KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Saturday, August 26, 2017

STAND UNITED YAPATA MKATABA WA MILIONI 100 KUTOKA BIKO



Wakati pazia la Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara 2017-2018 likitarajiwa kufunguliwa rasmi kesho Agosti 27, mwaka huu kwa timu zote 16 kuingia viwanjani,Kampuni ya Michezo ya Bahati Nasibu Mtandaoni – BIKO imeidhamini Klabu ya Stand United ‘Chama la Wana’ shilingi milioni 100 kuanzia mwaka huu.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika leo Ijumaa,Agosti 25,2017mjini Shinyanga, Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini Mheshimiwa Stephen Masele (CCM) alisema BIKO wameamua kuidhamini timu hiyo baada ya kuridhishwa na mwenendo wa timu hiyo.
“Baada ya Stand United kupoteza mwelekeo na wadhamini wake Kampuni ya Acacia kujiondoa katika udhamini,hivi sasa nimeamua kuwa msimamizi mkuu wa timu hii,nimetafuta udhamini mwingine,nimeiomba kampuni ya Kitanzania ya BIKO,imekubali kuwa wadhamini wakuu na imetupatia shilingi milioni 100 kwa mwaka huu”,alieleza Masele.
Mbunge huyo alisema ameamua kuwa msimamizi mkuu wa timu hiyo ili kuhakikisha kuwa timu hiyo inafanya vyema katika michezo mbalimbali.

“Najua mnaelewa uhusika wangu katika Stand United,mnafahamu jitihada nilizofanya kuhakikisha timu hii inafanya vizuri,ili timu hii iwe ya kimataifa na timu hii baada ya kupata matatizo yaliyotokea,ilikuwa kama timu yatima,haina ulezi,haina msaada,na mimi kama mbunge nilikuwa nimekasirika na nikasema Maeja na wenzake wasinisumbue katika mambo ya mpira”,alisema.
“Nilitafuta ufadhili wa shilingi bilioni 2.4 kutoka Acacia,lakini tuliuchezea,na baada ya kujiridhisha na uongozi mpya ulioingia ukiongozwa na Dk. Maeja nimetafuta wadhamini wengine ambao ni kampuni ya BIKO ili kuisadia timu yetu,naomba fedha hizi zitumike vizuri”,alisema Masele.

Masele alitumia fursa hiyo kuwatahadharisha viongozi wa timu kuhusu matumizi mabaya na ubadhirifu wa fedha zilizotolewa na wadhamini hao na kuwa hawatasita kuwachukulia hatua kali za kisheria.
“BIKO itapenda kuona fedha hizi zinatumikaje na kuanzia sasa mtu yeyote atakayejihusisha na ubadhirifu tutamfikisha katika vyombo vya sheria kwa sababu wanaumiza hisia za watu wengi”,aliongeza Masele.
“Nataka niwahikikishie kuwa timu hii haitashuka daraja kinatochotakiwa ni kutoa msaada kwa timu hii ikiwemo kuishangilia,jambo jingine naomba mjitahidi kubana matumizi katika masuala mbalimbali ikiwemo pale mnaposafiri punguzeni idadi ya watu wa kusafiri lakini pia lipeni mishahara ambayo haiumizi sana”,aliongeza.
Kwa upande wake,Mwenyekiti wa Klabu ya Stand United,Dkt. Ellyson Maeja alisema Klabu hiyo ya Stand United imejipanga vizuri kuhakikisha kuwa inafanya vizuri katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara 2017-2018.

“Hivi sasa timu imetulia kiuongozi tatizo ni bajeti,mpira ni pesa,bila pesa hakuna timu,lakini pia hatuna usafiri wala hosteli kwa ajili ya wachezaji,tunaomba wadau waendelee kujitokeza kuisaidia timu hii,tumesajili wachezaji wapya 19,jumla sasa wapo 30,tunaye kocha mzuri,walimu wazuri,malengo yetu ni kushika nafasi ya kwanza hadi ya tatu katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu huu wa 2017-2018?,alisema Dkt.Maeja.

No comments:

Post a Comment