KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, January 19, 2011

SIMBA HAOOO BRAZIL

MABINGWA wa soka wa Tanzania Bara, Simba wamepewa ahadi ya kukwea pipa kwenda Brazil iwapo wataishinda Atletico Paranaense ya nchini humo.
Simba na Atletico, inayoundwa na wachezaji wengi wadogo kiumri, zinatarajiwa kumenyana leo katika mechi ya kirafiki ya kimataifa, itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mwenyeji wa Wabrazil hao, Fatma Al-Kharoos aliwaambia waandishi wa habari juzi kuwa, ataipeleka Simba nchini Brazil kwa ajili ya mechi ya marudiano kati ya timu hizo mbili iwapo tu itashinda leo.
Katika mechi yake ya kwanza iliyochezwa juzi kwenye uwanja huo, Atletico iliichapa Yanga mabao 3-2.
“Napenda kuiona Simba ikiifunga na Atletico na iwapo itafanya hivyo, nitaipeleka Brazil kwa ajili ya mchezo wa marudiano,”alisema Rahma.
Mwanamama huyo pia amewapa ofa mashabiki wa soka wa Dar es Salaam kushuhudia mechi hiyo bure ili waweze kupata uhondo kutoka kwa timu hizo mbili.
Katika mechi hiyo, Simba itamkosa mshambuliaji wake nyota, Emmanuel Okwi, ambaye amerejea kwao Uganda kwa ajili ya kupatiwa matibabu ya mguu.
Okwi aliumia wakati Simba ilipomenyana na Ocean View katika mechi ya nusu fainali ya Kombe la Mapinduzi, iliyochezwa wiki iliyopita mjini Zanzibar.
Hata hivyo, Simba huenda ikawachezesha wachezaji Juma Kaseja, Juma Nyoso, Kelvin Yondani, Jabir Azizi na Abdalla Shiboli waliokuwa na kikosi cha Taifa Stars nchini Misri. Timu hiyo ilirejea nchini juzi usiku.
Mchezo huo ni wa pili wa kimataifa kwa Simba ndani ya wiki moja. Mwishoni mwa wiki iliyopita, Simba ilichapwa mabao 2-1 na ZESCO ya Zambia katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru.

No comments:

Post a Comment