KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, January 14, 2011

Ndlovu kuishtaki Yanga CAF

BEKI wa zamani wa Yanga, Wisdom Ndlovu amesema atawasilisha malalamiko yake kwa Shirikisho la Soka Afrika (CAF) ili kuishinikiza klabu hiyo imlipe haki zake.
Akizungumza kwa njia ya simu kutoka Malawi jana, Ndlovu alisema hakubaliani na uamuzi wa Kamati ya Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF ya kuishinikiza Yanga imlipe haki zake mchezaji Ally Msigwa pekee.
Ndlovu, Msigwa, John Njoroge pamoja na kipa Steven Marashi ni miongoni mwa wachezaji wanne waliowasilisha malalamiko yao kwa kamati hiyo wakiitaka Yanga iwalipe haki zao baada ya kukatisha mikataba yao.
Hata hivyo, TFF imeitaka Yanga imlipe Msigwa sh. milioni saba, ikiwa ni malipo ya miezi 36 yaliyokuwa yamebaki kwenye mkataba wake, lakini imetupilia mbali malalamiko ya wachezaji wengine watatu kwa madai kuwa walishindwa kuhudhuria vikao mara mbili.
Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah alisema juzi kuwa, Ndlovu, Njoroge na Marashi suala lao limeondolewa kwenye kamati hiyo kwa sababu hiyo.
Kufuatia uamuzi wa kamati hiyo, TFF imeizuia Yanga kusajili mchezaji yoyote mpya au kuuza mchezaji msimu wa 2011/2012 hadi itakapomlipa Msigwa haki zake.
“Mimi kwa sasa nipo Malawi, lakini nasikitika kusema kwamba sikuwahi kuitwa kujieleza na kamati hiyo, hivyo nitakuja Tanzania kufuatilia haki zangu,”alisema Ndlovu.
Alisema iwapo Yanga itaendelea kumpiga chenga, atawasilisha malalamiko yake CAF ili imsaidie kupata haki zake.
Naye kipa Marashi amesema hakuwahi kuitwa na kamati hiyo kwa ajili ya kujieleza na kuwasilisha vielelezo kuhusu malalamiko yake dhidi ya Yanga.
Marashi alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, hakuna kiongozi yeyote wa TFF aliyewahi kuwasiliana naye kuhusu suala hilo, hivyo hakubaliani na uamuzi wa kuyatupa malalamiko yake.
“Hadi naondoka Tanzania kwenda Botswana, sikuwahi kupigiwa simu na kiongozi yeyote wa TFF kwa ajili ya kuitwa kwenye kikao,”alisema kipa huyo. Kikao hicho kilifanyika Desemba 30 mwaka jana na Januari 7 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment