KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, April 19, 2010

MKE WA JOHN TERRY ATAKA TALAKA



LONDON, England
BEKI na nahodha wa timu ya soka ya Taifa ya England, John Terry wiki hii alikumbwa na mapigo mawili mazito, likiwepo la mkewe, Toni Poole kutimkia Dubai akiwa na watoto wao wawili.
Pigo lingine lililomkumba mchezaji huyo wa klabu ya Chelsea ya England ni tishio la mpenzi wake wa zamani, Vanessa Perroncel kuanika hadharani kila kitu kuhusu uhusiano wao wa kimapenzi na uja uzito alionao.
Toni ameamua kuondoka kwenye jumba lao lenye thamani ya pauni milioni nne, akiwaeleza rafiki zake kwamba anataka kutengana na Terry, kufuatia kubainika kwa uhusiano wa kimapenzi kati yake na Vanessa.
Vanessa ni mpenzi wa zamani wa mchezaji Wayne Bridge, aliyecheza pamoja na Terry katika kikosi cha Chelsea kabla ya kuhamia klabu ya Manchester City. Mwanadada huyo pia alikuwa rafiki wa karibu wa zamani wa Toni.
Mtu mmoja wa karibu na Toni alilieleza gazeti la Daily Mail la Uingereza kuwa, mama huyo wa watoto wawili aliamua kwenda Dubai mwishoni mwa wiki iliyopita.
Kwa mujibu wa mtu huyo, Toni alikwenda Dubai akiwa na watoto wake mapacha wawili aliozaa na Terry pamoja na wazazi wake wote wawili. Terry na Toni waliwahi kwenda fungate Arabuni mwaka 2007 baada ya kufunga ndoa.
Imeelezwa kuwa, Terry alifikia makubaliano na Vanessa waitoe mimba hiyo Jumatatu iliyopita baada ya mpenzi huyo wa zamani wa Bridge kupata uja uzito.
Msemaji wa Vanessa, Max Clifford alisema bosi wake huyo amechoshwa na taarifa zinazoripotiwa kuhusu uhusiano wake na Terry na kwamba sasa anataka kuanika ukweli hadharani.
Clifford ambaye alimtembelea Vanessa nyumbani kwake Jumatatu usiku alisema, mpenzi huyo wa zamani wa Bridge amepanga kuweka mambo hadharani baada ya kufikiria hatma ya mtoto wake wa kiume mwenye umri wa miaka minne.
Vanessa amezaa na Bridge mtoto mmoja wa kiume kabla ya kutengana na mchezaji huyo baada ya kuhamia klabu ya Manchester City.
“Amechanganyikiwa kutokana na kilichotokea,”alisema Clifford. “Amekuwa akijiuliza: ‘Nimefanya nini?’ Waandishi wa habari wanagonga mlango wa nyumba yangu mara kwa mara, watu wamekuwa wakikimbizana kuchukua picha zangu kila mahali ninapokwenda. Kamwe sikufikiria hili, sikupenda litokee na sikuwahi kuzungumza na mtu yeyote.”
Msemaji huyo alisema Vanessa amekuwa akijiuliza maswali mengi kuhusu tukio hilo, ikiwa ni pamoja na mustakabali wake iwapo ataamua kuzungumza na vyombo vya habari ama asipofanya hivyo. Baadhi ya wanasoka wa England wametaka Terry avuliwe unahodha wa timu ya taifa ama ajiuzulu kutokana na kukumbwa na kashfa hiyo ya aina yake.
Waziri wa Michezo wa Uingereza, Gerry Sutcliffe alisema wiki hii kuwa, atakiomba Chama cha Soka cha nchi hiyo kutoa ufafanuzi kuhusu tukio hilo.
Gerry alisema tuhuma zilizomkumba Terry zinaitia doa nafasi ya mchezaji huyo kama nahodha wa England. “Ndani ya uwanja, John Terry ni mchezaji wa aina yake na nahodha mzuri wa England, lakini kuwa nahodha wa England, unatakiwa kuwa na majukumu mapana kwa nchi na ni wazi kwamba, iwapo tuhuma hizi zitathibitika, itabidi kufikiria kuhusu nafasi yake kama nahodha wa England,” alisema.
Juhudi za Terry kuzima sakata hilo ziligonga mwamba mwishoni mwa wiki iliyopita baada ya Jaji wa Mahakama Kuu kutengua uamuzi wa kutaka habari hizo zisitangazwe kwenye vyombo vya habari.
Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya soka wamesema, kitendo cha Terry kimekigawa kikosi cha England, baadhi ya wachezaji wakitaka avuliwe unahodha na kuondolewa kwenye timu.
