KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, January 19, 2011

Papic: Nipo tayari kwa lolote


KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Yanga, Kostadin Papic amesema yupo tayari kwa lolote, kufuatia timu hiyo kufanya vibaya katika michuano mbalimbali.
Akizungumza mjini Dar es Salaam juzi, Papic alisema kufanya vibaya kwa Yanga katika mechi mbalimbali kumechangiwa na sababu zilizo nje ya uwezo wake.
Kauli hiyo ya Papic ilikuja saa chache baada ya Yanga kuchapwa mabao 3-2 na Atletico Paranaense ya Brazil katika mechi ya kirafiki ya kimataifa, iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Alizitaja baadhi ya sababu hizo kuwa ni pamoja na mwingiliano wa mashindano mbalimbali, unaotokana na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kutokuwa na kalenda ya uhakika.
"Hebu fikiri, Yanga inashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho,tumepanga programu zetu, mara yanazuka mashindano ya Kombe la Mto Nile, wachezaji wangu muhimu wanakwenda Misri,"alisema kocha huyo kutoka Serbia.
Alisema mwingiliano huo wa mashindano umesababisha programu yake ya mazoezi kuvurugika na mambo mengi kwenda kinyume na alivyoyapanga.
Papic pia aliushutumu uongozi wa Yanga kwa kushindwa kukamilisha uhamisho wa mchezaji Kenneth Asamoah, kitendo ambacho alidai kuwa kimemkera na kumvurugia mipango yake.
Mserbia huyo alikwenda mbali zaidi kwa kusema, baadhi ya wakati amekuwa akishindwa kutekeleza majukumu yake kutokana na wachezaji wengi pamoja na yeye binafsi kushindwa kulipwa haki zao kwa wakati mwafaka.
Kocha huyo, aliyelipwa mshahara wake wa mwezi uliopita mwanzoni mwa wiki hii alisema, kasoro hizo zimechangia kuwafanya wachezaji wacheze chini ya kiwango na timu kuvurunda.
“kutokana na sababu hizo na zinginezo, nipo tayari kwa lolote kutokana na timu kufanya vibaya,”alisema.
Papic pia alisema hana taarifa kuhusu kuteuliwa kwa Fred Felix Minziro kuwa msaidizi wake, lakini alisisitiza, yupo tayari kufanyanaye kazi pamoja.

No comments:

Post a Comment