KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, January 19, 2011

Yanga ubabe mtupu



HAKUNA kinachoeleweka! Ndivyo unavyoweza kuuelezea mgogoro uliozuka sasa kati ya uongozi wa klabu ya Yanga na viongozi wa matawi ya klabu hiyo ya mjini Dar es Salaam.
Wakati viongozi wa matawi wameitisha mkutano leo kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali yanayoihusu Yanga, Mwenyekiti wa klabu hiyo, Llyod Nchunga ametangaza kutoutambua na kuupiga marufuku.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari juzi, Nchunga alisema ameupiga marufuku mkutano huo kwa sababu unaweza kuchafua hali ya hewa ndani ya Yanga.
Lakini Mwenyekiti wa matawi ya klabu hiyo, Mohamed Msumi aliwaambia waandishi wa habari mjini Dar es Salaam jana kuwa, lazima mkutano huo ufanyike kama ulivyopangwa.
Nchunga alisema mkutano huo hauna madhara kwa uongozi kwa vile lengo lao ni kujadili matatizo yaliyopo ndani ya Yanga na kuyatafutia ufumbuzi.
Alizitaja ajenda zinazotarajiwa kujadiliwa kwenye mkutano huo kuwa ni hali ya kutokuelewana kati ya Nchunga na makamu wake, Davis Mosha pamoja na uteuzi wa Mbunge wa Temekem, Abbas Mtemvu (CCM), kuwa mdhamini wa klabu.
Ajenda nyingine ni matumizi ya sh. milioni 200 zilizotolewa na mfadhili mkuu wa klabu hiyo, Yusuf Manji kwa ajili ya usajili wa wachezaji Davis Mwape na Juma Sefu wakati wa usajili wa dirisha dogo.
Msumi alisema mkutano huo ni haki ya wanachama na hauna lengo la kuupinga uongozi uliopo madarakani, hivyo Nchunga hapaswi kuuhofia kwa sababu lengo lao ni kuweka mambo sawa.
Mgogoro kati ya uongozi na wanachama ulizuka siku chache baada ya Yanga kuchapwa mabao 2-0 na Simba katika mechi ya fainali ya michuano ya Kombe la Mapinduzi, iliyochezwa wiki iliyopita kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
Mapema jana asubuhi, mfadhili mkuu wa klabu hiyo, Yusuf Manji aliwaita wazee wa klabu hiyo ofisini kwake barabara ya Nyerere, Dar es Salaam kwa ajili ya kuteta nao ili kuweka mambo sawa.
Haikuweza kufahamika mara moja kilichojadiliwa katika kikao hicho, lakini kuna habari kuwa, Manji amewasihi wazee hao watulize mzuka ili kuepuka kuiingiza klabu kwenye mgogoro mpya.

No comments:

Post a Comment