Kuna imani kwa baadhi ya mashabiki kwamba, Terry amesababisha pigo kubwa kwa nafasi ya England kufanya vizuri katika fainali za mwaka huu za Kombe la Dunia, zinazotarajiwa kufanyika nchini Afrika Kusini.
Wakati Toni (28) alipoondoka na familia yake kwenda Dubai, aliwaeleza rafiki zake: “Amekuwa
akinifanyia matendo maovu kwa zaidi ya miaka kumi. Lakini sasa hakuna zaidi. Safari hii nitaomba talaka.”
Chanzo cha habari kilicho karibu na Terry kimesema, mchezaji huyo amekuwa akiendelea kukanusha kwa mkewe kwamba, hakuwa mwaminifu kwake.
Terry alianzisha uhusiano wa kimapenzi na Vanessa baada ya Bridge, waliyekuwa wakiishi katika eneo moja, kusajiliwa na Manchester City na kuhamia katika kitongoji cha Cheshire na kumuacha mpenzi wake huyo, ambaye ni mama wa mtoto wake akibaki kwenye nyumba yao ya zamani.
Vanessa aliripotiwa kupata uja uzito wiki chache baadaye na rafiki zake walisema taratibu za kuitoa zilipangwa na Terry na kufanyika kwenye kliniki moja binafsi Oktoba mwaka jana.
Vanessa aliripotiwa kufika kwenye kliniki hiyo kwa kupitia mlango wa nyuma na operesheni
ilicheleweshwa ili kumwezesha Terry kuishuhudia baada ya mazoezi na timu yake ya Chelsea.
Baada ya Toni kupata taarifa hizo, aliamua kumpigia simu Vanessa na kumshutumu kuhusu kitendo chake cha kujihusisha kimapenzi na mumewe.
“Kulikuwa na majibizano makali kati yao, lakini Vanessa alikanusha kuwa na uhusiano wa kimapenzi na Terry,” kilisema chanzo cha habari.
Chanzo kingine kilisema, Toni alimweleza Vanessa: “ Unajiita rafiki? Ni aina gani ya rafiki anayelala na waume wa rafiki zake?”
Terry analipa mshahara wa pauni 170,000 kwa wiki na thamani yake inakadiriwa kufika pauni milioni 25, akiwa pia na mikataba ya matangazo mbalimbali.
Iwapo maombi ya Toni kutaka talaka yatakubaliwa, atalipwa kitita kikubwa cha fedha kwa vile
anaruhusiwa kisheria kumiliki nusu ya utajiri wa mumewe.
Habari zaidi zimeeleza kuwa, Bridge aliwaeleza rafiki zake wiki hii kwamba, hataendelea kuichezea England iwapo Terry atabaki kuwa nahodha wa timu hiyo.
Wachezaji wenzake wengine wa timu hiyo wamemjia juu Terry wakimwelezea kuwa ni mtovu wa
adabu na kitendo chake hicho hakiwezi kusamehewa.
Mmoja wa wachezaji hao alisema, hawezi kutumia chumba kimoja cha kubadilishia mavazi na Terry wakati wachezaji wa Manchester City wameeleza wazi kumuunga mkono Bridge katika sakata hilo.
Nahodha msaidizi wa zamani wa England, Rio Ferdinand na kiungo, Frank Lampard wa Chelsea
walimpigia simu Bridge kumueleza kwamba wanamuunga mkono.
Kocha Mkuu wa England, Fabio Capello ameripotiwa kuwa, anataka kulitafutia ufumbuzi sakata hilo kabla ya upangaji wa ratiba ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Ulaya za mwaka 2012. Ratiba ya michuano hiyo inatarajiwa kupangwa Jumapili mjini Warsaw, Poland.
Capello amemuomba mmoja wa wasaidizi wake, Franco baldini kukutana na Terry pamoja na Bridge na kujadiliana nao kuhusu suala hilo.
Lakini chanzo cha habari kutoka ndani ya Chama cha Soka cha England kimeeleza kuwa, huenda
Capello akafikia uamuzi wa kumvua unahodha Terry.
“Terry anahitaji kuvuliwa unahodha na kuondolewa kwenye kikosi cha England na hiyo itasaidia
kusafisha hali ya hewa,” kilisema chanzo hicho. “Hana tena nafasi ya kucheza katika fainali za Kombe la Dunia.”
Bridge na Terry hawakuwa tayari kuzungumzia sakata hilo wiki hii. Wachezaji hao wawili wanatarajiwa kukutana ana kwa ana Februari 27 mwaka huu wakati Chelsea itakapomenyana na Manchester City katika ligi kuu ya England.
Mbali na tukio hilo, Terry pia amekuwa akidaiwa kuwa na uhusiano wa kimapenzi na wanawake
wengine wanne. Wanawake hao ni Karina Clarke, Linsey Dawn McKenzie, Nicola Ulian na Lauren Pope.


