KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 23, 2013

NGASA: SIKUONGEZA MKATABA SIMBA



MSHAMBULIAJI nyota nchini, Mrisho Ngasa mwanzoni mwa wiki hii alirejea rasmi katika klabu yake ya zamani ya Yanga baada ya kutia saini mkataba wa miaka miwili. Ngasa amerejea Yanga akitokea Simba, ambayo aliichezea kwa mkopo wa mwaka mmoja baada ya kuuzwa na Azam.

Katika makala hii ya ana kwa ana iliyoandikwa na ATHANAS KAZIGE, mshambuliaji huyo anaelezea mambo mbalimbali kuhusu mustakabali wake kisoka.

SWALI: Ni sababu ipi iliyokufanya uamue kurejea Yanga ukitokea Simba? Huoni kwamba utashusha kiwango chako kutokana na kuhama mara kwa mara?

JIBU: Niliichezea Simba kwa mkopo nikitokea Azam, ambayo ndiyo niliyokuwa na mkataba nayo. Yanga ilianza kunifuatilia miezi sita iliyopita, tukazungumza na kufikia makubaliano ndio sababu nimeamua kuondoka Simba.

Ukweli ni kwamba nina mapenzi makubwa na ya dhati kwa Yanga na ninachoweza kusema ni kwamba namshukuru Mungu kwa kuweza kupata nafasi hii. Ninawaomba viongozi na wachezaji wa Yanga wanipe ushirikiano wa kutosha ili niweze kutimiza malengo yangu.

SWALI: Ulipohama Yanga na kujiunga na Azam, 2009 uliondoka kwa mapenzi yako ama kulikuwa na shinikizo lolote kutoka kwa viongozi wa zamani wa klabu hiyo.

JIBU: Niliamua kuhamia Azam kwa mapenzi yangu mwenyewe kwa lengo la kutafuta maisha mazuri. Hakuna mtu yeyote aliyenishinikiza nifanye hivyo. Unajua mimi bado ni kijana na ninaendelea kupambana na maisha kwa ajili ya siku zijazo.

Kilichotokea ni kwamba, baada ya kutua Azam, nikagundua kwamba kuna baadhi ya mambo, ambayo kwa upande wangu hayakunifurahisha na niliyaona kama kikwazo.Nilipata wakati mgumu kuweza kutekeleza majukumu yangu. Nisingependa kuzungumza kiundani kuhusu suala hilo.

SWALI: Vipi ulipokuwa ukiichezea Simba kwa mkopo, kuna matatizo yoyote uliyokumbana nayo?

JIBU: Nilikwenda Simba kwa hiari yangu, nikiwa na lengo lingine la kutafuta maisha. Kilichotokea ni kwamba hawakuwa na imani na mimi. Kilichotokea ni kama ilivyokuwa kwa Azam. Lakini niliichezea kwa uwezo wangu wote kwa sababu mpira ndiyo kazi yangu.

SWALI: Hebu eleza kiundani, ni kwa nini viongozi wa Simba na Azam hawakuwa na imani na wewe?

JIBU: Tatizo kubwa lilikuwa likijitokeza wakati wa maandalizi ya mechi dhidi ya Yanga. Viongozi wa Simba na Azam walionekana kutokuwa na imani na mimi, sielewi kwa nini!

Kingine kilichokuwa kikionekana kuwakera viongozi wa Simba na Azam ni kuona mashabiki wa Yanga wakinishangilia na mimi kuonyesha mapenzi yangu kwao.

Lakini binafsi nilijitahidi kucheza kwa uwezo wangu wote kwa lengo la kuwaonyesha kwamba, mawazo yao yalikuwa tofauti na ukweli wa mambo ulivyo.

Kama ulivyoona, katika mechi ya mwisho kati ya Simba na Yanga, niliweza kufanya juhudi kubwa na hatimaye kuipatia Simba penalti iliyopigwa na Mussa Mudde, lakini alikosa.

SWALI: Hivi ni kwa nini ulikataa ofa ya kwenda kucheza soka ya kulipwa katika klabu ya El-Merreikh ya Sudan wakati ilikuwa tayari kukulipa fedha nyingi?

