KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 14, 2012

Hussein Jumbe ampokonya sare Buyungwa stejini

KIONGOZI wa bendi ya muziki wa dansi ya Talent, Hussein Jumbe mwishoni mwa wiki iliyopita alitoa kioja cha mwaka baada ya kuvamia onyesho la bendi ya WK Sound na kumnyang’anya sare mwanamuziki wake.
Tukio hilo lililoshuhudiwa na mwandishi wa habari hizi, lilitokea Jumapili iliyopita wakati bendi ya WK Sound ilipokuwa ikifanya onyesho kwenye ukumbi wa Pile Bar uliopo Temeke, Dar es Salaam.
Mara baada ya kuingia ukumbini saa nne usiku, Jumbe alipanda stejini na kusimamisha muziki huku akimtaka mpiga tumba wa WK Sound, Buyungwa Iddi ampatie sare zake.
“Wewe si mwanamuziki wangu, tena uliondoka bila kuaga, nipatie sare zangu,” Jumbe alisikika akimweleza Buyungwa, ambaye alijiunga na WK Sound akitokea bendi ya Talent.
Ilibidi Mkurugenzi wa WK Sound, Mama Pile aingilie kati na kumtaka Jumbe atumie busara kuwasilisha madai yake kwa Kuyunga na kumweleza kuwa, kitendo alichokifanya hakikuwa cha kistaarabu.
“Wewe ni mwanamuziki mkongwe na wa siku nyingi, hatukutegemea ufanye kitu kama hiki, tena mbele ya umati wa watu kama huu,”Mama Pile alimweleza Jumbe.
Hata hivyo, Jumbe hakuwa tayari kusikiliza ushauri wa mama huyo zaidi ya kusisitiza Kuyunga ampatie sare zake mara moja. Ilibidi Buyungwa aingie kwenye chumba cha wanamuziki na kumpatia sare hizo Jumbe.
Baadhi ya wateja waliokuwemo ukumbini wakati huo, walionekana kukerwa na tukio hilo na kusikika wakimweleza Jumbe kuwa, kitendo alichokifanya hakikuwa cha kiungwana.
Wateja hao, baadhi yao walisikika wakimweleza Jumbe kuwa, alipohama Mlimani Park Orchestra na Msondo Ngoma, aliondoka na sare za bendi hizo, lakini viongozi wake hawakumsumbua.
Akizungumzia tukio hilo, Buyungwa ambaye aliwahi pia kuwa mpiga tumba wa bendi ya Msondo Ngoma alisema, lilimsikitisha kwa vile hakutegemea iwapo Jumbe angeweza kumfanyia kitendo kile.
“Ni kweli mimi niliondoka Talent Band bila kumuaga Jumbe, lakini lengo langu lilikuwa kutafuta maisha kwa sababu pesa za Jumbe kutoka kwake ni kwa manati, hazina kiwango maalumu, chochote atakachokitoa mfukoni ndicho hicho hicho, sitarajii kurudi tena,”alisema.

Buyungwa alikiri kuchelewa kumrejeshea sare hizo Jumbe, lakini alisema siku ya tukio alikwenda nazo ukumbini akiamini kwamba lazima angezifuata kutokana na mazungumzo waliyoyafanya kwa njia ya simu siku chache zilizopita.
Jumbe hakuwa tayari kuzungumzia tukio hilo kwa vile alionekana kuwa mtu mwenye hasira.

No comments:

Post a Comment