KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 21, 2012

Lulu ana miaka 18- Serikali

UPANDE wa Mashitaka katika maombi ya uchunguzi juu ya umri halali wa msanii wa filamu,
Elizabeth Michael 'Lulu' umewasilisha ushahidi mahakamani unaoonyesha kuwa msanii huyo ana umri zaidi ya miaka 18.
Ushahidi huo, uliwasilishwa juzi katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, kutokana na amri iliyotolewa na Jaji Fauz Twaib, aliyeamuru upande huo na ule wa mawakili wanaomtetea Lulu kuwasilisha ushahidi wao.
Lulu anayekabiliwa na kesi ya mauaji ya msanii mwenzake Steven Kanumba, iliyopo Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kwa kupitia mawakili wanaomtetea Kenneth Fungamtama, Peter Kibatala na Flugence Massawe, waliwasilisha maombi Mahakama Kuu kufanya uchunguzi wa umri wa mteja wao.
Hatua hiyo, inatokana na mawakili hao kudai mteja wao ana umri wa miaka 17 huku upande ule wa mashitaka ukidai ana miaka 18.
Juzi, upande wa mashitaka uliwasilisha ushahidi wao katika Mahakama Kuu wa CD ya mahojiano ya Lulu na mtangazaji Zamaradi Mketema, na maelezo yake aliyoyatoa polisi.
Pia wamewasilisha maombi ya hati ya kusafiria na leseni ya udereva ya msanii huyo.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana katika vielelezo vyote vilivyowasilishwa mahakamani hapo, inaonekana Lulu akisema ana miaka zaidi ya 17.
Juni 13, mwaka huu, mawakili wanaomtetea Lulu waliwasilisha mahakamani hapo ushahidi wao wa hati ya kiapo waapaji wakiwa baba mzazi wa Lulu, Michael Kimemeta na mama yake na Lucresia Kalugila, ambao wameapa kwamba mtoto wao hadi anatuhumiwa kufanya tendo hilo la mauaji umri wake ni miaka 18.
Maombi hayo yamepangwa kusikilizwa Juni 25, mwaka huu, baada ya pande zote kuwasilisha ushahidi wao.

No comments:

Post a Comment