KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, January 27, 2011

Z'bar kupata uanachama FIFA 2012

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) imesema Zanzibar itakuwa mwanachama kamili wa Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) ifikapo mwaka 2012.
Hayo yalisemwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Abdillahi Jihadi Hassan wakati akijibu swali na nyongeza la Mwakilishi wa Kiwani, Hijja Hassan Hijja aliyetaka kujua mchakato wa Zanzibar kuwa mwanachama wa FIFA utakamilika lini. Jihadi alisema mchakato huo unakwenda vizuri na tayari FIFA imeshaanza kuonyesha dalili za kuikubalia Zanzibar kuwa mwanachama.
Alisema mchakato huo unatarajiwa kukamilika rasmi ifikapo mwaka 2012 wakati wa mkutano mkuu wa FIFA, unaotarajiwa kufanyika mjini Zurich, Uswisi. “Nataka kuwaambia wajumbe kwamba, yapo matumaini makubwa ya Zanzibar kukubaliwa kuwa mwanachama wa (FIFA). Mchakato huu unakwenda vizuri na mkutano wa mwaka 2012 ndio utakaotoa idhini ya maombi yetu,”alisema. Zanzibar imekuwa katika mikakati na juhudi za kuomba uanachama wa FIFA tangu mwaka 2002, ambapo Serikali ya Jamhuri ya Muungano imetoa baraka zote. Katika kutoa baraka hizo, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limekuwa likikisaidia Chama cha Soka cha Zanzibar (ZFA) kwa hali na mali ili kiweze kupata uanachama huo.
Zanzibar inataka kuwa mwanachama wa FIFA ili iweze kufaidika na misaada mbalimbali inayotolewa na shirikisho hilo, ikiwemo ya fedha na kiufundi na pia kupatiwa wataalamu wa kukuza mchezo wa soka.

No comments:

Post a Comment