KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, June 22, 2012

Yanga yavunja mkataba wa Asamoah

HATIMAYE uongozi wa klabu ya Yanga umefikia makubaliano ya kuvunja mkataba wa mshambuliaji wake wa kimataifa kutoka Ghana, Kenneth Asamoah.

Habari za uhakika kutoka ndani ya kamati ya usajili ya Yanga zimeeleza kuwa, Asamoah alikuwa bado amesaliwa na mwaka mmoja katika mkataba wake.

Kwa mujibu wa habari hizo, awali uongozi wa Yanga ulishindwa kuvunja mkataba wa Asamoah baada ya mchezaji huyo kutaka alipwe sh. milioni 30 na mshahara wa mwaka mmoja, ambapo vyote kwa pamoja vingegharimu sh. milioni 42.

Lakini baada ya mazungumzo ya kina kati ya uongozi na mchezaji huyo, amekubali kulipwa sh. milioni 20 na mshahara wa mwaka mmoja.

Asamoah anakuwa mchezaji wa pili wa kigeni mkataba wake kuvunjwa. Mwingine ni Davis Mwape wa Zambia, ambaye mkataba wake uliokuwa umalizike mwezi ujao, umevunjwa na tayari ameshalipwa chake.

Chanzo cha habari kimeeleza kuwa Asamoah huenda akalipwa fedha zaidi mwanzoni mwa wiki ijayo na kuruhusiwa kurejea kwao.

Asamoah atakumbukwa sana na mashabiki wa Yanga, kufuatia kuifungia bao la pekee na la ushindi katika mechi ya fainali ya Kombe la Kagame dhidi ya mahasimu wao Simba mwaka jana.

No comments:

Post a Comment