KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, August 31, 2017

MAYANGA AMWONGEZA EMMANUEL MARTIN KIKOSI CHA TAIFA STARS



Kocha Mkuu wa timu ya Mpira wa Miguu ya Tanzania ‘Taifa Stars’, Salum Mayanga amemwongeza Kiugo wa Young Africans, Emmanuel Martin kwenye kikosi chake kinachojindaa kucheza na Botswana Jumamosi Septemba 2, mwaka huu.

Mchezo huo wa kirafiki wa kimataifa utakaofanyika kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam chini ya utaratibu wa kalenda ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).

Emmanuel Martin anatarajiwa kujiunga na kambi ya Taifa Stars mara moja leo Agosti 30, mwaka huu na kuanza na mazoezi na wenzake yatakayofanyika jioni kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Emmanuel Martin ameongezwa na Mayanga baada ya mawasiliano kuonesha kwamba huenda akawakosa nyota wa kimataifa Simon Msuva kutoka Difaa El Jadidah ya Morocco na Orgenes Mollel wa FC Famalicao ya Ureno.

Taarifa kutoka Morocco inaonesha kwamba Msuva ana kibali cha muda cha kuingia na kutoka Morocco ‘visa’ ambacho kinamnyima haki ya kutoka na kuingia Morocco mara kwa mara.

Kuna juhudi zinafanywa na timu yake kadhalika Shirikisho la Mpira wa Miguu la Morocco kumfanikishia kupata kibali cha muda mrefu ili iwe rahisi kwa mchezaji kutoka na kuingia kama anahitaji katika timu ya taifa.

Kuhusu Mollel taratibu za ruhusa za kimataifa zinafanyiwa kazi kwa mujibu wa sheria za nchi ya Ureno ambako anacheza soka la kulipwa.

Nyota wengine wote wameripoti Taifa Stars wakiwamo wale wa kutoka nje ya mipaka ya Tanzania kama vile Mbwana Samatta (KRC Genk/Ubelgiji), Elias Maguli (Dhofar FC/Oman), Abdi Banda (Baroka FC/Afrika Kusini), Hamis Abdallah (Sony Sugar/Kenya) wakati Farid Mussa wa CD Tenerif ya Hispania anatarajiwa kutua leo.

Wengine ambao wako kambini Hoteli ya Sea Scape iliyoko Kunduchi, Dar es Salaam ni makipa Aishi Manula (Simba SC), Mwadini Ally (Azam FC) na Ramadhani Kabwili (Young Africans).

Pia wamo Walinzi ni Gadiel Michael (Young Africans), Boniphas Maganga (Mbao FC), Kelvin Yondani (Young Africans), Salim Mbonde (Simba SC) na Erasto Nyoni (Simba SC).

Viungo ni Himid Mao – Nahodha Msaidizi (Azam FC), Mzamiru Yassin (Simba SC), Said Ndemla (Simba SC), Shiza Kichuya (Simba SC), wakati Washambuliaji ni Raphael Daud (Young Africans) na Kelvin Sabato (Azam FC).

Benchi la Ufundi la Mayanga linaundwa na yeye mwenyewe ambaye ni Kocha Mkuu, Fulgence Novatus (Kocha Msaidizi), Patrick Mwangata (Kocha wa Makipa), Danny Msangi (Meneja), Dkt. Richard Yomba (Daktari wa timu), Dkt. Gilbert Kigadye (Daktari wa Viungo) na Ally Ruvu (Mtunza Vifaa).

No comments:

Post a Comment