KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, December 8, 2013

TANZANITE YAPIGWA 4-1 NA AFRIKA KUSINI



TIMU ya soka ya Taifa ya wanawake ya vijana wa chini ya miaka 20, Tanzanite imejiweka kwenye mazingira magumu ya kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia baada ya kuchapwa mabao 4-1 na Afrika Kusini.
Katika mechi hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Tanzanite ilicheza hovyo tangu mwanzo wa mchezo na kuwakatisha tamaa mashabiki waliofurika kwenye uwanja huo.
Iliwachukua Afrika Kusini dakika nne kuhesabu bao la kwanza lililofungwa na Amogelang Motay kabla ya Tanzanite kusawazisha dakika ya 13 kupitia kwa Theresa Yohana.
Afrika Kusini iliendeleza kasi ya mchezo na kufanikiwa kuongeza bao la pili dakika ya 17 kupitia kwa Shiwe Nogwanya. Timu hizo zilikwenda mapumziko Afrika Kusini ikiwa mbele kwa mabao 2-1.
Mabao mengine ya Afrika Kusini yalifungwa na Mosili Makhoali, dakika ya 61 na 78.
Timu mbili hizo zinatarajiwa kurudiana wiki mbili zijazo mjini Johannesburg. Ili isonge mbele, Tanzanite itahitaji ushindi wa mabao 4-0.
Kocha wa Tanzanite, Rogasiun Kaijage alikiri baada ya mchezo huo kuwa, vijana wake walizidiwa kimchezo na Afrika Kusini.
Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Vijana, Michezo na Utamaduni, Fenella Mukangara aliwataka wachezaji wa Tanzanite kuacha kulia, badala yake wawe jasiri na kujiandaa vyema kushinda mechi ya marudiano.
Alisema Tanzanite ilicheza vizuri kutokana na maandalizi iliyoyafanya, lakini wapinzani wao walicheza vizuri zaidi ndio sababu waliibuka na ushindi.

No comments:

Post a Comment