KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, January 19, 2011

Jordan atengana rasmi na mumewe


LONDON, England
BAADA ya kuwepo kwa wiki kadhaa za tetesi na uvumi, hatimaye mwigizaji na mwanamitindo nyota wa Uingereza, Katie Price ‘Jordan’ ametangaza kutengana na mumewe Alex Reid.
Jordan (32) ametangaza kutengana na mumewe miezi 11 tangu walipofunga ndoa na kuishi kama mume na mke.
Mama huyo wa watoto watatu alitoa taarifa hiyo juzi jioni baada ya Reid (35) kupigwa picha akionekana anahama kutoka nyumbani kwao eneo la Surrey na kurejea kwa wazazi wake eneo la Hampshire.
Jordan alikiri kuwa, ndoa yao ilikumbwa na matatizo mengi katika miezi michache iliyopita, ikiwa ni pamoja na msuguano kati yake na Reid kuhusu kuzaa naye mtoto. Kutengana kwa wanandoa hao kumekuja wiki chache baada ya kuvinjari kwa siri kwenye kisiwa kimoja kilichopo bahari ya Hindi kwa ajili ya mapumziko.
Mara baada ya kurejea England, Jordan aliwaeleza wasomaji wa mtandao wake kuwa, taarifa kuhusu ndoa yake kukumbwa na matatizo zilikuwa za kweli.
Katika taarifa yake, Jordan alimshutumu mumewe kwa kuwa na mabadiliko makubwa tofauti na alivyokuwa wakati alipojitosa kimapenzi kwake.
Jordan na Reid walianza kuwa na uhusiano wa kimapenzi Julai, 2009, ikiwa ni wiki nane baada ya mwanamama huyo kutengana na mumewe wa kwanza, Peter Andre. Wakati huo, Reid alikuwa mmoja wa waigizaji nyota wa filamu.
Kwa mujibu wa Jordan, walipanga kutoa taarifa ya pamoja kuhusu kutengana kwao mwishoni mwa wiki iliyopita, lakini alilazimika kusubiri baada ya kushawishiwa na mumewe, aliyetaka apewe muda wa kufikiria.
Lakini baada ya Reid kupigwa picha akiwa anamfundisha mtoto wa Jordan kupigana kwenye gym, mwanamama huyo aliamua kubadili mawazo.
Jordan amemshutumu Reid kwa kuvitumia vyombo vya habari kupata umaarufu kwa kumpiga picha kadhaa akiwa na mtoto wake Junior na pia kuchapisha habari kuhusu ndoa yao.
Alisema Reid anafahamu wazi kwamba hakuwa akitaka habari zinazohusu watoto wake zichapishwe hadharani kwa vile wanaweza kuathirika kisaikolojia.
Kwa upande wake, Reid alisema amekuwa akimuunga mkono Jordan katika uamuzi wake wa kuwaepusha wanawe na mapaparazi, lakini alishangaa kuona picha yake akiwa na Jordan imeuzwa kwenye chombo kimoja cha habari.
Alisisitiza kuwa, bado ataendelea kuvaa pete ya harusi kati yake na Jordan na pia kuipigania ndoa yake. Wanandoa hao walikutana kwa mara ya kwanza kwenye sherehe ya mwanamuziki Michelle Heaton kutimiza miaka 30 iliyofanyika Julai 19, 2009 kabla ya kufunga ndoa mwaka uliofuata.

No comments:

Post a Comment