KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, September 11, 2017

SIMBA, AZAM HAKUNA MBABE


KLABU Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, imetoka sare ya bila kufungana dhidi ya Simba katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) uliofanyika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Huo ni mchezo wa kwanza wa kihistoria kwa timu hiyo kuweza kucheza katika uwanja wake wa nyumbani dhidi ya Simba, ambao ulitawaliwa kwa ubabe kwa pande zote mbili huku Refari akionesha kadi za njano kama jungu.

Ulikuwa ni mchezo wa kugawana vipindi, ambapo Azam FC ilionekana kutawala kipindi cha pili huku wapinzani wao wakitawala kipindi cha kwanza na pande zote zikikosa mabao.

Winga wa Azam FC, Enock Atta, alipiga shuti la umbali dakika ya 18 lilidakwa na kipa wa timu hiyo, Aishi Manula, ambaye alikuwa akirejea kwa mara ya kwanza Azam Complex tokea asajiliwe na Simba msimu huu akitokea kwa mabongwa hao,

Wachezaji wengine waliokuwa wakirejea ndani ya viunga hivyo, ni gwiji wa Azam FC John Bocco ‘Adebayor’ na Erasto Nyoni, waliosajiliwa pia wakitokea kwa mabingwa hao wa Afrika Mashariki na Kati.

Dakika ya 33 Atta alimsetia pasi nzuri Yahaya Mohammed, alliyeingia na mpira huo ndani ya eneo la 18 lakini shuti alilopiga lilitoka sentimita chache ya lango na kuufanya mchezo huo kumaliza kipindi cha kwanza kwa suluhu hiyo.

Mabadiliko yaliyofanywa na benchi la ufundi la Azam FC ya kumuingiza kiungo Frank Domayo na kupumzishwa Atta yaliiongezea ubora timu hiyo kwenye eneo la kiungo hali iliyowafanya kutawala mchezo huo.

Dakika ya 63 Azam FC ilipata pigo baada ya beki wake wa kulia, Daniel Amoah, kuumia na nafasi yake kuchukuliwa na Ramadhan Singano ‘Messi’, mabadiliko hayo yalimlazimu nahodha Himid Mao, kuhamia beki wa kulia  na eneo la kiungo kubakia Stephan Kingue, Domayo na Salum Abubakar ‘Sure Boy’.

Dakika 10 za mwisho za mchezo huo, Yahaya Mohammed na Sure Boy, almanusura waipatie mabao Azam FC, lakini shuti alilopiga kiungo huyo lilitoka sm chache ya lango na kichwa alichopiga Yahaya kiliweza kudakwa na kipa.

Sare hiyo inaifanya Azam FC kupata pointi moja na kufikisha jumla ya pointi nne ikisogea hadi nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi hiyo sawa na Tanzania Prisons na Simba zilizokuwa juu yake kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa.

Mara baada ya mchezo huo, kikosi cha Azam FC kitapumzika kesho Jumapili kabla ya kurejea mazoezini Jumatatu jioni tayari kabisa kujiandaa na mtanange ujao dhidi ya Kagera Sugar, utakaofanyika Uwanja wa Azam Complex Septemba 15 saa 1.00 usiku.

No comments:

Post a Comment