KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, January 27, 2011

MWALUSAKO: Kuongoza Yanga matatizo



SWALI: Pole na matatizo ya kuumwa. Hivi ni kweli kwamba hiyo ndiyo sababu hasa iliyokufanya uamue kujiuzulu uongozi wa Yanga?
JIBU: Ukweli ni kwamba mimi ninaumwa. Nimekuwa nikisumbuliwa kwa muda mrefu la tatizo la moyo, ugonjwa ambao nimegundua unaweza kufupisha maisha yangu.
Tatizo hilo limetokana na kutumia kwangu muda mwingi kufanyakazi bila ya kupumzika, hali ambayo wakati mwingine imekuwa ikiniweka kwenye wakati mgumu.
Unajua ukiwa kiongozi wa klabu kubwa kama Yanga, hasa katika nafasi ya utendaji niliyokuwa nikiitumikia mimi, unakuwa ukipigiwa simu mara kwa mara za kutakiwa kutatua tatizo hili na lile. Hali hii ilikuwa ikisababisha wakati mwingine napitisha hata muda wa kunywa dawa zangu nah ii ni hatari.
Licha ya tatizo hilo, nilijitahidi kufanyakazi zangu kwa ufanisi, lakini wapo baadhi ya wanachama au watu binafsi waliokuwa wakiniona sifanyi lolote.
SWALI: Kwanini unasema hivyo? Au kuna shinikizo umelipata kutoka kwa mfadhili mkuu wa Yanga, Yusuf Manji?
JIBU: Hapana, Manji hajanipa shiniko lolote kuhusu kujizulu, isipokuwa nimeamua kukaa pembeni ili niweze kujiuguza.
Pamoja na hilo, bado nina kila sababu ya kukaa pembeni kwani nimegundua wapo watu walikuwa wananiandama kwa sababu mbalimbali.
Pale Yanga wapo baadhi ya wanachama wakitaka jambo lao, ambalo pengine linahitaji maamuzi ya pamoja, na ukimweleza mtu asubiri na kisha likakataliwa, tayari mtu huyo atakuchukia.
Lakini ukweli ni kwamba yapo mambo mengi, ambayo kwa asilimia kubwa yamechangia mimi kufikia uamuzi huu ili kukwepa kujiumiza.
SWALI: Tangu ulipoteuliwa kuwa katibu mkuu wa Yanga, nini hasa kilitokea kukukera na pengine kuchangia kwa kiasi kikubwa wewe kujiuzulu katika wadhifa huo mbali ya ugonjwa?
JIBU: Kwa kweli nimekuwa nikichukizwa na baadhi ya watu, ambao wanaeneza chokochoko ndani ya Yanga. Watu hawa wamekuwa wakichonganisha watu, hasa viongozi na kufikia hatua ya kuigawa klabu kitu, ambacho ni kibaya.
Pia nimekuwa nikikerwa sana na tabia ya uzushi wa mambo na wakati mwingine watu kufikia hatua ya kuchafuana.
Wapo baadhi ya watu au wanachama walioeneza uvumi kwamba mimi na viongozi wenzangu tumekula pesa nyingi za Yanga kitu, ambacho si kweli kwani mambo yote yapo wazi.
SWALI: Je, upo tayari kushirikiana na wakaguzi wa hesabu ili kuchunguza mapato na matumizi ya klabu ya Yanga kwa kipindi chote cha uongozi wako?
JIBU: Nipo tayari kushirikiana na watu hao ili niweze kuweka wazi mambo kwani tabia ya kuchafuana si nzuri na jambo hilo ni miongoni mwa mambo yaliyosababisha nijiondoe ndani ya uongozi wa Yanga. SWALI: Mwishoni mwa wiki hii Yanga itacheza na timu ya Dedebit ya Ethiopia katika mechi ya awali ya michuano ya Kombe la Shirikisho. Je, huoni kama kujiuzulu kwako kunaweza kuwachanganya wachezaji kwa kukosa huduma yako?
JIBU: Sidhani kama hilo linaweza kutokea. Wapo watendaji wengine, ambao naamini watafanyakazi zangu kwa ufanisi. Lakini binafsi nitaendelea kushirikiana na uongozi kwa vile mimi ni mwanachama wa Yanga.
Lakini nitafanya hivyo kama afya yangu itaniruhusu kwenda kufanya kazi za klabu iwapo nitahitajika. Kikubwa nawaomba wachezaji wa Yanga wajitume zaidi ili kuhakikisha wanashinda mchezo huo.
Pia nawaomba viongozi, wanachama na wapenzi wa Yanga tuwaunge mkono wachezaji wetu kwa kuwashangilia kwa nguvu ili waweze kushinda mchezo huo.
SWALI: Hivi sasa umeshajiondoa katika uongozi wa klabu ya Yanga, nini matarajio yako kwa siku zijazo?
JIBU: Natarajia kuendelea na kazi yangu niliyokuwa nikiifanya kabla ya kujiunga na Yanga huku nikiangalia afya yangu kwa ukaribu zaidi ili niweze kupona kabisa.
Naamini naweza kurejea kazini siku zijazo kwa ajili ya kujitafutia riziki, lakini nitaendelea kuwepo Yanga na milango ipo wazi wakati wowote kwa viongozi iwapo watanihitaji kuwapa ushirikiano kama hali yangu itakuwa nzuri kiafya.

No comments:

Post a Comment