KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, January 14, 2011

Babi atema cheche Vietnam


KIUNGO wa zamani wa klabu ya Yanga, anayecheza soka ya kulipwa klabu ya Dong An ya Vietnam, Abdi Kassim 'Babi' amesema ameanza mazoezi rasmi na kikosi hicho kwa ajili ya kujiandaa na mechi za ligi.
Akizungumza kwa njia ya simu kutoka Vietnam jana, Kassim alisema amepokewa vizuri na uongozi pamoja na wachezaji wa klabu hiyo na matarajio yake ni kucheza soka ya kiwango cha juu kwa lengo la kupeperusha vyema bendera ya Tanzania kimataifa.
Nahodha huyo wa timu ya taifa ya Zanzibar, Zanzibar Heroes alisema anaamini katika wa soka, hakuna linaloshindikana iwapo mchezaji ataamua kufuata misingi ya uchezaji na kuongeza kuwa, amekwenda Vietnam kucheza mpira akiwa na matarajio ya kwenda Ulaya.
Kassim amewataka wachezaji wanaocheza soka ya ridhaa nchini, kuongeza kasi na kuweka malengo ya kucheza soka nje ya nchi. Lakini ameonya kuwa, jitihada hizo zitafanikiwa iwapo wadau wa soka, vyama vya soka na viongozi wa klabu watakuwa mstari wa mbele kutaka kuinua kiwango cha mchezo huo.
"Kwa ufupi nimeshaanza kuzoea maisha mapya. Kama unavyofahamu, nipo ugenini. Napenda kutoa changamoto kwa wachezaji wenzangu niliowaacha nyumbani, kucheza kwa bidii na malengo yao yawe kucheza soka ya kulipwa nje," alisema mchezaji huyo.
Kiungo huyo anayetumia zaidi mguu wa kushoto, alisema anashukuru ameondoka akiwa na baraka za viongozi wa klabu ya Yanga, ambayo aliitumikia kwa moyo wote tangu alipojiunga nayo akitokea Mtibwa Sugar. Kassim alikuwa nahodha msaidizi wa Yanga akimsaidia Fredi Mbuna.
Klabu ya Don An, ilimsajili Kassim kwa kitita cha dola 40,000 (sh. milioni 60). Mbali ya kuitumikia Zanzibar, kiungo huyo alikuwa mchezaji wa timu ya taifa, Taifa Stars. Alijiunga na Mtibwa mwaka 2003 kabla ya kutua Yanga msimu wa 2006.

No comments:

Post a Comment