KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, January 27, 2011

TINO: Filamu ya Shoga itatikisa


MTUNZI na mwigizaji mkuu wa filamu inayozungumzia tabia na vitendo vya ushoga, Hisani Muya amesema tayari kazi ya kuitayarisha imeshakamilika na inatarajiwa kuingizwa sokoni wakati wowote.
Muya, maarufu zaidi kwa jina la Tino alisema wiki hii mjini Dar es Salaam kuwa, filamu hiyo ilichelewa kuingizwa sokoni kutokana na kazi ya kuihariri kufanywa kwa umakini zaidi.
Tino alisema, awali filamu hiyo ilipewa jina la Painfull, lakini wameamua kulibadili, ambapo sasa itajulikana kwa jina la Shoga.
Mwigizaji huyo mwenye mvuto alisema kwa sasa yupo kwenye maandalizi ya mwisho kwa ajili ya uzinduzi wa filamu hiyo, ambao alitamba kuwa utakuwa wa aina yake.
Alisema ameamua kuandaa uzinduzi wa filamu hiyo kwa lengo la kuitangaza zaidi ili ujumbe wake uweze kuifikia jamii kiurahisi.
“Ni kweli tangu nilipoingia kwenye gemu, sijawahi kufanya uzinduzi wa filamu, lakini kumbuka mambo yanakwenda yakibadilika kila siku na tunataka kuwa kama wenzetu waliotangulia,” alisema.
Akifafanua kuhusu uamuzi wake wa kucheza filamu hiyo kama shoga, Tino alisema haoni kama kuna tatizo kwa vile hiyo si tabia yake bali amejaribi kuvaa uhusika huo kwa lengo la kufikisha ujumbe kwa jamii.
Alisema filamu hiyo ni tofauti sana na zingine alizowahi kuzitayarisha kutokana na maudhui na ujumbe wake ndio sababu imezua utata kwa jamii inayomzunguka na watu wake wa karibu.
“Utata ninaouzungumzia hapa ni kama lilivyo jina lenyewe. Kwa mara ya kwanza Tino aliyezoeleka katika filamu za mapenzi anaigiza kama shoga badala ya filamu za malavidavi,”alisema mcheza filamu huyo huku akitabasamu.
Tino alisema hastushwi na hisia zilizoanza kujengeka kwa baadhi ya watu wanaodhani yeye ni shoga kwa sababu msanii anaweza kucheza nafasi yoyote anayopangwa.
“Wengi tayari wameshaanza kuhisi hii ni tabia yangu, lakini ukweli hii ni sanaa tu, haina maana kwamba ukiigiza kama shoga basi hiyo ndiyo tabia yako. Kwangu mimi hii si changamoto tu bali ni matatizo,”alisema.
Kijana huyo mtanashati alisema haoni iwapo filamu hiyo itamletea matatizo kwa waumini wenzake wa dini ya kiislamu kwa sababu alichokifanya ni kukemea tabi hiyo.
Alisema dini zote mbili, ya kiislamu na kikristo haziruhusu vitendo hivyo na kwamba katika filamu hiyo amejaribu kukemea tabia hiyo na kuonyesha madhara yake. Tino alisema haamini iwapo filamu yake hiyo inaweza kuchochea na kuhalalisha vitendo vya kishoga hadharani ama kuwakera viongozi wa dini hizo mbili kubwa nchini.
“Katika filamu hii, mimi nimeonyesha athari za ushoga, kwa ujumla ni kwamba shoga huyo katika filamu yangu anapata maambukizi ya ukimwi, lakini vilevile mkewe baada ya kugundua, anaamua kumuua kwa hiyo kupitia filamu hii, tumeona madhara ya ushoga,”alisema.
Kwa mujibu wa Tino, uzinduzi wa filamu hiyo umepangwa kufanyika Februari 4, 2011 katika ukumbi wa Travertine uliopo Magomeni, Dar es Salaam. Alisema uzinduzi huo utapambwa kwa burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali, likiwemo kundi la Mapacha Watatu.
Tino ameitaka jamii kuwa makini na vitendo vya ushoga kwa sababu vipo, lakini baadhi ya watu wanavifumbia macho na hawatakiKuvizungumza kwa kuvionea aibu.

No comments:

Post a Comment