KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 23, 2013

MOYES AANZA KIBARUA MAN UNITED



LONDON, England
KOCHA Mkuu mpya wa Manchester United, David Moyes mwanzoni mwa wiki hii alianza kazi katika klabu hiyo, ikiwa ni siku 43 kabla ya tarehe rasmi ya kutakiwa kufanya hivyo.

Moyes (50) aliwasili kwenye uwanja wa mazoezi wa klabu hiyo uliopo Carrington, Jumatatu iliyopita kabla ya saa 3.20 asubuhi kwa ajili ya kuanza maisha mapya ndani ya Old Trafford.

Kocha huyo wa zamani wa Everton anatakiwa kuanza rasmi kibarua cha kuinoa Manchester United, Julai Mosi mwaka huu, akichukua nafasi ya Sir Alex Ferguson. Ametia saini mkataba wa miaka sita.

Ferguson alikuwa miongoni mwa watendaji wa Manchester United waliompokea Moyes baada ya kuwasili Carrington pamoja na mtendaji mkuu aliyemaliza muda wake, David Gill.

Ujio wa Moyes kwenye uwanja wa Carrington ulipokelewa kwa mshangao mkubwa na wafanyakazi wachache wa uwanja huo kwa vile hawakumtarajia. Ilikuwa ni siku ya mapumziko.

Ferguson alimtambulisha Moyes kwa wafanyakazi hao na kumtembeza kwenye maeneo mbalimbali ya uwanja huo kabla ya kufanya naye mazungumzo kwa saa moja kwenye ofisi za kocha huyo.

Kocha huyo mpya wa Manchester United pia alipata nafasi ya kuzungumza na baadhi ya maofisa wa benchi la ufundi, akiwemo kocha wa makipa, Eric Steele. Alitarajia kukutana na kocha msaidizi namba mbili, Mike Phelan juzi asubuhi.

Katika mazungumzo yake na maofisa hao, Moyes aliwaeleza kuwa anatarajia kutangaza mabadiliko atakayoyafanya kwenye kikosi cha timu hiyo kesho.

Kocha huyo pia alizungumza na bosi wa kituo cha vijana cha klabu hiyo, Brian McClair na baadhi ya wasaidizi wake wakati walipokuwa wakijiandaa kucheza mechi ya fainali ya ligi kuu kwa timu za vijana wa chini ya miaka 21 dhidi ya Tottenham.

Katika mechi hiyo, vijana wa Manchester United walikuwa nyuma kwa mabao 2-0 kabla ya kuzinduka na kuibuka na ushindi wa mabao 3-2.

Hakukuwa na nafasi yoyote kwa Moyes kutoa hotuba kwa maofisa wa klabu hiyo. Ilikuwa ni nafasi yake ya kutembelea mazingira mapya kabla ya kuanza kibarua cha kuinoa timu hiyo.

Moyes alikaa kwenye uwanja huo kwa saa tatu kabla ya kuondoka kwa kutumia gari aina ya Chevrolet 4x4 lililokuwa likiendeshwa na mtunza vifaa wa klabu hiyo, Albert Morgan.

Baadaye kocha huyo wa zamani wa Everton aliongozana na Ferguson katika sherehe za kuwazawadia makocha wa ligi kuu ya England, ambapo Ferguson alitangazwa kuwa kocha bora wa mwaka.

Moyes alikanusha madai kuwa, aliandaliwa mapema na Ferguson kwa ajili ya kurithi mikoba yake. Alisema hizo zilikuwa hisia kwa vile wapo makocha wengi waliokuwa wakitajwa kumrithi Ferguson kama vile Roy Keane, Mark Hughes na Steve Bruce.

Hata hivyo, Moyes alieleza kuvutiwa kwake na Ferguson na kumwelezea kuwa ni kocha bora duniani.

Swali kubwa, ambalo mashabiki wa soka wa Manchester United wamekuwa wakijiuliza ni iwapo Moyes ataweza kufuata nyayo za Ferguson, ambaye alidumu kwenye klabu hiyo kwa miaka 27 na kuiwezesha kutwaa mataji lukuki.

Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya soka wamemuelezea Moyes kuwa, anafanana kwa kiasi fulani kiutendani na Ferguson ndiyo sababu bodi ya wakurugenzi ya klabu hiyo ilimpa kipaumbele kuliko makocha wengine.

Watu walio karibu na Moyes wanaamini kuwa, ana uwezo wa kuiongoza klabu hiyo kwa utaratibu ule ule uliokuwa ukitumiwa na Ferguson na pia kama alivyofanywa kwa Everton katika kipindi cha miaka 11 iliyopita.

Chanzo cha habari kimeeleza kuwa, Moyes amechangia kwa kiasi kikubwa kumshawishi beki Rio Ferdinand kuongeza mkataba wa mwaka mmoja kwa ajili ya kuichezea Manchester United msimu ujao.

Baadhi ya wachezaji wa Manchester United wamesema wapo tayari kukabiliana na changamoto mpya kutoka kwa Moyes baada ya kuanza kuinoa timu hiyo.

Moyes alizaliwa Aprili 25, 1963. Ni raia wa Scotland. Aliwahi kushinda tuzo za kocha bora wa mwaka wa England, 2003, 2005 na 2009.

Aliwahi kuwa mchezaji wa klabu ya Celtic ya Scotland na kuichezea katika mechi 540 akiwa beki wa kati. Pia amewahi kuzichezea klabu za Dunfermline Athletic na Preston North End.

Alianza kazi ya ukocha katika klabu ya Preston, akiwa kocha msaidizi kabla ya kupandishwa na kuwa kocha mkuu 1998.

Aliteuliwa kuwa kocha wa Everton 2002 na chini yake ilifuzu kucheza michuano ya ligi ya mabingwa wa Ulaya 2005 na kufuzu kucheza fainali ya Kombe la FA 2009.

Wakati wa sherehe za kutimiza miaka 10 katika klabu hiyo, Moyes alipokea pongezi nyingi kutoka kwa makocha wenzake, wakiwemo Ferguson, Arsene Wenger na Kenny Dalglish kutokana na mafanikio yake.

Moyes ni kocha wa tatu katika historia ya ligi kuu ya England kudumu kwenye klabu moja kwa miaka mingi, akiwa nyuma ya Ferguson na Wenger.

Kocha huyo mpya wa Manchester United anao watoto wawili, mmoja wa kike na mwingine wa kiume. Baba yake, David Sr ni mfuatiliaji wa vipaji vya wachezaji katika klabu ya Everton. Mama yake, Joan anafanyakazi katika duka la nguo.

No comments:

Post a Comment