MATUKIO MBALIMBALI YA JOHN TERRY
Novemba 1999: Alikuwa na uhusiano wa kimapenzi kwa miezi mitano na mwanamitindo maarufu wa England, Jayne Connery (42). Wakati huo, Terry alidaiwa kwamba hakuwa na mke, lakini tayari alishamchumbia Toni.
Machi 2002: Msichana mrembo Nicola Ulian (27) alionekana akiingia kwenye hoteli ya Terry wakati Chelsea ilipocheza na Liverpool wakati wa uhusiano wao wa kimapenzi uliodumu kwa miezi mitano.
Septemba 2003: Terry alijihusisha kimapenzi na mwanamitindo Rebecca Ryan (18) wakati England ilipoweka kambi kwenye hoteli moja mjini Manchester kwa ajili ya michuano ya fainali za Ulaya za mwaka 2004. Binti huyo alidai kuwa, walifanya mapenzi mchana kutwa.
Januari 2004: Alionekana akimpiga busu hadharani mwanamitindo Linsey Dawn Mckenzie.
Juni 2004: Mpiga picha za ngono maarufu Karina Clarke (29), alidai kuwa, aliwahi kufanya mapenzi na Terry wakati mwanamitindo, Emma Kearney (31) alidai kuwa, mchezaji huyo alikuwa na kawaida ya kufanya ngono kwa fujo.
Novemba 2004: Alianzisha uhusiano wa kimapenzi uliodumu kwa miezi sita na mwanamitindo, Lauren Pope.
Aprili 2005: Lianne Johnson (21), alidai kuwa, alifanya ngono na Terry kwenye choo cha klabu moja ya usiku, japokuwa alikuwa amevunjika mguu na kutembelea magongo.
Septemba 2005: Alikuwa na uhusiano wa kimapenzi kwa miezi miwili na Shalimar Wimble (36). Terry alikuwa akitumia nyumba ya Wayne Bridge kufanya ngono na mwanamke huyo.
Novemba 2005: Jenny Barker (17) alisema alifanya onyesho la ngono kwa ajili ya Terry kwenye gari lake.
Januari 2006: Mwanamitindo Alicia Douvall alidai kuwa, alifanya ngono mara kadhaa na Terry wakati mkewe Toni alipokuwa mja mzito.
Septemba 2009: Alianzisha uhusiano wa kimapenzi na mpenzi wa zamani wa Wayne Bridge, Vanessa Perroncel.

No comments:

Post a Comment