KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, January 27, 2011

SKENDO LA PAPIC


WAKATI hali ikiwa si shwari ndani ya klabu ya Yanga, imebainika kuwa, wachezaji wengi wa timu hiyo hawana mikataba inayoeleweka kutokana na kuchakachuliwa na baadhi ya viongozi.
Habari za uhakika kutoka ndani ya Yanga zimeeleza kuwa, wachezaji pekee wenye mikataba ya uhakika hawazidi watano na kuongeza kuwa, wengine mikataba yao ni hewa.
Kwa mujibu wa habari hizo, kufuatia kubainika kwa uchakachuaji huo, mfadhili mkuu wa Yanga, Yusuf Manji ameuagiza uongozi wa klabu hiyo kukusanya mikataba yote ya wachezaji kwa ajili ya kuhakikiwa.
Uamuzi wa Manji kukusanya mikataba hiyo umekuja siku chache baada ya kukutana na wachezaji wote wa timu hiyo katika kikao kilichofanyika Jumatatu iliyopita, makao makuu ya klabu hiyo mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam. Manji alikutana na wachezaji hao kwa lengo la kusikiliza madai yao ya pesa za usajili na malipo mengine kulingana na mikataba yao. Aliutaka uongozi uwe umemaliza kazi ya kukusanya mikataba hiyo jana.
Katika kikao hicho, baadhi ya wachezaji walimweleza Manji kuwa, hawajalipwa pesa zao za usajili, kauli iliyomshtua mfadhili huyo kwa vile alishawapatia viongozi fedha zote.
Wachezaji wengine walimweleza mfadhili huyo kuwa, wamekuwa wakilazimika kuwalipa baadhi ya viongozi sehemu ya malipo yao kama fadhila kutokana na kufanikisha usajili wao.
Mbali na hilo, wachezaji wengine walimweleza Manji kuwa, wamekuwa wakiishi kwa hofu kutokana na baadhi ya viongozi kujenga chuki dhidi yao kwa kukataa kuwapa chochote.
Miongoni mwa wachezaji wanaodaiwa kuonja machungu ya viongozi hao ni pamoja na viungo Athumani Idd 'Chuji' na Ernest Boakye, ambaye aliwahi kutimuliwa katika kambi huko Tanga baada ya kudai anaumwa tumbo.
Wachezaji wengine, ambao pia inadaiwa wamekumbana na adha hiyo ni Mohamed Mbegu, ambaye naye aliwahi kusimamishwa kwa muda kwa tuhuma za utovu wa nidhamu. Wengine ni Fred Mbuna na Chacha Marwa, ambao wamekuwa hawapati namba kwenye kikosi cha kwanza cha timu hiyo.
Uchunguzi wa Burudani umebaini kuwa, baadhi ya viongozi wa Yanga walikuwa wakiingia mikataba kinyemela na wachezaji wa timu hiyo na kuwaandikia kiasi kikubwa cha malipo, lakini fedha walizokuwa wakiwapatia zilikuwa kiduchu.
Chanzo cha habari kutoka ndani ya Yanga kimeeleza kuwa, kufuatia Manji kubaini kuwepo kwa mikataba hewa ya wachezaji, baadhi ya watendaji wakuu wa klabu hiyo wameamua kujiuzulu.
Miongoni mwa viongozi waliojiuzulu ni Katibu Mkuu, Lawrence Mwalusako, Meneja wa timu, Emmanuel Mpangala na Kocha Mkuu, Kostadin Papic.
Alipoulizwa jana kuhusu tuhuma za matumizi mabaya ya pesa na uchakachuaji wa mikataba ya wachezaji, Mwenyekiti wa Yanga, Llyod Nchunga alisema wameshaanza kufanya uchunguzi, ambao ndio utakaobaini iwapo ni kweli au la.
Nchunga alisema ukaguzi wa hesabu ndio utakotoa majibu iwapo viongozi waliojiuzulu wanahusika na tuhuma hizo ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yao.
Hata hivyo, Nchunga alimtetea Mwalusako kwa kusema hahusiki na tuhuma hizo na kusisitiza kuwa, kujiuzulu kwake kumetokana na matatizo ya kiafya kama taarifa yake kwa vyombo vya habari ilivyoeleza.
Kuhusu Papic, Nchunga alisema kocha huyo ameamua kujiuzulu baada ya kukataa kufanya kazi na Fred Minziro, ambaye ameteuliwa kuwa kocha msaidizi wa timu hiyo.
“Kwa vile hakutaka kufanyakazi na msaidizi wake, hakukuwa na sababu ya yeye (Papic), kubaki kwa sababu Yanga si ya mtu mmoja na ni lazima benchi la ufundi kama linamahitaji, lifanyiwe kazi,”alisema.
Kwa upande wake, Mwalusako alisisitiza kuwa, sababu alizozitoa kuhusu uamuzi wake wa kujiuzulu ni sahihi na hazina shaka na kuongeza kuwa, yupo tayari kuchunguzwa. Mpangala hakuweza kupatikana.

No comments:

Post a Comment