KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, January 19, 2011

Aki, Ukwa sasa kutengeneza filamu zao


LAGOS, Nigeria
BAADA ya kutamba kwa miaka mingi katika fani ya uigizaji filamu, Osita Iheme (Aki) na Chinedu Ikedieze (Ukwa) wameamua kutayarisha filamu zao wenyewe.
Aki na Ukwa walielezea mikakati yao hiyo wiki hii katika mahojiano maalum na mtandao wa Nigeria Films.
Mbali na kutengeneza filamu zao wenyewe, waigizaji hao wafupi na wenye vichekesho vya kuvunja mbavu, pia walikanusha madai kuwa hawaelewani na wana mpango wa kutengana.
Aki alisema si kweli kwamba wameamua kila mmoja kufanyakazi kivyake ndio sababu wameamua kushirikiana na kuandaa filamu zao wenyewe.
Kwa mujibu wa Aki, hawana haraka katika kuandaa filamu zao, lakini wanatarajia kuanza mpango huo mwaka huu. Alisema wataandaa filamu hizo kupitia kampuni yao ya APEN- (Aki and Pawpaw Entertainment Nigeria).
Naye Ukwa alisisitiza kuwa, bado wapo pamoja na anaamini vitu vyao vitaanza kuonekana hivi karibuni. Alisema kilichopangwa na Mungu hakuna anayeweza kukipangua.
“Sisi tumeunganishwa na Mungu,”alisema Ukwa na kudokeza kuwa, wanavyo pia vipaji vya uimbaji, lakini hakutaka kuzungumzia zaidi suala hilo.
Waliwataja waigizaji wenzao wanaowavutia na kufurahia kufanyanao kazi pamoja kuwa ni Rita Dominic, Nkem Owoh, John Okafor, Ini Edo, Sam Loco-Efe na Genevieve Nnaji.

No comments:

Post a Comment