama, leo hii mtoto wangu amekuwa mwigizaji maarufu na kushinda tuzo,”alisema Rose.
Kwa sasa, Rose na Daudi hawaishi pamoja, lakini wote wawili wanapenda kuwa karibu na binti yao huyo na wamepania kuhakikisha anapata mafanikio kimaisha.

No comments:

Post a Comment