KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, June 20, 2012

Mrembo wa Miss Dar Inter College kupatikana kesho

WASHIRIKI 14 wa shindano la Miss Dar Inter College 2012 kesho wanatarajiwa kupanda ulingoni kuwania taji hilo katika shindano litakalofanyika kwenye ukumbi wa Makumbusho, Dar es Salaam.
Mratibu wa shindano hilo, Dina Ismal alisema mjini Dar es Salaam juzi kuwa, maandalizi yanakwenda vizuri na kila mrembo amepania kuibuka na ushindi.
Kwa mujibu wa Dina, leo warembo hao wanatarajiwa kuhudhuria onyesho la bendi ya Twanga Pepeta International litakalofanyika kwenye ukumbi wa klabu ya Billicanas, Dar es Salaam.
Dina alisema wamejipanga kuhakikisha kuwa, shindano la mwaka huu linakuwa na mvuto na ubora wa kiwango cha juu ili kuwapata warembo wenye sifa zinazotakiwa.
“Mwaka huu tumejipanga vema kuhakikisha mmoja wa warembo kutoka Miss Dar Inter College anafanya vema katika fainali za Miss Tanzania,” alisema Dina.
Warembo watakaoshiriki shindano hilo wanatoka vyuo vya Biashara (CBE), Uandishi wa Habari (DSJ) na Time, Ustawi wa Jamii, Usimamizi wa Fedha (IFM) na Chuo Kikuu Huria (OUT). Taji hilo kwa sasa linashikiliwa na Rose Msuya kutoka IFM.
Warembo watakaopanda stejini kesho kuwania taji hilo ni Veronica Ngota, Rose Muchunguzi, Nancy Maganga, Hilda Edward, Diana Nyakisinda, Neema Michael, Veronica Yollla, Jacqueline Cliff, Sharifa Ibrahim, Natasha Deo, Saada Suleiman, Rose Masanja na Jamila Hassan.
Shindano hilo litapambwa kwa burudani mbalimbali, ikiwemo ya msanii nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Nassib Abdul ‘Diamond’ na bendi mpya ya muziki wa dansi ya Skylight.
Wadhamini wa shindano hilo ni Redd’s Premium, Dodoma Wine, Ndege Insurance, Skylight Band, Screen Masters, Makumbusho ya Taifa, Mustafa Hassanali, Shear Illusions, Lamada Hotel, Grand Villa Hotel, Clouds Media Group na blogu za Michuzi, Dina Ismail, BIN ZUBEIRY, Mtaa kwa Mtaa na Full Shangwe.

No comments:

Post a Comment