KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, January 14, 2011

Poulsen yaleyale ya Maximo


Na Mwandishi Maalum, Cairo
KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Taifa, Taifa Stars, Jan Poulsen amewapoza Watanzania kwa kuwataka wasikate tamaa licha ya timu yao kushindwa kufuzu kucheza nusu fainali ya michuano ya Kombe la Mto Nile.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Poulsen alisema Taifa Stars ni timu nzuri, isipokuwa wachezaji wake wanakosa umakini katika baadhi ya mechi.
Kauli hiyo ya Poulsen imekuja baada ya Taifa Stars kulazimishwa kutoka sare ya bao 1-1 na Uganda katika mechi yake ya mwisho iliyochezwa juzi kwenye uwanja wa Polisi mjini hapa.
Kufuatia kipigo hicho, Taifa Stars sasa inawania nafasi ya tano kwa kutegemea matokeo ya mechi ya mwisho kati ya Burundi na Misri itakayochezwa kesho.
Poulsen alisema kimchezo, Taifa Stars inacheza vizuri, lakini makosa madogo ya kiufundi ndiyo, ambayo yamekuwa yakiigharimu katika baadhi ya mechi na kusisitiza kuwa, ipo haja ya kulifanyiakazi tatizo hilo.
"Nimesikitishwa sana kushindwa kufuzu kucheza nusu fainali, lakini ndiyo soka ilivyo na jirani zetu Uganda na Kenya wao wameingia hatua hiyo, huo ndiyo mchezo ulivyo," alisea kocha huyo raia wa Denmark.
Kocha huyo alisema tatizo kubwa la Taifa Stars lipo kwenye safu yake ya ulinzi kujichanganya na ile ya ushambuliaji kushindwa kuzitumia vyema nafasi inazopata kufunga mabao.
Amewataka watanzania wasikatishwe tamaa na matokeo hayo kwa vile bado yupo kwenye mikakati ya kujenga kikosi imara kwa ajili ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Mataifa ya Afrika za mwaka 2012.
Nahodha wa timu hiyo, Shadrack Nsajigwa alisema wamefedheheshwa na matokeo hayo, lakini katika soka kuna kushinda, kufungwa ama kutoka sare.
Katika mechi yake ya kwanza, Taifa Stars ilinyukwa mabao 5-1 na wenyeji Misri kabla ya kutoka sare ya bao 1-1 na Burundi. Stars inatarajiwa kumenyana na Sudan kesho katika mechi ya kutafuta mshindi wa tano.
Mechi za nusu fainali pia zinatarajiwa kuchezwa kesho, ambapo Misri itamenyana na Kenya wakati Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo itavaana na Uganda.

No comments:

Post a Comment