KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, June 10, 2012

Taifa Stars yameremeta, yaitungua Gambia 2-1

MABAO yaliyofunga na mabeki Shomari Kapombe na Erasto Nyoni katika kipindi cha pili leo yameiwezesha timu ya Taifa, Taifa Stars kuichapa Gambia mabao 2-1 katika mechi ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za 2014 iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kapombe aliifungia Stars bao la kusawazisha dakika ya 60 baada ya kuunganisha wavuni kwa kichwa mpira wa krosi uliopigwa kutoka pembeni ya uwanja kabla ya Nyoni kufunga bao la pili na ushindi kwa njia ya penalti baada yaa beki mmoja wa Gambia kuunawa mpira ndani ya eneo la hatari.
Ushindi huo umeiwezesha Stars kushika nafasi ya pili katika kundi C ikiwa na pointi tatu baada ya kucheza mechi mbili, nyuma ya Ivory Coast inayoongoza kwa kuwa na pointi nne. Morocco ni ya tatu kwa kuwa na pointi mbili wakati Gambia inashika mkia kwa kuwa na pointi moja.

Katika mechi nyingine ya kundi hilo iliyochezwa jana mjini Casablanca, Ivory Coast ilitoka sare ya mabao 2-2 na Morocco.

Stars, ambayo katika mechi ya kwanza ilifungwa 2-0 na Ivory Coast mjini Abidjan, ilicheza hovyo kipindi cha kwanza, lakini kuingia kwa Haruna Moshi ‘Boban’, aliyechukua nafasi John Bocco ‘Adebayor’ kipindi cha pili, kuliifanya icheze kwa kasi na kulitia misukosuko lango la Gambia na hatimaye kupata mabao hayo mawili.
Gambia ilikuwa ya kwanza kupata bao lililofungwa na Mamadou Ceesay dakika ya nne.

No comments:

Post a Comment