JIBU: Si kweli kwamba nilikataa ofa ya kwenda kucheza soka ya kulipwa Sudan. Kilichotokea ni kwamba viongozi wa Simba na Azam walianza kujichanganya kuhusu klabu ipi iliyostahili kulipwa ada ya uhamisho. Klabu zote mbili zilitaka kuniuza bila kuzungumza na mimi.

Hivi katika ulimwengu wa sasa, kuna mchezaji yeyote anayeweza kukataa kulipwa pesa nyingi kama zilizoahidiwa na El-Merreikh? Kama yupo, atakuwa mtu wa ajabu. Mimi nilikataa kwenda Sudan kwa sababu niliona kuna ujanja ulikuwa unataka kufanyika.

Kwa jumla ninachoweza kusema kwa sasa ni kwamba, namshukuru Mungu nimemaliza salama mkataba wangu wa mkopo Simba na sasa nipo huru. Kiwango changu kilipanda sana nilipokuwa Simba. Niliifungia mabao mengi na kutoa pasi zilizozaa mabao. Soka ndiyo kazi yangu.

SWALI: Kwa maana hiyo siyo kweli kwamba ulikuwa ukicheza chini ya kiwango ulipokuwa Simba na Azam kwa lengo la kuzihujumu?

JIBU: Hicho kitu kisingewezekana kabisa kwangu. Nilichokuwa nikikifanya ni kutimiza wajibu wangu. Ninapaswa kuheshimu mkataba kati yangu na klabu yoyote. Mchezo wa soka ndio ulionifikisha hapa nilipo.

SWALI: Unaweza kueleza ni kwa nini ulipokuwa Azam kiwango chako kilikuwa cha chini tofauti na ulipojiunga na Simba, ambapo ulionyesha kiwango cha juu?

JIBU: Sina jibu la swali hilo kwa sababu mimi nilijiona nacheza katika kiwango changu cha kawaida. Lakini ni kweli kwamba, nilicheza vizuri zaidi nilipokuwa Simba kwa sababu nilipata ushirikiano mzuri kutoka kwa wachezaji wenzangu. Na nilikumbana na upinzani mkali kutoka kwa wachezaji wa timu pinzani.

SWALI: Je, ni kweli kwamba ulishatia saini mkataba mwingine na Simba kabla ya ligi kumalizika?

JIBU: Sikuwahi kuongeza mkataba mwingine na Simba kwa sababu nilikuwa na mkataba na Azam. Kule nilikwenda kucheza kwa mkopo. Sielewi kwa nini viongozi wa Simba wananizulia uongo huo. Mkataba wangu na Simba ulishamalizika na nimekubali kurejea Yanga kutokana na kupata ofa nzuri.

SWALI: Kabla ya kuzichezea Yanga, Azam na Simba, uliwahi kuzichezea timu za Toto African na Kagera Sugar. Umejifunza nini kutokana na kuzichezea timu zote hizo?

JIBU: Ninachoweza kusema ni kwamba nimejifunza mambo mengi sana,kuanzia kwa viongozi, wanachama na mashabiki wa soka nchini. Wanasoka wa Tanzania wanakwamishwa na mambo mengi.

Pengine tatizo kubwa linalowaathiri wachezaji wa Tanzania ni kutotimiziwa haki zao ipasavyo na viongozi wa klabu. Ni vyema kila upande utimize wajibu wake, vinginevyo soka ya Tanzania itaendelea kudumaa.

Binafsi nisingekuwa makini wakati wa kuingia mikataba na klabu, nadhani hivi sasa ningekuwa kwenye matatizo makubwa. Pengine ningekuwa nahangaika kule Sudan huku wanaofaidika kupitia mgongo wangu ni wengine kabisa. Nawaomba wanasoka wenzangu wawe makini kuhusu suala la mikataba.

SWALI: Iwapo utapata nafasi nyingine ya kwenda kucheza soka ya kulipwa nje hivi sasa, utakuwa tayari kufanya hivyo?

JIBU: Nipo tayari kwenda kufanyiwa majaribio nje wakati wowote, lakini itabidi nipate baraka za viongozi wa Yanga kwa vile tayari nimeshaingia nao mkataba wa miaka miwili.

No comments:

Post a Comment