KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, January 19, 2011

Msimbazi wamnasa Mcameroon


KLABU ya Simba imefanikiwa kukinasa kifaa kipya kutoka Cameroon, ambacho itakitumia katika mashindano ya soka ya klabu bingwa Afrika yanayotarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi huu.
Habari kutoka ndani ya Simba zimemtaja mchezaji huyo kuwa ni Cosmas Ekeh, anayecheza nafasi ya kiungo na ushambuliaji kutoka klabu ya Metro Security, inayocheza ligi daraja la kwanza nchini humo.
Kwa mujibu wa habari hizo, Ekeh alitua nchini mwishoni mwa wiki iliyopita na kupewa mkataba mnono, lakini uongozi wa Simba umekataa kuuweka hadharani.
Akizungumzia ujio wa mchezaji huyo, Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Phiri alisema amefurahi kupata mchezaji mwenye sifa zinazokubalika ndani na nje ya uwanja.
Phiri alisema kwa kipindi alichokaa na mchezaji huyo, amebaini kuwa, kiwango chake kipo juu na anaweza kuisaidia timu yake katika michuano hiyo.
Kocha huyo kutoka Zambia alisema, iwapo Ekeh atafanya vizuri katika michuano hiyo, huenda akasajiliwa na Simba katika msimu ujao wa ligi kuu ya Tanzania Bara.
Ekeh anatarajiwa kuanza kuonyesha cheche zake leo wakati Simba itakapomenyana na Atletico Paranaense ya Brazil katika mechi ya kirafiki ya kimataifa, itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Naye Ekeh alisema amekuja nchini kucheza soka na kuisaidia Simba ili iweze kufanya vizuri katika mashindano hayo makubwa ya ngazi ya klabu barani Afrika.
Ekeh alisema tayari ameshatia saini mkataba wa kuichezea timu hiyo, lakini hakuwa tayari kuuweka wazi kwa madai kuwa, hiyo ni siri yake na uongozi wa klabu.
Simba inatarajiwa kukata utepe wa michuano ya Afrika kwa kumenyana na Elam ya Comoro. Iwapo itashinda, itakutana na TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo katika raundi ya kwanza.

No comments:

Post a Comment