KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, June 17, 2012

Twiga Stars bye bye

TIMU ya soka ya taifa ya wanawake, Twiga Stars jana ilitolewa katika michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Afrika za 2012 baada ya kuchapwa bao 1-0 na Ethiopia katika mechi ya marudiano iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kipigo hicho kiliifanya Twiga Stars itolewe kwa jumla ya mabao 3-1, kufuatia kuchapwa mabao 2-1 katika mechi ya awali iliyochezwa wiki tatu zilizopita mjini Addis Ababa.

Dalili za Twiga Stars kuzidiwa na Ethiopia zilianza kuonekana mapema kutokana na wachezaji wa timu hiyo kishindwa kucheza kwa uelewano na pia kutocheza kwa mfumo unaoeleweka.

Kibaya zaidi, wachezaji wa Twiga Stars walionekana kutokuwa na nguvu na pia walichoka mapema na kutoa mwanya kwa wapinzani wao kutawala sehemu kubwa ya mchezo huo.

Washambuliaji Asha Mwalala na Mwanahamisi Omari walijaribu kucheza gonga za hapa na pale, lakini tatizo kubwa lilikuwa umaliziaji wa pasi za mwisho.

Baadhi ya mashabiki waliohojiwa na blogu ya liwazozito baada ya mchezo huo walionyesha wasiwasi wao kwa Kocha Charles Boniface kuwa umekuwa mdogo kutokana na kushindwa kutoa maelekezo yoyote kwa wachezaji wake uwanjani.

Mashabiki hao walisema kocha huyo amezoeana mno na wachezaji kiasi kwamba inawezekana kwa sasa wamekuwa hawamuheshimu kutokana na kuwa nao karibu mno. Wamelitaka Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kumtafuta kocha mpya kwa ajili ya timu hiyo na wamemtaja Rogasiun Kaijage, ambaye aliwahi kuifundisha kwa muda na kuiletea mafanikio makubwa.

No comments:

Post a Comment