KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, June 22, 2012

LULU: Nilidanganya umri kuipa hadhi filamu



MAMA mzazi wa msanii wa filamu Elizabeth Michael 'Lulu', Lucresia Kalugila, amedai kitendo cha mwanawe kutamka mbele ya umma kwamba ana umri wa zaidi ya miaka 18, kililenga kuipa hadhi filamu yake.
Alidai pia kwamba mtoto huyo, alifanya hivyo ili kuepuka unyanyapaa ambao ulikuwa ukifanywa dhidi yake na wasanii wenzake katika sanaa ya filamu wakimwelezea kuwa ni mtoto.
Lucresia alidai hayo kupitia hati ya kiapo majibu aliyoiwasilisha Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, akikana mwanae kuwa na umri wa zaidi ya miaka 18.
Hati hiyo ya majibu iliwasilishwa jana mahakamani hapo, mbele ya Jaji Dk. Fauz Twaib na mawakili Kenneth Fungamtama, Peter Kibatala na Flugence Massawe, wanaomwakilisha Lulu.
Mawakili hao waliwasilisha hati hiyo ya majibu baada ya Jamhuri kuwasilisha ushahidi wa CD ya mahojiano ya Lulu na mtangazaji Zamaradi Mketema, maelezo yake aliyoyatoa polisi, maombi ya hati ya kusafiria na leseni ya udereva.
Katika ushahidi huo wa Jamhuri inaonekana muombaji (Lulu) wa kufanyiwa uchunguzi kuhusu utata wa umri wake akisema ana miaka zaidi ya 18.
Kwa mujibu wa hati ya majibu ya mzazi wake Lulu, ameapa kwamba mwanae majina yake ni Elizabeth Michael Kimemeta na Diana Elizabeth Michael Kimemeta na siyo Diana Michael Kimemeta.
Mama huyo, pia amedai kuwa alimuliza Lulu sababu za kusema ana umri zaidi ya miaka 18 wakati si kweli ambapo alimjibu alifanya hivyo ili kuweza kuipa hadhi filamu yake.
Akifafanua, alidai Lucresia anaamini kwamba kama mwanawe angepewa msaada wa kisheria pamoja na wa wawazi kuwepo wakati akihojiwa polisi akiwa katika wakati mgumu na mwenye msongo wa mawazo, angeweza kusema umri wake sahihi ambao ni miaka 17.
Mama huyo amedai kwamba anaamini kuwa Lulu kutokana utoto wake, alitoa matamko ya uongo ili aweze kupata hati ya kusafiria la leseni ya udereva na kwamba si kweli amezaliwa Aprili 17, mwaka 1991 kama alivyoeleza. Amedai angekuwa kazaliwa tarehe hiyo angekuwa na miaka 21 kitu ambacho si kweli.
Lulu anayekabiliwa na kesi hiyo, iliyopo Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, aliwasilisha maombi katika Mahakama Kuu ya kufanywa uchunguzi wa umri wake.
Jaji Dk. Twaib amepanga kusikiliza maombi hayo baada ya pande zote kuwasilisha ushahidi wao, Jumatatu wiki ijayo.

No comments:

Post a Comment